Kujenga Uhusiano wa Karibu Pamoja na Yehova
1 “Lazima niseme kwamba nimeendelea kuwa katika kweli kwa miaka 20 hivi iliyopita kwa kwenda tu kwenye mikutano na kushiriki katika huduma ya shambani,” akiri dada mmoja Mkristo. Hata hivyo, aongeza, “nimekata kauli kwamba ingawa mambo yote hayo ni ya maana, mambo hayo pekee hayawezi kunisaidia mambo yaanzapo kuwa magumu. . . . Nang’amua kwamba lazima sasa nibadili kufikiri kwangu na kuanza programu ya maana ya kujifunza ili niweze kumjua Yehova kwelikweli na kumpenda na kuthamini kile ambacho Mwana wake ametupatia.”
2 Jitihada zinahitajiwa ili kujenga uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Haitoshi tu kushiriki utendaji wa Kikristo kidesturi. Tukikosa kusali kwa Yehova kwa ukawaida, muda si muda hatutakuwa na urafiki wa karibu naye tena. (Ufu. 2:4) Ebu tuchunguze jinsi funzo la Biblia la kibinafsi na sala zinavyoweza kutusaidia kujenga urafiki wa karibu na Yehova.—Zab. 25:14.
3 Kusali na Kutafakari Ni Muhimu: Funzo la kibinafsi linaloimarisha moyo huhusisha mengi zaidi kuliko kupiga mstari chini ya mambo makuu na kusoma maandiko yaliyotajwa. Tunapaswa kufikiria kile ambacho tunajifunza kuhusu njia za Yehova, sheria zake, na sifa zake. (Kut. 33:13) Kuelewa mambo ya kiroho hugusa hisia zetu na kutuchochea tufikirie maisha yetu. (Zab. 119:35, 111) Tunapaswa kujifunza kibinafsi tukiwa na lengo la kumkaribia Yehova. (Yak. 4:8) Ili tuwe na funzo la maana tunahitaji wakati wa kutosha na mazingira yanayofaa, na tunahitaji kujitia nidhamu ili tujifunze kwa ukawaida. (Dan. 6:10) Hata kama una shughuli nyingi, je, unatenga wakati kila siku kutafakari sifa za ajabu za Yehova?—Zab. 119:147, 148; 143:5.
4 Sala ya kutoka moyoni ni sehemu muhimu ya funzo la kibinafsi la maana. Tunahitaji roho takatifu ya Mungu ili kweli za Biblia ziguse moyo wetu na kutuchochea ‘tumtolee Mungu utumishi mtakatifu kwa woga wa kimungu na heshima.’ (Ebr. 12:28) Kwa hiyo, tunapaswa kuanza kila funzo kwa kumwomba Yehova atupe roho yake. (Mt. 5:3) Tunapotafakari Maandiko na kutumia vifaa vya funzo vilivyotayarishwa na tengenezo la Yehova, tunamfungulia Yehova mioyo yetu. (Zab. 62:8) Kujifunza kwa njia hiyo ni tendo la ibada ambalo huonyesha ujitoaji wetu kwa Yehova na huimarisha uhusiano wetu pamoja naye.—Yuda 20, 21.
5 Kama mahusiano mengine yote, ni lazima uhusiano wetu pamoja na Yehova uimarishwe daima ili uendelee kuwa wa karibu zaidi siku zote. Kwa hiyo, na tununue wakati kila siku ili tumkaribie Mungu, tukijua kwamba atatukaribia.—Zab. 1:2, 3; Efe. 5:15, 16.
[Maswali ya Funzo]
1. Dada mmoja alitambua nini kuhusu utendaji wake wa kiroho?
2. Kwa nini ni muhimu kujenga uhusiano wa karibu pamoja na Yehova?
3. Funzo letu la kibinafsi linapaswa kuwaje ili litusaidie kumkaribia Yehova?
4. Kusali wakati wa funzo la kibinafsi hutusaidiaje kujenga uhusiano wa karibu pamoja na Yehova?
5. Kwa nini ni muhimu kutafakari Neno la Mungu kila siku?