Yehova Hutawala kwa Huruma
KATIKA historia yote watawala wengi wa kibinadamu wametumia mamlaka bila kuwahurumia raia wao wenye kuteseka. Hata hivyo, Yehova aliandaa jambo lililo tofauti kwa kuchagua taifa fulani—Israeli—na kulitawala kwa huruma.
Waisraeli walipokuwa bado watumwa katika Misri ya kale, Yehova alisikia kilio chao cha kutaka msaada. “Katika mateso yao yote yeye aliteswa, . . . kwa mapenzi yake, na huruma zake, aliwakomboa mwenyewe.” (Isaya 63:9) Yehova aliokoa Israeli, akawaandalia chakula cha kimuujiza, akawakomboa na kuwaingiza katika nchi yao wenyewe.
Sifa ya Yehova ya kuhurumia ilidhihirishwa zaidi katika sheria alizotolea taifa hilo. Aliwaamuru Waisraeli washughulike kwa huruma na mayatima, wajane, na wakazi-wageni. Hawakupaswa kuwatumia isivyo haki watu wasiojiweza ili kujinufaisha.
Sheria ilitaka wale wenye uhitaji wahurumiwe. Maskini wangekusanya masazo baada ya mavuno. Madeni yalifutwa mwaka wa Sabato (mwaka wa saba). Ilibidi mashamba yote yaliyorithiwa ambayo yalikuwa yameuzwa yarudishwe mwaka wa Yubile (mwaka wa 50). Kichapo Ancient Israel—Its Life and Institutions charipoti hivi: “Katika Israeli, kwa kweli hakukuwa matabaka ya kijamii katika maana ya kisasa.” “Mapema katika siku za kufanya makazi, Waisraeli wote walionea shangwe kwa kadiri fulani viwango vilevile vya maisha.”—Mambo ya Walawi 25:10; Kumbukumbu la Torati 15:12-14; 24:17-22; 27:18.
Kuiga Huruma ya Yehova
Watumishi wa Mungu huchochewa na huruma yake. Kwa kielelezo, katika historia yote, wafalme fulani waliotawazwa karibuni wamewaua washiriki waliobaki hai wa nasaba ya kifalme iliyotangulia. Lakini mtumishi wa Yehova, Daudi hakufanya hivyo. Baada ya kifo cha Mfalme Sauli, Daudi alimhami Mefiboshethi, mjukuu na mrithi aliyebaki hai wa Sauli. “Mfalme akamwachilia [“akamhurumia,” NW] Mefiboshethi, mwana wa Yonathani, mwana wa Sauli.”—2 Samweli 21:7.
Hakuna mwanadamu mwingine ambaye ameiga huruma ya Yehova kama vile Yesu alivyofanya. Mingi ya miujiza yake ilichochewa na huruma ya kimungu. Wakati mmoja mtu mwenye ukoma alimsihi sana hivi: “Ikiwa tu wewe wataka, waweza kunifanya safi.” Yesu alisukumwa na sikitiko, akamgusa akisema hivi: “Mimi nataka. Fanywa safi.” (Marko 1:40-42) Wakati mwingine umati mkubwa ulimfuata Yesu. Katikati ya hiyo rabsha, Yesu alikazia uangalifu wanaume wawili vipofu waliopaaza sauti hivi: “‘Bwana, uwe na rehema juu yetu, Mwana wa Daudi!’ . . . Akasukumwa na sikitiko, Yesu akagusa macho yao, na mara wakapata kuona.”—Mathayo 20:29-34.
Umati mkubwa haukufisha hisia za Yesu kwa wengine. Kwa sababu haukuwa umekula muda fulani, alisema hivi wakati mmoja: “Nahisi sikitiko kwa ajili ya umati.” Kwa hiyo akaulisha kimuujiza. (Marko 8:1-8) Yesu alipozunguka, hakuufunza umati tu bali pia alikuwa mwangalifu kuelekea mahitaji yao. (Mathayo 9:35, 36) Baada ya kuzunguka huko, Yesu na wanafunzi wake hawakuwa hata na wasaa wa kula mlo. Simulizi la Biblia latuambia hivi: “Kwa hiyo wakaenda zao wakiwa katika mashua wakawe mahali pa upweke peke yao wenyewe. Lakini watu wakawaona wakienda na wengi wakapata kujua hilo, na kutoka katika majiji yote wakakimbia kwenda huko pamoja kwa miguu na kufika mbele yao. Basi, aliposhuka, akaona umati mkubwa, lakini akasukumwa na sikitiko kwa ajili yao, kwa sababu walikuwa kama kondoo wasio na mchungaji. Naye akaanza kuwafundisha mambo mengi.”—Marko 6:31-34.
