Onyesha Shukrani Zako
1 Ingawa tunaishi “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo,” tuna sababu nyingi za kumshukuru Yehova. (2 Tim. 3:1) Kwanza kabisa tunamshukuru Yehova kwa sababu ya zawadi yenye thamani ya Mwana wake kwa ajili yetu. (Yoh. 3:16) Zaidi ya hayo, sisi tuna chakula kingi cha kiroho ilhali wale walio katika dini za uwongo wana njaa ya kiroho. (Isa. 65:13) Sisi ni sehemu ya undugu wa ulimwenguni pote na tuna pendeleo lenye kusisimua la kushiriki katika upanuzi wa ibada ya kweli. (Isa. 2:3, 4; 60:4-10, 22) Tunawezaje kuonyesha shukrani zetu kwa Yehova kwa baraka ambazo anatumiminia?—Kol. 3:15, 17.
2 Utumishi wa Shangwe, wa Moyo Wote: Alipokuwa akizungumzia utoaji wa vitu vya kimwili, mtume Paulo aliandika: “Mungu humpenda mtoaji mchangamfu.” (2 Kor. 9:7) Kanuni hiyo inatumika pia kuhusu utumishi wetu kwa Mungu. Shukrani zetu zinaonyeshwa tunapokuwa na shauku kwa ajili ya kweli, shangwe katika mikutano ya Kikristo, bidii katika utumishi wa shambani, na furaha katika kufanya mapenzi ya Mungu.—Zab. 107:21, 22; 119:14; 122:1; Rom. 12:8, 11.
3 Katika Israeli la kale, Sheria haikuwaamuru watu watoe kiasi hususa cha matoleo fulani. Kila mwabudu alionyesha shukrani zake kwa kutoa “kulingana na baraka za Yehova” alizopokea. (Kum. 16:16, 17) Vivyo hivyo leo, moyo wenye shukrani utatuchochea kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi kadiri hali zetu zinavyoruhusu. Mara nyingi miezi ya Julai hadi Septemba hutupa nafasi zaidi za kuonyesha shukrani zetu. Wengine hutumia vizuri siku za likizo ya kazi au ya shule kuongeza utumishi wao wa shambani au hata kufanya upainia msaidizi. Je, unaweza kupanua huduma yako miezi hiyo?
4 Kujawa Kabisa na Shukrani: Sala ni njia moja muhimu ya kuonyesha shukrani zetu kwa Yehova. (1 The. 5:17, 18) Neno la Mungu linatuhimiza tuwe ‘tukijawa kabisa na imani katika kutoa shukrani.’ (Kol. 2:7) Hata tunapokuwa na shughuli nyingi sana au tunapokuwa na mkazo, nyakati zote tunapaswa kutoa shukrani katika sala zetu za kila siku. (Flp. 4:6) Naam, na tuendelee kuwa “matajiri kwa maonyesho mengi ya shukrani kwa Mungu” kupitia huduma yetu na vilevile sala zetu.—2 Kor. 9: 12.