Kuhubiri Katika Ulimwengu Unaozidi Kubadilika
1 Mambo hubadilika haraka kama nini! Kwa ghafula, msiba wa asili, msukosuko wa kiuchumi na wa kisiasa, au janga kubwa laweza kuwa habari kuu ya mazungumzo. Lakini punde si punde, fikira za watu hugeukia mambo mengine. (Mdo. 17:21; 1 Kor. 7:31) Katika ulimwengu huu unaozidi kubadilika, tunawezaje kuvuta fikira za watu ili wasikilize ujumbe wa Ufalme?
2 Tambua Mambo Yanayowahangaisha Watu: Njia moja ya kuvuta fikira za watu ni kwa kutaja matukio ya hivi karibuni. Pindi moja alipokuwa akiwahimiza wasikilizaji wake wafikirie kwa uzito kuhusu uhusiano wao na Mungu, Yesu alitaja misiba ya karibuni ambayo walikuwa wanakumbuka. (Luka 13:1-5) Vivyo hivyo, tunapohubiri habari njema, itafaa tutumie tukio la hivi karibuni ambalo linawahusu watu katika eneo letu. Hata hivyo, tunapozungumzia mambo hayo, lazima tuwe waangalifu tusiunge mkono masuala ya kisiasa au ya kijamii.—Yoh. 17:16.
3 Tunawezaje kujua mambo ambayo watu wanafikiria sasa? Labda njia bora zaidi ni kuwauliza swali kisha kusikiliza jibu lao. (Mt. 12:34) Kupendezwa na watu kutatuchochea tufikirie maoni yao na kuuliza maswali zaidi kwa busara. Maelezo ya mwenye nyumba yanaweza kuonyesha jambo linalowahangaisha watu wengi katika eneo na hilo laweza kufungua njia ya kutoa ushahidi.
4 Kutayarisha Utoaji: Tunapojitayarisha kushiriki utumishi wa shambani katika ulimwengu unaozidi kubadilika, twaweza kutumia kitabu Kutoa Sababu. Madokezo yanayofaa kuhusu kutumia matukio ya karibuni katika utoaji wetu yanapatikana katika ukurasa wa 12-13, chini ya kichwa “Matukio ya Sasa” na “Uhalifu/Kutopatwa na Madhara.” Habari zaidi yaweza kupatikana katika Huduma Yetu ya Ufalme ya Septemba 2000, ukurasa wa 4. Unapotayarisha utoaji wako, hakikisha kwamba unatia ndani andiko moja linalofaa.
5 Tunapoona mahangaiko mbalimbali ya watu katika eneo letu, twahitaji kubadili utoaji wetu wa habari njema kupatana na hali zao. Tukifanya hivyo, tutakuwa tukiongea na watu kuhusu mambo yaliyo mioyoni mwao. Kwa njia hiyo, tunawasaidia watu wengi zaidi wamjue Yule ambaye sifa na kanuni zake hazibadiliki.—Yak. 1:17.