Barua Kutoka Ofisi ya Tawi
Wahubiri wa Ufalme Wapendwa:
Tungependa kuwashukuru kwa msaada wenye upendo ambao mliwatolea ndugu na dada wengi walioathiriwa na ukame na mafuriko ambayo yalisababisha upungufu wa chakula katika wilaya fulani kwenye eneo letu.—Yoh. 13:35.
Ndugu mmoja aliyepokea msaada wa chakula alisema: “Msaada ulikuja kwa wakati uliofaa kabisa. Tunamshukuru sana Yehova na tengenezo lake kwa msaada huu. Tumeshuhudia upendo halisi unaotambulisha Wakristo wa kweli.” Michango yenu kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote inathaminiwa sana.
Kwa mfano, huko Marekani maelfu ya ndugu na dada walipokea msaada wenye upendo walipoathiriwa na tufani zilizoharibu eneo la Ghuba ya Pwani mwaka wa 2005. Zaidi ya ndugu na dada 8,000 waliokuwa wakifanya kazi chini ya Halmashauri za Ujenzi za Mkoa zipatazo 60 walitoa muda wao, ujuzi, na mali zao ili kuwasaidia wengine. Walirekebisha na kujenga upya Majumba ya Ufalme 86 na nyumba 4,178. Ili waweze kusaidia, baadhi ya akina ndugu walisafiri kutoka maeneo yote ya nchi ya Marekani. Tunathamini kama nini jitihada zao za upendo!—1 The. 5:18.
Mjitoleaji mmoja kutoka Michigan alisema: “Nilifurahi sana kuona tabasamu za familia mbalimbali walipoona paa mpya tulizoezeka kwenye nyumba zao. Siwezi kueleza jinsi ninavyohisi kuwa sehemu ya undugu huu wa ajabu.” Kwa kweli huo ni mfano mzuri wa jinsi ya kuwasaidia wale waliokumbwa na janga hilo.
Tunaomba mwendelee kusali kwa ajili ya ndugu zetu wapendwa ambao huenda wameathiriwa na majanga mengi yanayotokea siku hizi za mwisho na vilevile kwa ajili ya wanaotoa msaada.—2 Kor. 1:11.
Ndugu zenu,
Ofisi ya Tawi ya Burundi, Kenya, Sudan, Tanzania, na Uganda