Mtumikie Yehova Bila Kukengeuka-Fikira
1 “Heri [wenye furaha ni, NW] watu wenye BWANA kuwa Mungu wao”! (Zab. 144:15) Je! maneno hayo ya Mfalme Daudi yangali ya kweli, hata katika siku hizi zenye uovu? (Efe. 5:16) Ndiyo! Wakristo bado hupata shangwe katika kumtumikia Yehova. Hali si rahisi kwetu sikuzote. Shetani hutusababishia magumu katika “nyakati [hizi] za hatari,” hata hivyo hatushuki moyo. (2 Tim. 3:1, 2) Hali zinazozidi kuwa mbaya ni ithibati zaidi kwamba wakati u karibu ambapo Ufalme wa Mungu utaondolea mbali ulimwengu huu mbovu wa zamani na kuweka ulimwengu mpya ulio safi mahali pao. (2 Pet. 3:13) Giza la ulimwengu huu halififishi wala kuzima mwali wa tumaini letu la furaha; badala ya hivyo, tumaini letu la Ufalme huangaza kwa nguvu zaidi. Je! hufurahi kuwa wamtumikia Yehova ukiwa mmulikaji katika ulimwengu huu wenye giza?—Flp. 2:15.
2 Tukiwa watu mmoja-mmoja, ni lazima tuwe macho daima kuhusu jinsi tunavyomtumikia Yehova. Kwa nini? Kwa sababu Shetani ni Mkengeusha-Fikira mkuu. Kamusi moja hufasili neno “kengeusha-fikira” kuwa “kugeuza kando,” “kuvuta au kuelekeza (fikira za mtu) kwenye kitu tofauti au mahali tofauti-tofauti wakati uleule,” na “kufadhaisha au kuvuruga kwa hisiamoyo au madhumuni yenye kupingana.” Tangu avurumishwe chini hadi dunia hii, Shetani amefanikiwa katika ‘kuwaongoza vibaya’ wanadamu. Yeye hutumia hila nyingi za kugeuza fikira za mwanadamu kutoka kwenye masuala ya kweli ya siku yetu. (Ufu. 12:9, NW) Ingawa Mashahidi wa Yehova wamejikakamua wenyewe katika kuhubiri Ufalme kwa miaka mia moja ambayo imepita, ni watu wangapi wanaothamini yale masuala ya maana zaidi juu ya utakasaji wa jina la Mungu na kutetewa kwa enzi kuu yake kupitia Ufalme wa Mungu? Ni wachache kwa kulinganisha. (1 Yoh. 5:19) Ikiwa Shetani aweza kuwakengeusha-fikira mabilioni ya watu juu ya dunia hii, hatari iliyopo sikuzote ni kwamba yeye aweza kutukengeusha-fikira au kukamata uangalifu wetu ili tuache utumishi wa Yehova. Kwa kuhuzunisha, baadhi ya ndugu zetu wamevurugwa na vikengeusha-fikira vya Shetani. Wameruhusu akili zao zivutwe kuelekea mahali tofauti-tofauti. Kuna aina nyingi mbalimbali za vikengeusha-fikira leo. Fikiria chache tu kati yazo.
3 Matatizo ya Kiuchumi na Kupenda Vitu vya Kimwili: Katika nchi nyingi duniani, ukosefu wa kazi za kuajiriwa na gharama za juu za maisha husababisha mahangaiko. Ni kweli, ni lazima tujiandalie wenyewe na familia zetu chakula, mavazi, na makao. Lakini tukijiruhusu kuwa wenye kuhangaikia mno mahitaji ya maisha, mahangaiko hayo yatatawala fikira zetu. Kusalimika kwetu kimwili kwaweza kuwa jambo la maana zaidi maishani kuliko kutegemeza kwetu suala la Ufalme. Mtume Paulo alitoa shauri kuhusiana na jambo hilo kwenye Waebrania 13:5, 6. Yesu Kristo atuhakikishia kwamba wale wanaoutafuta Ufalme kwanza hawahitaji kuhangaika; Yehova huandaa yale tunayohitaji kwelikweli. (Mt. 6:25-34) Mapainia na watumishi wengine wa wakati wote kotekote ulimwenguni waweza kuhakikisha kwamba hilo ni kweli.
