Programu Mpya ya Kusanyiko la Pekee
Wakiwa wametiwa nguvu na roho takatifu, Wakristo wa mapema walifanya kazi kwa bidii ili kueneza habari njema kwa kadiri kubwa iwezekanavyo. (Mdo. 1:8; Kol. 1:23) Programu ya kusanyiko la pekee ya mwaka wa utumishi wa 2007 yenye kichwa, “Shughulika Sana na Lile Neno,” itatutia moyo kuiga mfano wao bora.—Mdo. 18:5.
Akieleza kuhusu Neno la Mungu Mfalme Daudi alisema: “Kikumbusho cha Yehova ni chenye kutegemeka, humfanya asiye na uzoefu awe na hekima.” (Zab. 19:7) Programu ya kusanyiko la pekee la 2007 iliyotayarishwa kwa makini, itakazia umuhimu wa maandiko katika “kunyoosha mambo” nayo itatutia moyo tutumie Neno la Mungu kuhubiri tukiwa na hisi ya uharaka. (2 Tim. 3:16, 17) Programu hiyo mpya itaonyesha jinsi tunavyoweza kuepuka hatari na jinsi ya kujinufaisha kwa kuishi kulingana na kanuni za Biblia kila siku. Pia itatuonyesha jinsi tunavyoweza kutumia Neno la Mungu kuwasaidia vijana na wapya wafanye maendeleo ya kiroho.
Hakikisha upo programu inapoanza, na usikilize kwa makini. Andika mambo unayoweza kutumia kibinafsi. Onyesha unathamini maagizo na vikumbusho vitakavyotolewa, na utafakari jinsi utakavyotumia mambo utakayojifunza.
Programu ya kusanyiko la pekee itaongeza uthamini wetu wa Neno la Mungu, itatukumbusha kuendelea kuhubiri habari njema za Ufalme kwa bidii, na kutuonyesha jinsi tunavyoweza kuwasaidia wengine wafanye vivyo hivyo. Kwa hiyo, azimia kutokosa mwelekezo na maagizo yote ambayo Yehova atatuandalia!—Isa. 30:20b, 21.