Shule ya Mazoezi ya Kihuduma—Mlango Mkubwa Unaoongoza Kwenye Utendaji
1 Yehova alitabiri hivi kupitia nabii Yeremia: “Nami nitasimamisha juu yao wachungaji ambao kweli watawachunga; nao hawataogopa tena, wala hawataingiwa na hofu yoyote, na hakuna hata mmoja atakayekosekana.” (Yer. 23:4) Uchungaji huo unafanywa leo kati ya watu wa mataifa yote. Huo unafanywa na makumi ya maelfu ya wazee wa makutaniko. Zaidi ya hayo, kundi la vijana walio wengi kama umande wamejitoa kwa hiari ili kufanya utumishi wa Yehova. (Zab. 110:3) Ndugu hao wanyenyekevu ni baraka kwelikweli kwa makutaniko ya watu wa Mungu! Kazi ya uvunaji wa kiroho inapoendelea, bado kuna uhitaji wa wanaume wenye sifa za kustahili wajitolee ili kuwatumikia ndugu zao.
2 Shule ya Mazoezi ya Kihuduma ni mpango mzuri wa kuwazoeza wazee na watumishi wa huduma walio waseja kwa ajili ya madaraka zaidi. Zaidi ya wanafunzi 22,000 kutoka nchi 140 hivi wamepokea mazoezi hayo katika madarasa 999 ambayo yamefanywa tangu kuanzishwa kwa shule hiyo mwaka wa 1987. Kwa ndugu hao, shule hiyo imekuwa “mlango mkubwa unaoongoza kwenye utendaji.”—1 Kor. 16:9.
3 Kusudi la Shule Hiyo: Kusudi la Shule ya Mazoezi ya Kihuduma ni kuwazoeza na kuwatayarisha wanaume wenye sifa za kustahili kwa ajili ya madaraka mahali popote palipo na uhitaji katika tengenezo. Shule hiyo inaongeza ustadi wao wa kuongoza katika kazi ya kueneza Injili, kushiriki katika kulichunga kundi, na kufundisha kutanikoni. Baada ya kuhitimu, wanafunzi fulani hupewa migawo ya kuwa mapainia wa pekee au waangalizi wanaosafiri katika nchi zao au katika nchi za nje. Wengine hupewa migawo ya kutumikia makutaniko yao au mahali ambapo pana uhitaji mkubwa katika eneo la ofisi ya tawi.
4 Wakati wa masomo hayo yanayochukua majuma manane, wanafunzi hujifunza Biblia kwa makini sana. Wanajifunza kwa uangalifu mafundisho mengi ya Biblia na vilevile madaraka ya uchungaji na miongozo ya kushughulikia matatizo katika maisha ya Mkristo. Pia wanajifunza yale ambayo Maandiko husema kuhusu mambo ya usimamizi, ya hukumu, na ya kitengenezo. Wao hupokea mazoezi ya pekee yanayohusu kutoa hotuba, nao hupewa mashauri ya kibinafsi ili wafanye maendeleo yao ya kiroho kwa haraka zaidi.
5 Matakwa: Ni wazi kwamba matakwa ya kuhudhuria shule hiyo si rahisi. Wenye kutoa maombi lazima wawe wametumikia wakiwa wazee au watumishi wa huduma kwa angalau miaka miwili mfululizo. Ni lazima wote wawe waseja na wenye umri wa kati ya miaka 23 na 50. Wenye kutoa maombi lazima waweze kusoma, kuandika, na kusema vizuri lugha inayotumiwa katika shule hiyo, nao lazima wawe na afya nzuri, wasiwe wanahitaji utunzaji wa pekee au chakula cha pekee. Wale ambao ni mapainia wa kawaida hufikiriwa kwanza.
6 Wale wanaojitolea lazima wawe na nia na uwezo wa kutumikia popote pale wanapohitajiwa. Hilo linahitaji mtu awe na roho kama ile ya nabii Isaya, aliyejitoa kwa hamu kufanya kazi ya pekee, akisema: “Mimi hapa! Nitume mimi.” (Isa. 6:8) Pia alikuwa na unyenyekevu katika maisha yake yote. Wale wanaotoa maombi ya kuhudhuria Shule ya Mazoezi ya Kihuduma wanapaswa kuchochewa na upendo kwa ndugu zao na hamu ya kutaka kuwatumikia badala ya kutamani umashuhuri au cheo. Baada ya kupokea mazoezi hayo mazuri, ndugu hao wanatarajiwa kutumia yale waliyojifunza ili kuwafaidi wengine.—Luka 12:48.
7 Faida: Wakati wa majuma hayo manane ya mazoezi makali, ndugu hao ‘hulishwa maneno ya imani na ya fundisho zuri.’ (1 Tim. 4:6) Hayo huwatayarisha ili wawasaidie na kuwatia moyo wengine katika makutaniko na mizunguko waliyogawiwa. Katika maeneo mengi ambapo wahitimu wa Shule ya Mazoezi ya Kihuduma wametumwa, utumishi wa shambani umeongezeka; utumishi wa painia umechochewa, hasa kati ya vijana; na wapya wanaoshirikiana na watu wa Mungu wamesaidiwa zaidi.
8 Je, wewe ni mzee au mtumishi wa huduma aliye mseja, na una umri wa kati ya miaka 23 na 50? Kwa nini usifikirie kutoa maombi ya kuhudhuria Shule ya Mazoezi ya Kihuduma? Je, wewe ni ndugu mchanga anayefikiria miradi ya muda mrefu katika utumishi wa Yehova? Kwa nini usiishi maisha rahisi yasiyo na vikengeusha-fikira ili uweze kuingia huu “mlango mkubwa unaoongoza kwenye utendaji”? Hilo linaweza kukuletea shangwe nyingi na uradhi. Naam, Shule ya Mazoezi ya Kihuduma imekuwa baraka, si kwa wahitimu wa shule hiyo tu, bali pia kwa makutaniko ya watu wa Mungu ulimwenguni pote.
[Sanduku katika ukurasa wa 3]
Jinsi Walivyofaidika na Mazoezi ya Shule Hiyo
“Mazoezi hayo yameiboresha kwelikweli huduma yangu na uwezo wangu wa kuchunga kutaniko kwa hekima, nikitumia Maandiko.”
“Shule hiyo imenifanya niwe na uhakika zaidi ninaposhughulikia madaraka yangu mbalimbali kutanikoni.”
“Shule hiyo imebadili karibu kila jambo maishani mwangu, kutia ndani jinsi ninavyoiona mipango ya Mungu na tengenezo lake.”
“Mazoezi niliyopokea yalinisaidia kutambua uhitaji wa kujitolea kutumikia mahali palipo na uhitaji.”