4 Ulimwengu wa Shetani huendeleza hali ya kupenda vitu vya kimwili. Kupata mali zaidi au kuzilinda ndiyo kani yenye nguvu maishani mwa mamilioni ya watu. Vikengeusha-fikira kama hivyo vilikuwako katika siku za Yesu. Mtawala tajiri mchanga alimuuliza Yesu yale aliyohitaji kufanya ili kurithi uhai wa milele. Yesu alijibu hivi: “Ukitaka kuwa mkamilifu [au, kamili], enenda ukauze ulivyo navyo, uwape maskini, nawe utakuwa na hazina mbinguni; kisha njoo unifuate.” (Mt. 19:16-23) Kwa wazi, mali zake nyingi zilimkengeusha-fikira kijana huyo asimtumikie Mungu kwa moyo wote. Moyo wake uligeuzwa kuelekea mali zake. Yesu alijua kwamba kijana huyo angenufaika ikiwa angejiondolea mzigo wa kulemea wenye kukengeusha-fikira hivyo. Vilimzuia asiwe kamili katika utoaji wake kwa Mungu. Namna gani wewe? Je! wewe hujipata mwenyewe ukitumia wakati mwingi zaidi katika kazi ya kimwili ili tu kudumisha mtindo-maisha ambao umezoea? Je! hilo limeathiri utumishi wako kwa Yehova? Je! mali zako za kimwili zinachukua wakati wote wa masilahi ya Ufalme? (Mt. 6:24) Je! waweza kurahisisha maisha yako ili kutumia wakati mwingi zaidi kwa masilahi ya kiroho?
5 Mambo ya Kawaida ya Kila Siku: Tusipokuwa waangalifu, twaweza kushughulikia sana mambo ya kawaida ya maisha hivi kwamba twaanza kupuuza mambo ya kiroho. Kumbuka watu wa siku za Noa. Wao walishughulikia sana mambo ya kijamii, kula na kunywa, kuoa na kuoza watoto wao, hivi kwamba hawakutambua ujumbe wa Noa wenye kuonya juu ya Gharika iliyokuwa ikija. Kabla ya wao kung’amua, Gharika ilikuja na kuwafagilia mbali. Vikengeusha-fikira vilimaanisha uharibifu kwao. Yesu alisema hivi: “Ndivyo kutakavyokuwa kuja [kuwapo, NW] kwake Mwana wa Adamu.” (Mt. 24:37-39) Kwa kweli, watu walio wengi wanashughulikia sana maisha yao wenyewe wasiweze kutolea uangalifu ule ujumbe wenye kuonya tunaowaletea. Wao huonyesha kutojali kabisa mambo ya kiroho.
6 Je! maisha yako yamejawa sana na utendaji mbalimbali wa kijamii hivi kwamba mambo ya kiroho yanazidi kutolewa uangalifu uliopungua zaidi? Katika pindi moja, Yesu alialikwa nyumbani mwa Martha na Mariamu. Mariamu alikuwa akisikiliza kwa makini yale ambayo Yesu alikuwa akisema. Kwa upande ule mwingine, Martha “alikuwa akihangaika kwa utumishi mwingi.” Martha alihangaikia mno kuwa mkaribishaji mzuri. Alishindwa kuthamini uhitaji wa kuchukua wakati wa kumsikiliza Yesu. Yesu alimwonyesha Martha kwa fadhili kwamba maandalizi yenye madoido hayakuhitajika; uangalifu zaidi wapasa kutolewa mambo ya kiroho. Je! wewe wahitaji kutumia shauri hilo? (Lk. 10:38-42) Yesu alionya pia kwamba ni lazima tujiangalie wenyewe tusije tukala kupita kiasi wala kunywa kileo kingi mno, na kudhoofisha hisi zetu. Katika wakati huu wa hatari wa historia ya kibinadamu, tunahitaji kuwa macho kikamili.—Lk. 21:34-36.
7 Ufuatiaji wa Anasa: Kimojapo vikengeusha-fikira vikubwa zaidi ambavyo Ibilisi hutumia kuvuta uangalifu kutoka kwenye suala la Ufalme ni ufuatiaji wa anasa. Mamilioni ya watu katika Jumuiya ya Wakristo wameweka anasa mahali pa Mungu. Wao hupendelea kujifurahisha kwa tafrija fulani badala ya kupendezwa na Neno la Mungu kwa uzito. (2 Tim. 3:4) Bila shaka, vitumbuizo na tafrija ifaayo si mbaya yenyewe. Lakini kutumia wakati mwingi mno kila juma kwa mambo kama vile televisheni, sinema, vidio, michezo, kusoma vichapo vya kilimwengu, au mambo ya kujifurahisha kwaweza kuruhusu moyo mdanganyifu usitawi na kutuvuta mbali na Yehova. (Yer. 17:9; Ebr. 3:12) Hilo laweza kutukiaje? Wakati wa mikutano ya Kikristo, huenda ukapata kwamba akili yako huzurura-zurura; huenda hata ukataka sana mkutano uishe ili uweze kurudi kwenye ufuatiaji wa anasa. Upesi, ungeweza kujipata ukitafuta sababu za kubaki nyumbani badala ya kuhudhuria mikutano au kushiriki katika utumishi wa shambani. Sasa ndio wakati wa kuamua kwa wazi kama ufuatiaji huo mbalimbali umekuja kuwa vikengeusha-fikira maishani mwako. (Lk. 8:14) Je! sehemu ya muda wa saa hizo zenye thamani zinazotumiwa kwa vitumbuizo yaweza kutumiwa vema zaidi kwa ajili ya ukuzi wa kiroho?
8 Masuala ya Kando-Kando Yenye Kutumia Wakati: Wengine wamenaswa na jitihada za kusuluhisha matatizo yaliyo ya kawaida katika jamii ya kisasa. Wakristo wanahitaji kuepuka kujiingiza katika ile mijadala ya ulimwengu isiyo na mwisho inayohusu masuala ya kijamii au kule kung’ang’ana kwao kwa bure ili kurekebisha hali ya ukosefu wa haki. (Yn 17:16) Hayo yote ni sehemu ya ubuni wa Shetani wa kugeuza uangalifu kutoka kwenye shauri la Biblia na lile jambo la hakika kwamba kuna suluhisho moja tu la kudumu—Ufalme wa Mungu. Ikiwa tumepatwa na dhara la kibinafsi au kutendwa isivyo haki, ni lazima tujilinde dhidi ya kuwa wenye kutaka kisasi au kufadhaika sana kihisiamoyo hivi kwamba twasahau sisi ni nani—Mashahidi wa Yehova. Zaidi ya hayo yote, ni Yehova ambaye ametendwa vibaya, na ni jina lake ambalo ni lazima tutakase.—Isa. 43:10-12; Mt. 6:9.
9 Ingawa kila mtu ataka kudumisha kadiri fulani ya afya njema, kutoa uangalifu mwingi mno kwa zile nadharia na dawa zisizo na mwisho zinazotolewa kwaweza kumfanya mtu ahangaikie sana mambo ya afya. Kuna watu wengi mno wanaopendekeza ulaji mwingi mbalimbali, tiba, na taratibu za kuponya matatizo ya kimwili na ya kihisiamoyo, ambazo nyingi yazo hupingana. Yale ambayo mtu afanya kuhusiana na mambo ya afya ni uamuzi wa kibinafsi, maadamu hayapingani na kanuni za Biblia. Sikuzote na tudumishe kutumaini kwetu kikamili katika Ufalme wa Mungu kuwa dawa ya kweli kwa magonjwa ya wanadamu.—Isa. 33:24; Ufu. 21:3, 4.
10 Uwe Imara, Usiyeondoleka: Mwisho ukaribiapo, Shetani ataongeza jitihada zake za kukukengeusha-fikira kutoka kwenye utumishi wako kwa Yehova. “Mpingeni huyo, mkiwa thabiti katika imani.” (1 Pet. 5:9) Jinsi gani? Ni lazima ujilishe na mawazo ya Mungu. (Mt. 4:4) Usiruhusu vikengeusha-fikira vya ulimwengu vikunyang’anye wewe na familia yako ule wakati unaohitaji ili kutafakari na kufikiri kwa ukimya juu ya Neno la Mungu. Wakati wa milo ya familia, zungumzieni pamoja maono yenye kujenga na mambo mengine ya kiroho. Shikamana na ratiba ya kawaida ya funzo la kibinafsi na kujitayarisha kwa ajili ya mitukano.
11 Mahangaiko yanapotisha kuvuruga akili yako, mtwike Yehova katika sala mzigo wako wa kulemea. Uwe na hakika kwamba yeye hukujali wewe. (1 Pet. 5:7) Acha amani ya Mungu ilinde moyo wako na nguvu zako za akilini. (Flp. 4:6, 7) Usiruhusu vikengeusha-fikira viharibu mwono wako wa kiroho. Mweke Yehova mbele yako daima, kama vile Yesu alivyofanya. (Mdo. 2:25) Kazia macho yako mbele kabisa kwenye mradi wako, kama vile Mithali 4:25-27 latutia moyo: “Macho yako yatazame mbele, na kope zako zitazame mbele yako sawasawa. Ulisawazishe pito la mguu wako, na njia zako zote zithibitike; usigeuke kwa kuume wala kwa kushoto.”
12 Hudhuria mikutano yote kwa uaminifu, na ujitie nidhamu ili utoe uangalifu kwenye mafundisho kutoka katika Neno la Mungu. (Ebr. 2:1; 10:24, 25) Na badala ya kutafuta anasa zinazotolewa na ulimwengu huu ulioshuka kiadili, fanya mradi wako uwe kudumisha huduma yenye matokeo. Hiyo ndiyo huleta shangwe na uradhi wenye kudumu. (1 The. 2:19, 20) Mwishowe, usiruhusu jambo lolote wala mtu yeyote akukengeushe-fikira kutoka kwenye utumishi wako mtakatifu. “Iweni imara, wasioondoleka, sikuzote mkiwa na mambo tele ya kufanya katika kazi ya Bwana, mkijua kwamba kazi yenu ya jasho si bure kuhusiana na Bwana.”—1 Kor. 15:58, NW.