Iweni Timamu Katika Akili Mwisho Unapokaribia
1 Neno la Mungu husema tena na tena kwamba siku ya Yehova itakuja “kama mwizi,” yaani, kwa ghafula, mara moja, na bila onyo. (1 The. 5:2; Mt. 24:43; 2 Pet. 3:10; Ufu. 3:3; 16:15) “Kwa sababu hiyo,” Yesu alisema, “jithibitisheni wenyewe kuwa tayari, kwa sababu kwenye saa msiyoifikiri kuwa hiyo, Mwana wa binadamu anakuja.” (Mt. 24:44) Tunawezaje kuwa macho kiroho kadiri mwisho unavyokaribia? Tutafanikiwa tukifuata maneno haya yaliyoandikwa kwa mwongozo wa Mungu: “Iweni timamu katika akili.”—1 Pet. 4:7.
2 Kuwa timamu katika akili kwahusisha kuona mambo kama Yehova anavyoyaona. (Efe. 5:17) Hutusaidia kujiona kuwa “wakaaji wa kigeni na wakazi wa muda” katika mfumo huu wa mambo. (1 Pet. 2:11) Hutuwezesha kufahamu mambo yaliyo ya maana kabisa, kuamua mambo ya kutanguliza, na kufanya maamuzi mazuri.—Flp. 1:10.
3 Weka Miradi ya Kiroho: Kuweka na kutimiza miradi ya kiroho hutusaidia kuwa timamu katika akili. Je, una miradi ya kiroho unayojitahidi kutimiza? Je, unajitahidi kusoma Biblia kila siku, kuhudhuria mikutano yote ya Kikristo, kusoma kila toleo la Mnara wa Mlinzi na Amkeni!, au labda kuhubiri zaidi? Ukiweka miradi inayokufaa, uazimie kuitimiza, na kumwomba Yehova abariki jitihada zako, utapata matokeo mazuri ajabu.
4 Mzee mmoja aliwauliza wenzi wa ndoa vijana kuhusu miradi yao ya kiroho. Swali hilo liliwafanya watambue kwamba wangeweza kuwa mapainia iwapo wangefanya maisha yao kuwa sahili na kulipa deni kubwa walilokuwa nalo. Waliamua kuweka mradi huo. Walijitahidi kulipa deni hilo na kutafuta njia za kupunguza mambo yasiyo ya lazima yaliyokuwa yakichukua wakati wao na nguvu zao. Baada ya mwaka mmoja tu, walitimiza mradi wao. Matokeo yakawaje? Mume anasema hivi: “Kama hatungekuwa na miradi, hali yetu ingekuwa tofauti. Tuna furaha na utulivu zaidi. Maisha yetu yana kusudi halisi.”
5 Tunapongoja siku ya Yehova, na tuendelee kuwa macho kiroho kwa kuishi kwa utimamu wa akili, na kufanya mapenzi ya Mungu bila kukengeushwa.—Tito 2:11-13.