Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g96 6/8 kur. 10-12
  • Adabu Zako za Simu Zikoje?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Adabu Zako za Simu Zikoje?
  • Amkeni!—1996
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Simu na Wewe
  • Ufikirio Wenye Kujali Wengine
  • Ubora wa Usemi
  • Uwe Msikilizaji Mzuri
  • Mambo ya Mwisho ya Kufikiriwa
  • Mahubiri ya Simu Yenye Matokeo
    Huduma Yetu ya Ufalme—2004
  • “Jiendesheni kwa Namna Inayozistahili Habari Njema”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Kusitawisha Adabu za Kikristo Katika Ulimwengu Usio na Adabu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1989
  • Kuhubiri kwa Simu Kunaweza Kuwa na Matokeo
    Huduma ya Ufalme—2009
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1996
g96 6/8 kur. 10-12

Adabu Zako za Simu Zikoje?

“Pamoja na shauku ya kifamilia, afya, na kupenda kazi, je, kuna lolote ambalo huchangia sana uzuri wa maisha, likitokeza na kukuza kujistahi kama yafanyavyo mazungumzo yenye fadhili?”

AKIULIZA swali hilo, mtungaji na mwelimishaji aliyekufa Lucy Elliot Keeler alikuwa akikazia sana raha za kibinafsi na utimizo uwezao kupatikana kutokana na mazungumzo, uwezo ambao kwa upendo mwanadamu alipewa alipoumbwa.—Kutoka 4:11, 12.

Yenye kuchangia sana ongezeko la usemi wa kibinadamu kwa zaidi ya miongo 12 ambayo imepita ni ule ubuni wa simu wa Alexander Graham Bell. Leo, kwa mabilioni ya wakazi wa dunia, simu, iwe inatumiwa kikazi au kwa ajili ya raha, huandaa kiunganisho cha maana kati ya wanadamu.

Simu na Wewe

Matumizi ya simu huongeza kwa kadiri gani ubora wa maisha yako? Je, hukubali kwamba jibu lako kwa swali hilo hutegemea zaidi watu wahusikao kuliko chombo chenyewe? Kwa kweli, huu ni wakati ufaao kuuliza lile swali, Adabu zako za simu zikoje?

Adabu za simu hutia ndani maeneo kama vile mtazamo wa akilini, ubora wa usemi, na uwezo wa kusikiliza. La maana pia ni jinsi ya kutumia simu na jinsi ya kushughulikia simu za kusumbua.

Ufikirio Wenye Kujali Wengine

Kama ilivyo kweli na mawasiliano mengineyo yote ya kibinadamu, adabu nzuri za simu hutokana na hisia-mwenzi. Mtume Paulo aliandika: “Angalieni mapendezi ya kila mmoja na si mapendezi yenu wenyewe tu.”—Wafilipi 2:4, The New English Bible.

Alipoulizwa lile swali, “Ni vipi vielelezo ambavyo umeona kuwa vya kawaida sana vya adabu mbaya za simu?,” opareta wa swichibodi ya simu mwenye uzoefu alijibu kwamba kielelezo cha kwanza katika orodha yake kilikuwa “mpiga-simu mwenye kusema, ‘Mimi ni Mary’ (Wewe unajua Mary wangapi?) au, kibaya hata zaidi ni wakati asemapo, ‘Ni Mimi,’ au ‘Kisia ni nani huyu.’” Mifikio yenye kukosa ufikirio kama hiyo, ingawa yenye makusudio mazuri, yaweza kutokeza aibu na kukosa subira. Huyo opareta aliendelea kusema: “Mbona usianzishe mazungumzo kwa njia nzuri kwa kujitambulisha wazi na zaidi, kwa kumfikiria umpigiaye simu, ukimuuliza ikiwa huo ni wakati ufaao wa kuzungumza?”

Kumbuka kwamba ingawa ishara zako za uso haziwezi kuonekana, mtazamo wako utadhihirika. Jinsi gani? Kupitia namna ya sauti yako. Kukosa subira, uchoshi, hasira, ubaridi, unyoofu, uchangamfu, hali ya kutaka kusaidia, na shauku—yote yaonyeshwa. Ni kweli kwamba kukasirika kwaweza kuwa itikio la kiasili mtu akatiziwapo shughuli na simu. Katika hali hii, ili kudumisha adabu njema, jaribu kutua na kuonyesha “tabasamu” katika sauti yako kabla ya kuongea. Yawezekana kukataa jambo bila ya kutumia sauti ya kukataa.

Ufikirio wenye kujali wengine pamoja na sauti nzuri ya kuongea yaweza kutokeza maneno ‘mema ya kumfaa mwenye kuhitaji’ na yenye kuwapa “neema wanaosikia.”—Waefeso 4:29.

