Siku ya Yehova Iko Karibu
1 Wakristo wanatamani sana kuja kwa siku ya Yehova, wakati ambapo Mungu ataharibu ulimwengu huu na kuleta ulimwengu mpya wenye uadilifu. (2 Pet. 3:12, 13) Kwa kuwa hatujui siku hiyo itakuja lini, ni lazima tuendelee kukaa macho na kuwasaidia wengine kufanya vivyo hivyo. (Eze. 33:7-9; Mt. 24:42-44) Kutafakari Neno la Mungu la kinabii kutaimarisha usadikisho wetu kwamba “ile siku kuu ya Yehova iko karibu.”—Sef. 1:14.
2 Mfuatano wa Serikali Kuu za Ulimwengu: Katika Ufunuo 17:9-11 mtume Yohana anawataja “wafalme saba” ambao wanafananisha serikali kuu saba za ulimwengu. Yohana anamtaja pia “mfalme wa nane,” ambaye anafananisha Umoja wa Mataifa. Je, tutarajie serikali nyingine kuu za ulimwengu zitokee? La. Unabii unasema kwamba yule mfalme wa nane “anaenda zake kwenye uharibifu,” na baada yake hakuna wafalme wengine wa dunia wanaotajwa. Je, unabii huu unakusaidia kutambua tunaishi katika kipindi gani cha wakati?
3 Andiko la Danieli 2:31-45 linatusaidia kuelewa kule kuja kwa siku ya Yehova. Katika unabii huo, sanamu kubwa ambayo Nebukadneza aliiona katika ndoto inafananisha mfuatano wa serikali kuu za ulimwengu. Tayari kila moja ya serikali hizo imetokea. Ni serikali gani inayotawala leo? Ni ile inayofananishwa na nyayo za sanamu hiyo. Unabii huo unaonyesha waziwazi matukio yatakayofuata. Serikali za wanadamu zitaharibiwa kabisa ili “ufalme ambao hautaharibiwa kamwe” utawale. Je, unaona jinsi jambo hilo linavyoonyesha kwamba siku ya Yehova iko karibu?
4 Uthibitisho Mwingine: Sisi huona mambo mengine ambayo yanathibitisha kwamba siku ya Yehova iko karibu. Tunaona utimizo wa yale ambayo mtume Paulo alitabiri kuhusu sifa za watu “katika siku za mwisho.” (2 Tim. 3:1-5) Nasi tunashiriki kutoa ushahidi ulimwenguni pote, ushahidi unaopaswa kutolewa kabla ya ule mwisho. (Mt. 24:14) Kazi yetu ya kuhubiri na ionyeshe umuhimu wa ujumbe huu wa malaika: “Mwogopeni Mungu na kumpa utukufu, kwa sababu saa ya hukumu yake imefika.”—Ufu. 14:6, 7.