Ziara za Kurudia Huongoza Kwenye Mafunzo ya Biblia
1 Yesu aliamuru wanafunzi wake wahubiri na pia ‘kufanya wanafunzi na kuwafundisha.’ (Mt. 28:19, 20) Mhubiri hutangaza ujumbe, lakini mwalimu hufanya mengi zaidi. Yeye hufundisha, hueleza, na kuthibitisha mambo. Njia moja ya kuwafundisha watu ni kuwarudia waliopendezwa tukiwa na kusudi la kuanzisha mafunzo ya Biblia.
2 Unapaswa kuwarudia akina nani? Hakikisha unawarudia wote waliokubali vichapo au wale wanaopendezwa na habari njema hata kwa kadiri ndogo. Ukimkuta mtu anayependezwa unapohubiri mahali pa umma, jaribu kumwomba anwani au namba yake ya simu ili usitawishe upendezi wake. Uwe na maoni yanayofaa kuhusu kuanzisha mafunzo ya Biblia. Endelea kuwatafuta wale watakaokubali funzo la Biblia, na yaelekea utawapata.—Mt. 10:11.
3 Pendezwa Nao Kibinafsi: Matayarisho ya ziara za kurudia zenye matokeo huanza kwenye ziara ya kwanza. Wahubiri wenye matokeo hutambua mambo yanayompendeza mwenye-nyumba, nao huyatumia kuwa msingi wa mazungumzo zaidi. Wengine hupata matokeo kwa kuuliza swali mwishoni mwa ziara ili kuamsha hamu ya mwenye-nyumba kwa ajili ya mazungumzo yatakayofuata. Kupendezwa kikweli na watu hutufanya tuendelee kuwafikiria hata baada ya kuondoka nyumbani mwao, na pia hutusukuma kurudi bila kukawia. Ikiwezekana, jaribu kurudi kama wangali wanapendezwa—labda baada ya siku moja au mbili.
4 Unapofanya ziara ya kurudia, jitahidi kuendeleza mazungumzo ya wakati uliopita. Uwe na lengo la kumfunza angalau jambo moja la Kimaandiko la kumjenga kila mara, na uwe tayari kusikiliza. Jaribu kumfahamu zaidi mwenye-nyumba. Kisha kwenye ziara zitakazofuata, mfundishe kweli za Neno la Mungu ambazo zinalenga mahangaiko yake.
5 Tafuta Fursa za Kuanzisha Mafunzo ya Biblia: Fanya ziara za kurudia ukiwa na lengo la kuanzisha funzo la Biblia. Wawezaje kufanya hivyo? Mtajie kwamba ungependa kumwonyesha jambo moja lenye kupendeza, kisha umwonyeshe fungu moja ambalo unafikiri litampendeza katika kitabu Ujuzi au broshua Anataka. Soma fungu hilo, uliza swali na uzungumzie andiko moja au mawili yaliyotajwa. Waweza kufanya hivyo kwa dakika tano au kumi ukiwa mlangoni au langoni. Malizia kwa kuuliza swali la fungu lifuatalo na upange kuendeleza mazungumzo wakati mwingine.
6 Kusitawisha upendezi tunaopata ni muhimu katika huduma yetu. Kwa hiyo, tenga wakati kila juma ili ufanye ziara za kurudia. Utapata matokeo zaidi na shangwe katika huduma yako ukifanya hivyo.
[Maswali ya Funzo]
1. Kwa nini ni muhimu kufanya ziara za kurudia?
2. Tunapaswa kuwarudia akina nani?
3, 4. Ziara za kurudia zenye matokeo zinahusisha nini?
5. Ni njia gani rahisi inayoweza kutumiwa kuanzisha mafunzo ya Biblia?
6. Tutaonyeshaje kwamba tunaelewa umuhimu wa kufanya ziara za kurudia?