Weka Miradi ya Kiroho
1 Litakuwa pendeleo kubwa kama nini kumsifu Yehova milele! Ili kutusaidia tufikie mradi huo, twaweza kuweka miradi mingine ya kiroho ya wakati huu na kufanya bidii kuifikia. Kufanya hivyo kwatuwezesha kutumia nguvu zetu kwa hekima. (1 Kor. 9:26) Unaweza kutimiza miradi gani kwa urahisi?
2 Funzo la Biblia: Je, wewe hujitayarisha kwa ajili ya kila mkutano wa kutaniko? Ikiwa ndivyo, je, unatumia wakati kufanya utafiti na kutafakari unapojifunza? Kwa mfano, unapotayarisha Funzo la Mnara wa Mlinzi na Funzo la Kitabu la Kutaniko, je, wewe hupiga tu mistari kwenye majibu au unasoma maandiko yaliyowekwa hapo na pia kutafakari sababu za maelezo yanayotolewa? Je, unaweza kuweka mradi wa kufanya utafiti wa mambo machache kutokana na usomaji wa Biblia wa kila juma katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi? Utafiti huo wa kiroho huhitaji muda na jitihada, lakini huleta matokeo mazuri.—Mit. 2:4, 5.
3 Mikutano ya Kutaniko: Mradi mwingine ni kuhudhuria mikutano yote mitano ya kutaniko kwa ukawaida. Kufika mapema na kushirikiana na waamini wenzetu na kushiriki katika wimbo na sala ya kufungua husaidia kuimarisha hali ya kutaniko. Pia twaweza kujitahidi kutoa maelezo kwenye kila mkutano na kujitahidi kuboresha maelezo yetu. Labda unaweza kueleza jinsi andiko katika fungu linavyohusiana na mazungumzo au unaweza kueleza jinsi ambavyo habari hiyo inatumika katika maisha ya kila siku.—Ebr. 10:24, 25.
4 Utumishi wa Shambani: Huduma yetu huwa bora zaidi tunapoweka miradi. Je, una mradi wa saa unazopanga kutumia shambani kila mwezi? Wengine wamefaidika kwa kufanya hivyo. Au je, unaweza kuboresha sehemu fulani ya huduma yako, kama vile kutumia Biblia katika utumishi wa nyumba kwa nyumba, kufanya ziara za kurudia zenye mafanikio, kujitahidi kuanzisha funzo la Biblia, au kufundisha mafunzo kwa njia yenye matokeo zaidi?
5 Wazazi, je, mnawatia moyo watoto wenu waweke miradi katika utumishi wa Yehova? Wasaidieni kuona kwamba kutumikia wakiwa mapainia au washiriki wa familia ya Betheli ni njia nzuri zaidi ya kuonyesha shukrani zao nyingi kwa Yehova.—Mhu. 12:1.
6 Tunapochunguza shughuli zetu, kuweka miradi ya kiroho, na kujitahidi kuifikia, tutapata shangwe kubwa katika utumishi na kuwatia moyo wengine.—Rom. 1:12.