Onyesha Unawajali Watu Kikweli—Kwa Kuwa Mwenye Neema
1 “Yehova ni mwenye neema.” (Zab. 145:8) Hata ingawa yeye ndiye Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote, yeye huwatendea wanadamu wasio wakamilifu kwa fadhili, ufikirio, na kwa heshima. (Mwa. 13:14; 19:18-21, 29) Tunaweza kuboresha jinsi tunavyohubiri kwa kumwiga Mungu wetu mwenye neema. (Kol. 4:6) Hilo linatia ndani mengi zaidi ya kuwa mwenye adabu na kuzungumza kwa heshima.
2 Kutoka Mlango Hadi Mlango: Tunapaswa kufanya nini tunapomtembelea mwenye nyumba wakati usiofaa au ikiwa yeye ana shughuli nyingi sana hivi kwamba hawezi kuzungumza nasi? Tunapaswa kutambua hali hiyo na kufupisha ujumbe wetu au kumwambia kwamba tutarudi wakati mwingine. Hatutawalazimisha watu wachukue vichapo vyetu ikiwa hawataki. Kuwafikiria wengine pia kutatufanya tuheshimu mali zao, kama vile kufunga milango na kuwazoeza watoto wetu kufanya hivyo pia. Tunapaswa kuhakikisha kwamba vichapo vyovyote tulivyoacha kwenye nyumba ambazo hatukupata watu havionekani na wapita njia. Kwa kweli, kuwa wenye neema kutatuchochea kuwatendea wengine katika njia ambayo tungetaka wao watutendee.—Luka 6:31.
3 Katika Mahubiri ya Barabarani: Tunapohubiri barabarani, tunaweza kuwa wenye adabu kwa kutoziba njia au kukusanyika mbele ya maduka. Tutatambua hali za watu na kujaribu kuzungumza na wale wanaoonekana kuwa wana wakati badala ya kuzungumza na wale ambao tunaona wazi kwamba wana haraka. Nyakati nyingine, itatubidi tuzungumze kwa sauti kwa sababu ya kelele barabarani. Lakini tunapaswa kufanya hivyo kwa heshima, na kutojielekezea fikira.—Mt. 12:19.
4 Tunapohubiri kwa Kutumia Simu, Inapowezekana: Kuwafikiria wengine kutatuchochea tuhubiri kwa kutumia simu mahali pasipo na kelele. Tunaonyesha kuwa tuna adabu kwa kujitambulisha mara moja na kueleza kusudi letu la kupiga simu. Kushika simu vizuri na kuzungumza kwa uchangamfu kutasaidia kuwahusisha wengine katika mazungumzo ya Biblia yenye kujenga. (1 Kor. 14:8, 9) Tunamwiga Yehova, Mungu wetu mwenye neema kwa kuwa wenye fadhili, kuwafikiria wengine na kuwa wenye adabu katika njia hizo.