Yehova Huwasaidia Wale Wanaomtegemea
1 Watu wengi huona pesa, mamlaka, na vipawa vya kibinadamu kuwa ndizo funguo za kupata mafanikio. (Zab. 12:4; 33:16, 17; 49:6) Hata hivyo, Biblia inawahakikishia wale wanaomwogopa Yehova na kumtegemea kwamba “yeye ndiye msaada wao na ngao yao.” (Zab. 115:11) Na tuchunguze njia mbili ambazo tunahitaji kuonyesha kwamba tunamtegemea Yehova.
2 Tukiwa Wahudumu Wakristo: Wakati wowote tunapokuwa na migawo katika kutaniko au tunapofundisha katika huduma ya shambani, lazima tumtegemee Mungu wetu. Fikiria mfano wa Yesu. Ingawa alikuwa Mwana wa Mungu, hakutegemea hekima yake au uwezo wake mwenyewe, bali alimtegemea kabisa Baba yake wa mbinguni. (Yoh. 12:49; 14:10) Sisi pia tunahitaji kumtegemea hata zaidi, sivyo? (Met. 3:5-7) Ni kupitia tu baraka za Yehova ndipo jitihada zetu kidogo zitamletea heshima na kuwafaidi wengine.—Zab. 127:1, 2.
3 Tunaonyesha kwamba tunamtegemea Yehova tunaposali ili kupata mwongozo wake na msaada wa roho yake takatifu. (Zab. 105:4; Luka 11:13) Kwa kuongezea, tunaonyesha kwamba tunamtegemea Mungu tunapotegemeza mafundisho yetu juu ya Neno lake, Biblia. Ujumbe wake una nguvu za kufikia mioyo na kubadilisha maisha ya watu. (Ebr. 4:12) ‘Tunapohudumu kama tunaotegemea nguvu ambazo Mungu hutoa,’ Yehova hutukuzwa.—1 Pet. 4:11.
4 Kushughulika na Matatizo: Pia tunahitaji kutafuta msaada wa Yehova tunapokabiliwa na mikazo na matatizo. (Zab. 46:1) Kwa mfano, huenda mwajiri akasita kutupatia ruhusa ya kuhudhuria kusanyiko, au huenda tukakabili hali ngumu katika familia yetu. Tunaonyesha kwamba tunamtegemea Yehova kwa kumsihi kwa bidii na kutumia mwongozo anaotoa kupitia Neno na tengenezo lake. (Zab. 62:8; 119:143, 173) Kwa kufanya hivyo, watumishi wa Yehova huona msaada wake maishani mwao.—Zab. 37:5; 118:13, 16.
5 Yehova mwenyewe anatuhakikishia hivi: “Amebarikiwa yule mtu hodari anayemtegemea Yehova, na ambaye Yehova amekuwa uhakika wake.” (Yer. 17:7) Na tumtegemee katika mambo yote tunayofanya!—Zab. 146:5.