“Iweni Tayari”
1 Katika unabii wake mkuu kuhusu umalizio wa huu mfumo wa mambo, Yesu alionya kuhusu kuhangaikia sana mambo ya kawaida ya maisha. (Mt. 24:36-39; Luka 21:34, 35) Kwa kuwa dhiki kuu inaweza kuanza wakati wowote, ni lazima tutii onyo hili la Yesu: “Iweni tayari, kwa sababu Mwana wa binadamu atakuja katika saa msiyofikiria.” (Mt. 24:44) Ni nini kinachoweza kutusaidia kufanya hivyo?
2 Kupambana na Mahangaiko na Vikengeusha-Fikira: Mojawapo ya mitego ya kiroho ambayo lazima tujilinde nayo ni “mahangaiko ya maisha.” (Luka 21:34) Katika nchi fulani, umaskini, ukosefu wa kazi, na gharama za juu za maisha hufanya iwe vigumu kupata mahitaji ya lazima ya maisha. Katika nchi nyingine, kurundika mali ni jambo la kawaida. Tukianza kufikiria sana vitu vya kimwili tutashindwa kukazia fikira mambo ya Ufalme. (Mt. 6:19-24, 31-33) Mikutano ya Kikristo hutusaidia kuendelea kukazia fikira mambo ya Ufalme. Je, una lengo la kuhudhuria kila mkutano?—Ebr. 10:24, 25.
3 Leo ulimwengu umejaa vikengeusha-fikira ambavyo vinaweza kutupotezea wakati muhimu sana. Kutumia kompyuta kunaweza kuwa mtego ikiwa mtu anatumia Internet kwa saa nyingi mno, anasoma na kutuma barua-pepe, au anacheza michezo ya kompyuta kwa saa nyingi. Tunaweza kupoteza wakati mwingi tukitazama televisheni, sinema, kufanya mambo tunayopenda, kusoma vitabu vya kilimwengu, na kushiriki michezo huku tukibaki na wakati na nguvu kidogo tu za kufanya mambo ya kiroho. Ingawa burudani na starehe zinaweza kutuburudisha kidogo, funzo la Biblia la kibinafsi na la familia huleta faida za milele. (1 Tim. 4:7, 8) Je, wewe hununua wakati wa kutafakari Neno la Mungu kila siku?—Efe. 5:15-17.
4 Twaweza kushukuru sana kwamba tengenezo la Yehova limefanya mipango ya mafundisho ya kiroho ya kutusaidia tupate ‘kufanikiwa kuponyoka mambo yote yaliyokusudiwa kutukia, na kusimama mbele ya Mwana wa binadamu’! (Luka 21:36) Na tufaidike kabisa na mipango hiyo ya kiroho na ‘tuwe tayari’ ili imani yetu ipate kuwa “sababu ya sifa na utukufu na heshima wakati wa ufunuo wa Yesu Kristo.”—1 Pet. 1:7.