Kuhubiri Nyumba kwa Nyumba
1 “Wale wenye uzoefu katika njia mbalimbali za kueneza Kweli wanakubali kwamba kuhubiri nyumba kwa nyumba kwa kutumia vitabu vya MILLENNIAL DAWN kwa sasa ndiyo njia bora zaidi ya kuhubiri Kweli.” Maneno hayo ya toleo la Zion’s Watch Tower la Julai 1, 1893, yalionyesha umuhimu wa huduma ya nyumba kwa nyumba. Watu wanaiona huduma hiyo kuwa alama ya kuwatambulisha Mashahidi wa Yehova duniani kote. Kwa vile inakuwa vigumu zaidi kuwakuta watu nyumbani katika baadhi ya nchi je, bado njia hii ni muhimu?
2 Kazi Muhimu Inayopatana na Maandiko: Mahubiri ya nyumba kwa nyumba yana msingi wa Kimaandiko. Yesu aliwaagiza wanafunzi wake 70 waende wawili-wawili kwenye nyumba za watu. (Luka 10:5-7) Muda mfupi baada ya kifo cha Yesu, Biblia inasema hivi kuhusu wanafunzi wake: “Na kila siku katika hekalu na nyumba kwa nyumba wakaendelea bila kuacha kufundisha na kutangaza habari njema.” (Mdo. 5:42) Mtume Paulo pia alifundisha kwa bidii nyumba kwa nyumba.—Mdo. 20:20.
3 Leo, kuhubiri nyumba kwa nyumba bado ni njia muhimu ya kueneza habari njema. Kunatuwezesha ‘kutafuta’ wanaostahili kwa mpango na utaratibu. (Mt. 10:11) Kwa kawaida watu huwa wametulia zaidi nyumbani kwao. Kuongea nao ana kwa ana—kusikia sauti zao, kuona jinsi wanavyoitikia, na kuona mazingira yao—kunatusaidia kutambua mapendezi yao na mambo yanayowafadhaisha. Kwa kawaida tunapata nafasi nzuri ya kuwa na mazungumzo marefu.
4 Rekebisha Ratiba Yako: Mtume Paulo alikuwa tayari kubadili ratiba yake “kwa ajili ya habari njema.” (1 Kor. 9:23) Labda unaweza kubadili ratiba yako ili uhubiri wakati unapoweza kuwakuta watu wengi nyumbani kama vile, jioni, mwisho wa juma, au siku kuu. Weka rekodi ya nyumba ambazo huwakuti watu kisha jaribu kurudi tena siku tofauti au wakati tofauti.
5 Hata wale wenye matatizo ya kiafya wanaweza pia kushiriki mahubiri ya nyumba kwa nyumba. Labda tunaweza kufanya mipango ya kwenda nao kwenye nyumba ambazo zinafikika kwa urahisi na kuwaacha wahubiri kwa mwendo wanaoweza. Dada mmoja aliyekuwa na shida ya kupumua angeweza kufanya nyumba moja tu kwa kila nusu saa. Lakini alifurahi na kuridhika sana aliposhiriki mahubiri pamoja na wengine!
6 Watu wengi wenye mfano wa kondoo wanaendelea kupatikana katika mahubiri ya nyumba kwa nyumba. Mhubiri mmoja alipobisha mlango aliambiwa: “Karibu. Najua wewe ni nani. Nimekuwa nikiomba Mungu atume mtu anisaidie, kisha ukabisha. Alinisikia, akakutuma.” Matokeo yanathibitisha kwamba Yehova anabariki njia hii ya kuhubiri. (Mt. 11:19) Azimia kufanya mahubiri ya nyumba kwa nyumba yawe sehemu ya kawaida ya utumishi wako.
[Maswali ya Funzo]
1. Ni swali gani linalotokea kuhusiana na huduma ya nyumba kwa nyumba, na kwa nini?
2. Kuna msingi gani wa Kimaandiko wa kuhubiri nyumba kwa nyumba?
3. Kuna faida zipi za kuhubiri nyumba kwa nyumba?
4. Tunaweza kufanyaje mahubiri ya nyumba kwa nyumba yawe yenye matokeo zaidi?
5. Wale wenye matatizo ya kiafya wanaweza kuhusishwaje katika mahubiri ya nyumba kwa nyumba?
6. Kwa nini tufanye mahubiri ya nyumba kwa nyumba yawe sehemu ya kawaida ya utumishi wetu?