Ubora wa Usemi

Ndiyo, aina ya usemi tutumiao ni ya maana. Je, wewe hukubaliana na kanuni zifuatazo na kuzishika? Sema kikawaida, wazi na kwa njia ielewekayo. Usinong’one. Usipige kelele—hata upigapo simu ya mbali. Usivute-vute maneno yako. Epuka usemi wa kizembe unaofupisha au kuruka silabi; pia epuka matumizi ya maneno kama “na-eh” na hali ya kujirudia-rudia, mambo ambayo yaweza kutatanisha na kuudhi. Epuka kabisa kutumia sauti moja tu isiyopendeza. Kukazia maana ifaavyo, na ubadilifu wa sauti hufanya usemi kuwa na maana, wenye kupendeza, na wenye kuburudisha. Pia kumbuka kwamba kula wakati unapozungumza kwenye simu hakuongezi ubora wa usemi wala adabu nzuri.

Kuchagua maneno kwafaa kufikiriwa pia. Utambuzi huhitajiwa. Tumia maneno dhahiri na rahisi yaelewekayo kwa urahisi. Maneno hudokeza mambo. Yaweza kuwa ya fadhili au makatili, yenye kufariji au kudhulumu, yenye kutia moyo au kuvunja moyo. Na zaidi, mtu aweza kuwa mcheshi bila kuudhi, aweza kusema mambo wazi bila kuwa mkali au mjeuri, na aweza kuwa mwenye busara bila kuhepa mambo. Maneno ya hisani kama vile “tafadhali” na “asante” sikuzote hupendeza. Maneno yenye fadhili, yenye ufikirio, na yenye kupendeza ndiyo ambayo mtume Paulo alikuwa nayo akilini alipoandika: “Maneno yenu yawe na neema siku zote, yakikolea munyu, mpate kujua jinsi iwapasavyo kumjibu kila mtu.”—Wakolosai 4:6.

Uwe Msikilizaji Mzuri

Kuna hadithi ya mwanamume kijana aliyemwomba baba yake amwambie siri ya kuwa msemaji mzuri. “Sikiliza mwanangu,” akajibiwa. “Nasikiliza,” akasema yule kijana. “Nieleze zaidi.” “Hakuna la ziada la kukueleza,” baba yake akamjibu. Kwa kweli, kuwa msikilizaji mwenye upendezi na mwenye hisia-mwenzi ni kwa maana ili kuwa na adabu nzuri za simu.

Kushindwa kushika kanuni ndogo kwaweza kufanya uonekane kuwa mpiga-simu mchoshi. Ni kanuni ipi? Usitawale mazungumzo. Kwa kielelezo, usiseme mengi katika mazungumzo yasiyoisha ya mambo madogo-madogo yaliyokupata au masimulizi ya matatizo madogo-madogo ya kiafya. Kwa mara nyingine tena, tuna kanuni ya Biblia yenye kutumika iliyo sahihi, wakati huu kutoka kwa mwanafunzi Yakobo. “Basi kila mtu na awe mwepesi wa kusikia, bali si mwepesi wa kusema.”—Yakobo 1:19.

Mambo ya Mwisho ya Kufikiriwa

Acheni sasa tuelekeze fikira kwa maswali mawili ya mwisho ambayo huhusiana na adabu za simu. Ni nini kiwezacho kusemwa juu ya matumizi ya vyombo vya simu? Je, kuna maagizo juu ya jinsi ya kushughulikia simu zisizotakwa?

Utumiapo simu, je, umepata kuona kwamba sauti iliyo upande ule mwingine hufifia na kurudi? Hilo lapaswa kukukumbusha useme katika chombo cha mdomo, kikiwa karibu sentimeta mbili kutoka midomo. Kwa kuongezea, ni jambo la hisani kuzuia kelele zinazokuzunguka. Upigapo simu, piga nambari kwa uangalifu ili kuepuka kupiga nambari isiyofaa; na umalizapo kupiga simu, weka kipokezi polepole.

Je, wewe umekuwa ukipata simu zenye kusumbua? Kwa kuhuzunisha hizo zaonekana kuwa zinaongezeka. Lugha isiyo na staha, yenye kudokeza mambo machafu, au lugha chafu yastahili itikio moja tu—kukata hiyo simu. (Linganisha Waefeso 5:3, 4.) Mambo yapaswa kuwa vivyo hivyo wakati mwenye kupiga simu akataapo kujitambulisha. Ukishuku simu kwa sababu fulani, kichapo How to Write and Speak Better hudokeza kwamba “usijibu wakati sauti usiyoijua iulizapo, ‘Ni nani anayeongea?’” nawe hupaswi kuzungumza mipango yako na mtu usiyemjua.

Jinsi inavyofurahisha kujua kwamba hatimaye, kujizoeza adabu nzuri za simu hakuhitaji orodha ndefu ya kanuni na miongozo! Kama vile katika shughuli zote miongoni mwa watu, mahusiano yenye kupendeza na yenye kuthawabisha hutokana na kutumia ile iitwayo na wengi Kanuni Bora. Yesu Kristo alisema: “Basi yo yote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo.” (Mathayo 7:12) Kwa Mkristo, pia kuna ile tamaa ya kumpendeza Yule aliyempa mwanadamu zawadi ya usemi. Mtunga-zaburi alisali hivi: “Maneno ya kinywa changu, na mawazo ya moyo wangu, yapate kibali mbele zako, Ee BWANA, mwamba wangu na mwokozi wangu.”—Zaburi 19:14.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki