Malaika Wanatusaidia
1 “Tazama! mimi nipo pamoja nanyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” Maneno hayo yanawatia moyo kama nini wale wote wanaotii amri hii ya Yesu: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi”! (Mt. 28:18-20) Njia moja muhimu ambayo Yesu yuko pamoja na Wakristo wa kweli ni kupitia malaika zake. (Mt. 13:36-43) Inasisimua kama nini kutangaza “habari njema ya milele” pamoja na viumbe hao waaminifu wa roho!—Ufu. 14:6, 7.
2 Katika Huduma Yetu: Biblia huonyesha kwamba malaika wanatumwa “kuhudumu kwa ajili ya wale watakaorithi wokovu.” (Ebr. 1:14) Katika karne ya kwanza, malaika walihusika katika kuwaongoza wafuasi wa Yesu kwa watu waliostahili. (Mdo. 8:26) Leo, watumishi wa Mungu wanaendelea kuona uthibitisho wa mwongozo wa malaika. Mara nyingi, Mashahidi walipowatembelea wenye nyumba, watu hao walisema kwamba walikuwa wanasali ili wapate msaada. Sisi pamoja na malaika hufurahi kama nini watu hao wanapokubali ujumbe wa Ufalme!—Luka 15:10.
3 Kukabili Upinzani: Danieli, Waebrania wenzake watatu wachanga, mtume Petro, na wengine wengi ambao wamepatwa na majaribu makali wameona ulinzi wa Yehova kupitia malaika, wenye “uwezo katika nguvu.” (Zab. 103:20; Dan. 3:28; 6:21, 22; Mdo. 12:11) Ingawa nyakati nyingine huenda tukahisi tumelemewa tunapokabili upinzani, mambo yaliyompata mtumishi wa Elisha alipojua kwamba “walio pamoja nasi ni wengi kuliko wale walio pamoja nao,” yanaweza kututia moyo. (2 Fal. 6:15-17) Hata kama tumetenganishwa kinguvu kutoka kwa ndugu zetu, hatukosi tumaini. Neno la Mungu linatuhakikishia hivi: “Malaika wa Yehova anapiga kambi pande zote kuwazunguka wanaomwogopa.”—Zab. 34:7.
4 Hivi karibuni majeshi ya malaika yatawaondoa wapinzani wote wa utawala wa Kristo. (Ufu. 19:11, 14, 15) Tunapoingojea siku hiyo, na tuendelee kumsifu Yehova kwa ujasiri, tukiwa na uhakika kamili wa kupata msaada wenye nguvu wa majeshi ya mbinguni yaliyo chini ya amri ya Kristo.—1 Pet. 3:22.