Msaada kwa Wakati Unaofaa
1 Mtume Petro aliwaimarisha na kuwapa vikumbusha na kitia-moyo cha upendo waamini wenzake kwa sababu aliwajali. (2 Pet. 1:12, 13; 3:1) Aliwahimiza ‘wale ambao walipata imani’ waendelee kukuza sifa za kiroho ili wasiwe “ama wasiotenda ama wasiozaa matunda kuhusu ujuzi sahihi juu ya Bwana wetu Yesu Kristo.” (2 Pet. 1:1, 5-8) Petro alitaka kuwasaidia wafanye wito na kuchaguliwa kwao na Yehova kuwa hakika ili ‘wapatikane wakiwa bila doa na bila waa na katika amani.’ (2 Pet. 1:10, 11; 3:14) Waamini wengi waliona kitia-moyo hicho kuwa cha wakati unaofaa.
2 Vivyo hivyo, waangalizi Wakristo leo wanawajali watu wa Mungu. Katika ‘nyakati hizi za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,’ watumishi wengi wa Yehova wanalazimika kukabili hali ngumu. (2 Tim. 3:1) Kwa sababu ya matatizo yasiyoisha ya kiuchumi, ya familia, au ya kibinafsi, huenda wengine wakahisi kama Daudi: “Mabaya yasiyohesabika yamenizunguka mimi. Maovu yangu yamenipata, wala siwezi kuona. Yamezidi kuliko nywele za kichwa changu, na moyo wangu umeniacha.” (Zab. 40:12) Mikazo hiyo inaweza kuwalemea sana watu hao na kuwafanya wapuuze mambo muhimu ya kiroho na kuacha kushiriki huduma ya Kikristo. Hata hivyo, ‘hawajasahau maagizo ya Yehova’ licha ya matatizo yao. (Zab. 119:176) Huu ndio wakati unaofaa kwa wazee kuwasaidia watu hao wanaohitaji msaada.—Isa. 32:1, 2.
3 Ili kutimiza mgawo huo, wazee wametiwa moyo wafanye jitihada ya pekee kuwasaidia wale ambao sasa wameacha kuhubiri. Jitihada kubwa ya kuwasaidia imeanza na itaendelea hadi mwezi wa Machi. Waangalizi wa mafunzo ya kitabu wanaombwa wawatembelee wasiotenda na kuwasaidia kiroho ili warudie tena utendaji wao kutanikoni. Funzo la Biblia la kibinafsi laweza kupangwa kukiwa na uhitaji. Huenda wengine wakaombwa wasaidie. Ukiombwa kusaidia, jitihada zako zinaweza kufaidi sana, hasa ukitoa kitia-moyo kwa fadhili na kwa ufahamu.
4 Sote tunapaswa kufurahi mtu anaporudia tena utendaji wake kutanikoni. (Luka 15:6) Jitihada zetu za kuwatia moyo wasiotenda zinaweza kuwa “neno linenwalo wakati wa kufaa.”—Mit. 25:11.