‘Nifuateni Sikuzote’
1 Watu wengi hufuatilia mapendezi yao, lakini mara nyingi hawana furaha. Tofauti na hilo, Yesu alipendekeza kujitoa bila ubinafsi ambako huleta furaha ya kweli. (Mdo. 20:35) Alisema: “Mtu yeyote akitaka kunifuata, na ajikane mwenyewe . . . na kunifuata sikuzote.” (Marko 8:34) Hilo linatia ndani mengi zaidi ya kujinyima raha mara kwa mara tu. Linamaanisha kumpendeza Yehova kila siku badala ya kujipendeza wenyewe.—Rom. 14:8; 15:3.
2 Fikiria mfano wa mtume Paulo. Kwa sababu ya “thamani bora zaidi ya kumjua Kristo Yesu,” Paulo aliacha kufuatilia tamaa zake na kujitoa kuendeleza mambo yanayohusiana na Ufalme. (Flp. 3:7, 8) Alisema: “Kwa upande wangu mimi nitatumia kwa furaha zaidi na kutumiwa kabisa” kuwatumikia wengine. (2 Kor. 12:15) Kila mmoja wetu anapaswa kujiuliza: ‘Ninatumiaje wakati, nguvu, uwezo, na mali zangu? Je, ninatanguliza mapendezi yangu, au ninatafuta kumpendeza Yehova?’
3 Fursa za Kujitoa: Kila mwaka, watu wa Mungu hutumia zaidi ya saa bilioni moja katika kazi inayookoa uhai ya kuhubiri Ufalme. Katika kutaniko, vijana kwa wazee hutimiza migawo mbalimbali ambayo huwanufaisha wengine. Pia kazi nyingi hufanywa kuhusiana na makusanyiko na pia kujenga na kudumisha majengo yanayotumiwa kuendeleza ibada ya kweli. Na hebu fikiria msaada wenye upendo ambao hutolewa na ndugu wanaotumikia katika Halmashauri za Uhusiano na Hospitali na vilevile Vikundi vya Kuwatembelea Wagonjwa. Jitihada zote hizo zinazotolewa bila ubinafsi huthaminiwa na undugu wetu wa Kikristo!—Zab. 110:3.
4 Fursa za kutoa msaada katika njia mbalimbali zinaweza kujitokeza wakati msiba au hali ya dharura inapotokea. Lakini, mara nyingi tunaweza kutambua kwamba Mkristo mwenzetu anahitaji msaada au kitia moyo. (Met. 17:17) Tunapojitoa wenyewe kuwatumikia wengine na kuendeleza mambo yanayohusiana na Ufalme, tunafuata kielelezo cha Yesu. (Flp. 2:5-8) Na tujitahidi kufanya hivyo sikuzote.