Shambulizi la Wapanda-Farasi Linalokuhusu Wewe
1 “Malaika wa sita akaipiga tarumbeta yake.” Kisha, “majeshi ya askari wapanda-farasi” ambayo hesabu yake ni “makumi mawili ya maelfu ya makumi ya maelfu” yanguruma. Hili si jeshi la kawaida. ‘Vichwa vya farasi hao ni kama vichwa vya simba.’ Moto, moshi, na kiberiti vyafoka kutoka vinywani mwao, na “mikia yao ni kama nyoka.” Jeshi hili la mfano la wapanda-farasi laharibu kila kitu linaposhambulia. (Ufu. 9:13-19) Je, unajua jinsi unavyohusika katika utimizo wa maono haya ya kinabii yenye kutokeza?
2 Mabaki watiwa mafuta na waandamani wao, wale kondoo wengine, wameungana pamoja kutangaza hukumu za Mungu. Wanafunua waziwazi kwamba Jumuiya ya Wakristo imekufa kiroho. Na tuchunguze sehemu mbili za maono hayo ya kinabii zinazokazia kwa nini huduma ya watumishi wa Mungu ina matokeo sana.
3 Wamezoezwa na Kupewa Vifaa vya Kutangaza Ujumbe wa Mungu: Kupitia Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na mikutano mingine ya kutaniko, wahudumu wa Mungu wamezoezwa kusema ujumbe wa Mungu kwa mamlaka. Wanamwiga Yesu na wanafunzi wake kwa kwenda kuwatafuta watu wanaostahili, na kuhubiri popote watu wanapopatikana. (Mt. 10:11; Marko 1:16; Luka 4:15; Mdo. 20:18-20) Njia hii ya kuhubiri ambayo imetajwa katika Biblia imekuwa na matokeo sana!
4 Mabilioni ya Biblia, vitabu, broshua, na magazeti yamesambazwa na wahudumu Wakristo wanapohubiri kama walivyoagizwa na Mungu. Vichapo hivyo vimeandikwa katika lugha zipatazo 400, vina habari mbalimbali na vimeandikwa kwa njia inayowavutia watu mbalimbali. Je, wewe unatumia vichapo hivyo kwa njia yenye matokeo?
5 Mwongozo na Msaada Kutoka Mbinguni: Maono hayo ya kinabii pia yanaonyesha wazi kwamba Mungu anaunga mkono utendaji wa jeshi la mfano la wapanda-farasi. (Ufu. 9:13-15) Kazi ya kuhubiri inayofanywa ulimwenguni pote inatimizwa kwa nguvu za roho ya Mungu wala si kwa hekima au nguvu za wanadamu. (Zek. 4:6) Yehova anawatumia malaika kuiongoza kazi hii. (Ufu. 14:6) Kwa hiyo, Yehova anawavuta watu wanyenyekevu kupitia jitihada za Mashahidi wake wanadamu.—Yoh. 6:45, 65.
6 Watu wa Yehova ni jeshi lisiloshindika kwa sababu wamezoezwa, wamepewa vifaa vya kutangaza ujumbe wa Mungu, na wanaoongozwa na malaika. Na tuendelee kutimiza daraka letu katika utimizo wa maono haya ya kinabii yenye kusisimua.
[Maswali ya Funzo]
1, 2. Watumishi wa Mungu leo wanahusikaje katika utimizo wa maono ya kinabii yaliyoandikwa katika Ufunuo 9:13-19?
3. Umezoezwaje kusema ujumbe wa Mungu kwa matokeo?
4. Wahubiri wengi wana vifaa gani vya kuwasaidia kuhubiri?
5, 6. Ni nini kinachoonyesha kwamba watu wa Yehova wanaungwa mkono na Mungu?