Mpango Mpya wa Maktaba za Majumba ya Ufalme
Kwa miaka mingi, makutaniko ulimwenguni pote yamenufaika na maktaba za Majumba ya Ufalme, ambazo hapo zamani ziliitwa maktaba ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Hapo awali, ilionwa kuwa lazima kila kutaniko liwe na maktaba yake. Hata hivyo, kwa sababu Majumba mengi ya Ufalme yanatumiwa na makutaniko zaidi ya moja, mengine yakiwa makutaniko ya lugha za kigeni, yaelekea kwamba itafaa kuwe na maktaba moja tu kwa ajili ya kila lugha katika kila Jumba la Ufalme. Maktaba hizo zinapaswa kuwa na vitabu vyote, kutia ndani vile vya karibuni. Katika Majumba ya Ufalme yaliyo na ukumbi zaidi ya mmoja, kila ukumbi wapaswa kuwa na maktaba kwa ajili ya kila lugha ya makutaniko yanayokutania hapo.
Tunatazamia kwamba mpango huu utasaidia kuokoa nafasi na kupunguza gharama. Isitoshe, maktaba za makutaniko mawili au zaidi zikiwekwa pamoja huenda ikafanya maktaba hiyo moja iwe bora zaidi. Maktaba hizo zinapowekwa pamoja, vitabu vya ziada vyaweza kuhifadhiwa na kutumiwa baadaye wakati Majumba ya Ufalme mapya yatakapojengwa. Iwapo kuna kompyuta yenye Watchtower Library iliyo na CD-ROM kwenye Jumba la Ufalme, wengine watafaidika sana na kifaa hicho.
Kwa kila maktaba ya Jumba la Ufalme, ndugu mmoja, hasa ikiwezekana mmoja wa waangalizi wa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, atawekwa kutunza maktaba. Anapaswa kuongeza vitabu vinavyofaa kwenye maktaba, na kuandika vizuri ndani ya jalada kwamba kitabu hicho ni cha maktaba ya Jumba la Ufalme. Angalau mara moja kwa mwaka, anapaswa kuhakikisha kwamba vitabu vyote vya maktaba vipo navyo ni nadhifu. Vitabu vya maktaba hizi havipasi kuondolewa kwenye Majumba ya Ufalme.
Maktaba za Majumba ya Ufalme zinathaminiwa sana na washiriki wote wa kutaniko. Kwa hivyo, wazee wahakikishe kwamba washiriki wote wa kutaniko wanaweza kutumia maktaba za Majumba ya Ufalme. Sote na tuonyeshe kwamba tunathamini maktaba hizo kwa kuzitunza na kuzitumia ili “kupata kumjua Mungu.”—Mit. 2:5.