Nyumba kwa Nyumba Bila Kuacha
1 Katika Israeli ya kale, dhabihu zilitolewa kila siku. (Kut. 29:38-42) Moto wa madhabahu uliachwa ukiwaka; nao moshi uliofuka ulikuwa “harufu nzuri” iliyompendeza Yehova. (Kut. 29:18) Leo, twasihiwa “tumpe Mungu dhabihu ya sifa daima, yaani, tunda la midomo iliungamayo jina lake.” (Ebr. 13:15) Badala ya kutumia dhabihu zilizoamriwa na Sheria, twamwabudu Yehova kwa kusimulia sifa zake bila kuacha.—Isa. 43:21; Mdo. 5:42.
2 Yesu Kristo, yule Shahidi mkubwa zaidi aliyepata kuishi duniani, alitufundisha jinsi twapaswa kutoa ibada safi kwa kutoa dhabihu za sifa. Alifundisha wanafunzi wake kwamba kulikuwa na uharaka wa ujumbe waliouhubiri. Alijua kwamba njia bora zaidi yenye matokeo ya kufikia watu na habari njema ilikuwa ni kwa kuongea nao kibinafsi nyumbani mwao. (Mt. 10:7, 12) Kwa hiyo twaona kwamba mitume walifuata mwongozo uliovuviwa kimungu wa kuhubiri nyumba kwa nyumba.—Mdo. 20:20.
3 Hakuna tofauti leo. Wakiwa wanafunzi wa Yesu, Wakristo wa kweli hufuata kielelezo chake kwa kuhubiri habari njema nyumba kwa nyumba. Ijapokuwa huenda tukachambuliwa na kunyanyaswa kwa jambo hilo, mamilioni wamejifunza kweli na mamia ya maelfu ya wanafunzi wapya wanajiunga na umati mkubwa kila mwaka, wakitoa uthibitisho kwamba hii ndio njia ya Yehova ya kutimiza mapenzi yake. Ndio kwa sababu tunadumu katika huduma yetu.
4 Manufaa za Kuhubiri Nyumba kwa Nyumba: “Mungu hana upendeleo . . . Mtu amchaye na kutenda haki hukubaliwa na yeye.” (Mdo. 10:34, 35) Kwenda moja kwa moja katika kila nyumba kwenye eneo letu kwaonyesha kwa wazi kutokuwa na ubaguzi, tukimpa kila mtu fursa ya kusikiliza ujumbe wa Ufalme kwa ukawaida. Kisha wenye kukubali wanapokea msaada wa binafsi kulingana na mahitaji yao wakiwa mmoja-mmoja.
5 Karibu wahubiri wote, kutia ndani wachanga, wazee-wazee, na hata wale wapya, wanaweza kushiriki katika mahubiri ya nyumba kwa nyumba. Kwa njia hii kila mtu aweza ‘kukiri hata kupata wokovu.’ (Rum. 10:10) Kushiriki na wengine katika huduma ya nyumba kwa nyumba hutuunganisha katika vifungo vya upendo na umoja. Wakati uleule, tunapewa fursa ya kuonyesha uvumilivu wetu tunapopata ubaridi au upinzani. Kuonyesha imani yetu peupe hutufanya tuwe “tamasha kwa dunia,” ambayo husaidia watu wenye mioyo minyoofu watambue kwamba tuna mpango uliopangwa vizuri wa kufundisha Biblia na kwamba wanaweza kunufaika kutokana nao. (1 Kor. 4:9) Kila kitu chaonyesha waziwazi kwamba Yehova anabariki mahubiri ya nyumba kwa nyumba naye anaitumia kukusanya umati mkubwa kwenye “nyumba” yake ya ibada safi.—Isa. 2:2-4.
6 Sasa kuliko wakati mwingine wowote wa historia, watu wanahitaji kusikia ujumbe wa Ufalme. Na tuendelee kuhubiri nyumba kwa nyumba bila kuacha hadi Yehova aseme imetosha. (Isa. 6:11) Kwa kufanya hivyo, tutathawabishwa na shangwe ambayo hutokana na kushiriki katika huduma ya maana na yenye kunufaisha ya nyumba kwa nyumba wakati huu wa mwisho.—1 Kor. 15:58.