Wewe Unatanguliza Nini?
1 Ungejibuje swali hilo? Bila shaka, sisi sote hutamani kutanguliza mambo ya Ufalme. (Mt. 6:33) Lakini huenda tukajiuliza, ‘Je, mambo ninayochagua kufanya yanaonyesha kwamba ninatanguliza Ufalme?’ Biblia inatutia moyo hivi: “Endeleeni kuthibitisha ninyi wenyewe jinsi mlivyo.” (2 Kor. 13:5) Tunaweza kujithibitishiaje kwamba tunatanguliza Ufalme?
2 Jinsi Unavyotumia Wakati: Tunaweza kuanza kwa kuchunguza jinsi tunavyotumia wakati wetu. (Efe. 5:15, 16) Tunatumia wakati mwingi kadiri gani kila juma pamoja na marafiki, kutazama televisheni, kutumia Intaneti, au kufanya jambo fulani tunalopenda? Tukiandika wakati ambao tunatumia kufanya mambo hayo na tuulinganishe na wakati tunaotumia katika utendaji wa kiroho, huenda tukashangaa. Je, tunatumia wakati mwingi sana kazini bila kujali utumishi mtakatifu ili tu tuwe na pesa za kutosha kwa ajili ya vitu vya bei ghali? Ni mara nyingi kadiri gani tunadhabihu mikutano au mahubiri ili tusafiri katika miisho ya juma kwa ajili ya tafrija?
3 Panga Mambo ya Kutanguliza: Wengi kati yetu hawana wakati wa kutosha kufanya kila jambo wanalotaka. Hivyo, ili kutanguliza mambo ya Ufalme, tunahitaji kuchunguza mambo tunayotanguliza kisha tupange wakati kwa ajili ya “mambo yaliyo ya maana zaidi.” (Flp. 1:10) Mambo hayo yanatia ndani kujifunza Neno la Mungu, kushiriki katika huduma, kutunza familia, na kuhudhuria mikutano ya Kikristo. (Zab. 1:1, 2; Rom. 10:13, 14; 1 Tim. 5:8; Ebr. 10:24, 25) Utendaji mwingine, kama vile mazoezi ya kiasi na tafrija zinazofaa ni muhimu. (Marko 6:31; 1 Tim. 4:8) Lakini mambo hayo yasiyo ya maana sana yanapaswa kuwekwa mahali pake.
4 Ndugu mmoja kijana aliamua kutanguliza mambo ya Ufalme kwa kuwa mtumishi wa wakati wote badala ya kufuatia elimu ya juu ili apate kazi ya kimwili. Alijifunza lugha nyingine na kuhamia eneo lenye uhitaji mkubwa. Alisema: “Ninafurahia maisha kabisa huku. Utumishi unaburudisha sana! Laiti vijana wote wangefanya jambo kama hilo na kupata uradhi. Hakuna jambo bora kuliko kumtumikia Yehova kwa nafsi yote.” Naam, kutanguliza Ufalme hutuletea baraka, lakini, la muhimu zaidi, humfurahisha Baba yetu wa mbinguni, Yehova.—Ebr. 6:10.