Elekezea Sana Fikira Mpango wa Kibinafsi
1 “Ukitaka kazi fulani ifanywe, mpe mtu mwenye shughuli nyingi.” Wazo linalohusiana na usemi huu ni kwamba kwa kawaida mtu mwenye shughuli nyingi huwa amepanga mambo vizuri na kwa hivyo anaweza kutimiza mengi. Sisi sote tuna saa 24 za kutumia kila siku. Kama tukiupoteza wakati huo au tukiutumia vizuri mara nyingi inategemea utaratibu wetu wa kibinafsi.
2 Sikuzote kuna “mengi ya kufanya katika kazi ya Bwana.” (1 Kor. 15:58, NW) Tuna mikutano ya kuhudhuria na kushiriki huduma ya shambani. Lakini kujitayarisha kunatangulia haya. Ndiyo kusema, tunahitaji kutumia wakati tukijifunza ili ‘tufanye wanafunzi’ kwa matokeo na tuchochee wengine “katika upendo na kazi nzuri,” sawa na tulivyoamuriwa kufanya. (Mt. 28:19; Ebr. 10:24) Mambo ya kawaida maishani, kama vile kazi ya kimwili, kununua vitu, kula, kusafisha, kusafiri, kuhudhuria shule, na kulala, yote yana mahali payo. Wakati fulani unaweza kutumiwa katika tafrija pia. Kuweka kila kitu mahali pacho panapokifaa kunatokeza mwito wa ushindani tunaolazimika kukabili. Tunaweza kufanyaje hivyo?
KUWEKA MAMBO YA KUTANGULIZWA KWANZA
3 Yesu alisema: “Basi utafuteni kwanza ufalme wake, na haki yake; na hayo yote mtazidishiwa.” (Mt. 6:33) Kwa wazi, masilahi ya ufalme yanapasa kutangulizwa kwanza matumizi ya wakati wetu yanapohusika. Ikiwa tungehitaji kuratibu wakati wetu katika njia ile tunayopangia matumizi ya pesa zetu, wakati tunaoweka kando kwa ajili ya mikutano ya Kikristo, funzo la Biblia la jamaa, na utendaji wa kitheokrasi kama huduma ya shambani na funzo la kibinafsi haungetumiwa kufuatia masilahi mengine.
4 Katika kila ratiba lazima mambo ya maisha yanayohitajiwa sana yaingizwe. Wakati unawekwa kando wa kufanya kazi ya kimwili na kujitegemeza mwenyewe na jamaa ya mtu. Lazima kula na kulala, na pia kuelekezea fikira kibinafsi mahitaji ya jamaa ya mtu yatiwe ndani pia. Katika orodha ya mambo ya kutangulizwa kwanza ya wazee na watumishi wa huduma mambo yaliyo juu ni wakati wanaotumia kutayarisha kwa ajili ya na kutimiza madaraka ya kiroho. Mbona usiketi chini na ufanye ratiba kama hiyo, na uone kama kuna mambo yasiyo ya maana sana yaliyo juu katika orodha yako ya mambo ya kutangulizwa kwanza kuliko yanavyohitajiwa kuwa.
KUENDELEZA JICHO RAHISI
5 Yesu alipokuwa akizungumzia utendaji wa wafuasi wake, yeye alitaarifu hivi: “Ikiwa, basi, jicho lako ni rahisi mwili mzima wako utakuwa mwangavu.” (Mt. 6:22, NW) Hii ingetia ndani nini? Kwa msingi inamaanisha kuendeleza maisha yasiyotatanisha. Kuna vikengeusha-fikira vingi vinavyoweza kupokonya wakati wa mtu. Televisheni ni mojapo mambo haya. Katika nyumba fulani, televisheni hufunguliwa asubuhi na kuachwa hivyo siku nzima. Mtu anaweza kuketi chini akatazame kipindi kifupi. Lakini anapata kwamba wakati ule aliokuwa amepangia hapo awali kuutumia kwa ajili ya funzo la kibinafsi au pamoja na jamaa unaponyoka anapoendelea kutazama vipindi vingine. Jinsi ilivyo rahisi kupoteza jioni nzima bila kutimiza jambo lolote lenye mafaa! Watu wengine hawajui wakati wa kuzima televisheni. Ikiwa wewe una tatizo hili, huenda ukaamua kwamba hakuna haja ya kufungulia televisheni. Kazi anayofanya mtu kupisha wakati tu, ambayo ni njia ya kustarehe kwa watu fulani, inaweza kuchukua wakati ambao ulikuwa umewekwa kando kwa mambo mengine yenye maana zaidi.
6 Kujihusisha katika utendaji wa michezo, kuhudhuria matukio ya michezo, au kuyatazama kwenye televisheni kunaweza kumeza wakati wenye thamani. Waume, wake, na watoto, wanafanya vema kuhakikisha kwamba hawapokonywi wakati ambao wangeweza kutumia kujifunza au kushiriki pamoja. Sisi sote tunapasa kuwa waangalifu tusifanye maisha yetu yawe yenye kutatanisha kwa michezo na tafrija zenye kupita kiasi.