Mbali na ugonjwa na umaskini wa watu Yesu pia alisukumwa na hali yao ya kiroho. Viongozi wao walikuwa wakiwatumia kwa kujinufaisha, hivyo Yesu “akasukumwa na sikitiko kwa ajili yao.” Neno la Kigiriki “akasukumwa na sikitiko” lamaanisha “kuhisi kutamani sana kwa matumbo.” Yesu kwa kweli alikuwa mtu mwenye huruma!
Huruma Katika Ulimwengu Wenye Jeuri
Yesu Kristo sasa ni mfalme wa Ufalme wa kimbingu wa Yehova. Kama alivyofanya katika Israeli la kale, leo Mungu hutawala watu wake kwa huruma. “Nao watakuwa wangu, asema BWANA wa majeshi, katika siku ile niifanyayo; naam, watakuwa hazina yangu hasa; nami nitawaachilia [“nitawahurumia,” NW].”—Malaki 3:17.
Lazima wale watakao kuwa wapokeaji wa huruma ya Yehova waige njia zake. Ni kweli, twaishi katika ulimwengu ambamo watu wapendezwa zaidi na kuhifadhi mitindo-maisha yao kuliko kusaidia wale wenye uhitaji. Watu walio mamlakani mara nyingi hujaribu kupata faida huku wakidhabihu usalama wa wafanyakazi na wanunuzi wao. Kwenye 2 Timotheo 3:1-4, Biblia yafafanua kwa usahihi hali ya kiadili ya wakati wetu ambayo imeangamiza huruma mioyoni mwa watu wengi.
Hata hivyo, yaelekea twaweza kupata fursa za kuonyesha huruma. Je, twaweza kuwatolea majirani wetu msaada fulani ambao wahitaji? Je, kuna mtu fulani mgonjwa ambaye tungeweza kumzuru? Je, twaweza kuwatia moyo walioshuka moyo kulingana na shauri hili: “Semeni kwa kuliwaza nafsi zilizoshuka moyo, tegemezeni walio dhaifu”?—1 Wathesalonike 5:14.
Huruma itatusaidia pia tuepuke kuitikia kwa ukali wengine wafanyapo makosa. Twaambiwa hivi: “Acheni uchungu wote wenye nia ya kudhuru na hasira na hasira ya kisasi na kupiga kelele na usemi wenye kuudhi viondolewe mbali kutoka kwenu pamoja na ubaya wote. Bali iweni wenye fadhili nyinyi kwa nyinyi, wenye huruma kwa njia nyororo, mkisameheana kwa hiari mtu na mwenzake kama vile Mungu pia kupitia Kristo alivyowasamehe nyinyi kwa hiari.”—Waefeso 4:31, 32.
Huruma itatusaidia kuepuka mwelekeo wa kutumia vibaya mamlaka. Biblia yasema hivi: “Jivikeni wenyewe shauku nyororo za huruma, fadhili, hali ya akili ya kujishusha chini, upole, na ustahimilivu.” (Wakolosai 3:12) Hali ya akili ya kujishusha chini hutuwezesha tujiweke katika hali ya wale walio chini ya usimamizi wetu. Kuwa wenye huruma huhusisha kuwa wanyenyekevu na wenye kukubali sababu kuliko kuwa wagumu kupendeza. Utendaji bora wa kazi haupasi kuwa sababu ya kuwatendea wengine kama sehemu tu za mashine. Pia, katika familia waume wenye huruma hukumbuka kwamba wake zao ni vyombo dhaifu zaidi. (1 Petro 3:7) Kufikiria kwa makini kielelezo cha Yesu cha huruma kwaweza kutusaidia katika mambo haya yote.
Kwa kuwa Yesu aliwahurumia watu sana wakati alipohudumu duniani, twaweza kuwa na hakika kwamba yeye sasa ni Mtawala mwenye huruma, na ataendelea kuwa hivyo. Zaburi ya 72 yasema kiunabii hivi juu yake: “Atawahukumu walioonewa wa watu, atawaokoa wahitaji, atamseta mwenye kuonea. Na awe na enzi toka bahari hata bahari, toka Mto hata miisho ya dunia. Atamhurumia aliye dhaifu na maskini, na nafsi za wahitaji ataziokoa.”—Zaburi 72:4, 8, 13.
Neno la Mungu latabiri hivi: “Kwa haki atawahukumu maskini, naye atawaonya wanyenyekevu wa dunia kwa adili . . . atawaua wabaya.” Baada ya kufafanua jinsi watu fulani wenye jeuri na walio kama hayawani watakavyobadili njia zao, huo unabii waendelea kusema hivi: “Hawatadhuru wala hawataharibu katika mlima wangu wote mtakatifu; maana dunia itajawa na kumjua BWANA, kama vile maji yanavyoifunika bahari.” (Isaya 11:4-9) Kwa kweli unabii huu waahidi kuwako kwa jamii ya duniani pote ya watu wamjuao Yehova na kuiga njia zake zenye huruma!