Kuhubiri Hutusaidia Kuvumilia
1 Neno la Mungu linatuhimiza “tukimbie kwa uvumilivu shindano la mbio lililowekwa mbele yetu.” (Ebr. 12:1) Kama mkimbiaji anavyohitaji kuvumilia ili amalize mbio, ndivyo tunavyohitaji kuvumilia ili tupate zawadi ya uzima wa milele. (Ebr. 10:36) Huduma ya Kikristo inaweza kutusaidiaje kuvumilia kwa uaminifu mpaka mwisho?—Mt. 24:13.
2 Tunaimarishwa Kiroho: Kutangaza ahadi nzuri ya Biblia kuhusu ulimwengu mpya wenye uadilifu hutusaidia kudumisha uhakika wa tumaini letu wenyewe. (1 The. 5:8) Tunapohubiri kwa ukawaida, tunakuwa na fursa ya kuwajulisha wengine kweli ambazo tumejifunza kutoka katika Biblia. Tunapata fursa ya kuitetea imani yetu, na kufanya hivyo hutuimarisha kiroho.
3 Ni lazima tuelewe waziwazi kweli za Biblia ili tuweze kuwafundisha wengine vizuri. Tunahitaji kufanya utafiti na kutafakari kuhusu habari hiyo. Tunapojitahidi kufanya hivyo, ujuzi wetu unaongezeka, imani yetu inaimarika, na tunapata nguvu mpya ya kiroho. (Met. 2:3-5) Kwa hiyo, tunapojitahidi kuwasaidia wengine, tunajiimarisha sisi wenyewe.—1 Tim. 4:15, 16.
4 Kuhubiri kwa bidii ni sehemu muhimu ya “mavazi kamili ya silaha kutoka kwa Mungu,” ambayo tunahitaji ili kusimama imara dhidi ya Ibilisi na roho wake waovu. (Efe. 6:10-13, 15) Kujishughulisha sana na utumishi mtakatifu hutusaidia kukazia akilini mwetu mambo yanayojenga na kuepuka kuchafuliwa na ulimwengu wa Shetani. (Kol. 3:2) Tunapowafundisha wengine njia za Yehova, tunakumbushwa daima kwamba sisi pia tunahitaji kudumisha mwenendo mtakatifu.—1 Pet. 2:12.
5 Mungu Anatutia Nguvu: Hatimaye, kushiriki katika kazi ya kueneza injili hutufundisha kumtegemea Yehova. (2 Kor. 4:1, 7) Ni baraka iliyoje! Kusitawisha sifa hiyo ya kumtegemea Yehova hutusaidia kutimiza huduma yetu na vilevile kukabiliana na hali yoyote maishani. (Flp. 4:11-13) Kwa kweli, kujifunza kumtegemea Yehova kabisa ndio msingi wa kuvumilia. (Zab. 55:22) Kuhubiri hutusaidia katika njia nyingi kuvumilia.