Huduma Yetu—Kazi Inayoonyesha Huruma
1 Yesu aliona kwamba watu waliokuwa wakisikiliza ujumbe wake walikuwa “wamechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.” (Mt. 9:36) Kwa wororo na upendo, aliwafundisha viwango vya Yehova, akawafariji, na kwa huruma akawaandalia mahitaji yao ya kiroho. Tunapotafakari njia za Yesu, tunajifunza kufikiri na kuhisi kama yeye, na sifa hiyo ya huruma huonekana wazi katika huduma yetu.
2 Hebu tua kidogo na ufikirie jinsi Yesu alivyowatendea watu waliohitaji sana msaada walipomwendea. (Luka 5:12, 13; 8:43-48) Aliwajali wale waliokuwa na mahitaji ya pekee. (Marko 7:31-35) Alijali hisia za wengine na akawahangaikia. Hakutazama tu sura ya nje ya mtu. (Luka 7:36-40) Kwa kweli, Yesu aliiga kabisa huruma nyororo za Mungu wetu.
3 ‘Aliwasikitikia’: Yesu hakuhubiri ili kutimiza wajibu tu. ‘Aliwasikitikia’ watu. (Marko 6:34) Vivyo hivyo leo, sisi hatutangazi tu ujumbe bali tunajaribu kuokoa uhai wenye thamani. Jaribu kuelewa ni kwa nini watu huitikia ujumbe kwa njia fulani. Kwa nini wanahangaika au wana wasiwasi? Je, wamepuuzwa na kudanganywa na wachungaji wa dini za uwongo? Tukionyesha kwamba tunawajali wengine kikweli, huenda wakachochewa kusikiliza habari njema.—2 Kor. 6:4, 6.
4 Huruma hugusa mioyo. Fikiria kisa hiki: Mwanamke mmoja alifiwa na binti yake mwenye umri wa miezi mitatu. Mashahidi wawili walipomtembelea, aliwakaribisha akiwa na nia ya kupinga hoja zao kuhusu sababu za Mungu kuruhusu kuteseka. Hata hivyo, mwanamke huyo alisema hivi baadaye: “Walinisikiliza kwa huruma sana, na walipokuwa wakiondoka, nilihisi vizuri sana hivi kwamba nilikubali wanitembelee tena.” Je, wewe hujitahidi kumwonyesha huruma kila mtu unayemhubiria?
5 Kuwa wenye huruma kutatusaidia kuwafariji wengine kikweli. Kwa kuwa wenye huruma, tunamtukuza Yehova, “Baba ya rehema nyororo.”—2 Kor. 1:3.