7 Tatizo zito linaweza kutokea ikiwa tunaruhusu kazi ya kimwili ijiingize katika wakati wa kutangulizwa kwanza. Huenda wengine wakajikuta wakiwa wamejishughulisha sana katika kazi yao au wakihangaikia sana mataraja ya faida za kifedha hivi kwamba hawana tena mahali katika ratiba yao kwa ajili ya mikutano, huduma ya shambani, au hali ya kiroho ya jamaa yao. (Efe. 5:15, 16) Ni vema tujiulize wenyewe, ‘Ni nani ambaye angefurahishwa sana na kutolea kwangu masilahi ya kimwili wakati ambao tayari nimeuweka wakfu kwa ibada ya Yehova Mungu?’
NJIA ZA KUTUMIA WAKATI KWA MATOKEO MAZURI
8 Kupanga maisha ya mtu kwa ajili ya matumizi ya wakati yenye matokeo zaidi kunahitaji kuwa na miradi ya kiroho na fungu lenye kueleweka wazi la thamani. Huu ndio ufunguo wa kuweka mambo ya kutangulizwa kwanza kila siku. Usiahirishe mambo. Ikiwa umeweka kando wakati wa kufanya kazi fulani, utumie kwa kusudi hilo. Jiwekee mipaka ya saa unazopaswa kuwa umetimiza mambo. Jitahidi kujifunza habari fulani kwa wakati wa kutosha ili uitumie katika huduma ya shambani na mikutanoni. Fanya hivyo hivyo kuhusiana na kazi za kila siku nyumbani.
9 Jizoeze kutumia wakati ambao ungeweza kupotezwa. Kwa kielelezo, wakati unapolazimika kuwangojea wengine, tumia wakati huo vizuri kwa kusoma, kuandika barua, au kutimiza kazi nyingine ya maana. Ukijikuta ukiwa kwenye mstari wa kungojea, huenda ukaanzisha mazungumzo yanayoweza kuongoza kwenye kutoa ushuhuda. Jambo lingine la maana kwa wote ni kupata pumziko na tafrija ya kutosha ili kubaki mwenye afya nzuri na mwepesi. Hii itakusaidia kufanya kazi kwa njia yenye matokeo zaidi. Magonjwa yanayotokea kwa sababu ya kukosa pumziko au usingizi unaohitajiwa sana yanaweza kukufanya usielekezee fikira mambo ya kutangulizwa maishani.
KUFANYIA MAENDELEO MPANGO WA KIBINAFSI
10 Katika ulimwengu wa biashara, wakati na jitihada nyingi inatumiwa katika kupanga tu jinsi kazi fulani itakavyotimizwa. Mwanabiashara mzuri anapata kuwa ni jambo lenye matokeo kupanga wafanya kazi na vifaa kabla ya kutokeza kazi iliyotolewa. Yeye anatambua kwamba ikiwa wafanya kazi na vifaa vinavyohitajiwa kabisa havipo mahali na wakati vinapohitajiwa, wakati na pesa nyingi zinaweza kupotezwa naye hatapata faida. Hata hivyo, sisi tuna sababu kubwa za kupanga mambo sisi wenyewe. Hii inatia ndani tamaa yetu ya kudumisha uhusiano bora pamoja na Yehova, kuwa wenye matokeo katika kufanya wanafunzi, na kufikia mradi wetu wa uhai wa milele. Kwa hiyo, ni jambo linalohitajiwa tuhakikishe kwamba tuna vyombo vinavyofaa katika wakati unaofaa.
11 Kwa kielelezo, kila juma tuna mikutano mitano ya kundi. Msingi wa habari za mikutano hii unatoka katika vichapo tofauti tofauti. Je! vichapo hivi vinapatikana kwa urahisi? Je! Mnara wa Mlinzi tunaojifunza juma hilo umewekwa kando, au wakati unatumiwa kuutafuta-tafuta? Namna gani vichapo vingine vinavyohitajiwa, kama vile Huduma ya Ufalme Yetu, kitabu cha nyimbo, Biblia, na kichapo tunachojifunza kwenye Funzo la Kitabu la Kundi? Ni vizuri kuwa na mahali palipochaguliwa pa kuweka vifaa hivyo na kuviweka hapo wakati ambao havitumiwi. Katika njia hii, tunaweza kupata kichapo kinachofaa tunapotayarisha kwa ajili ya utumishi wa shambani au mikutano.
12 Wazee na watumishi wa huduma hasa wanahitaji kuangalia mpango wao kibinafsi. Wakiwa na mambo mengi sana ya kufanya, kimwili na katika kundi, nyakati nyingi “mambo yaliyo ya maana zaidi” yanaweza kusahaulika au kuwekwa kando. (Flp. 1:10, NW) Kutumia dokezo la kuwa na orodha ya mambo ya kutangulizwa kwanza kunaweza kuwa na mafaa kweli kweli. Je! wewe umejaribu hivyo? Ndugu mmoja ana orodha kama hiyo naye huirudia kabla ya kila mkutano. Kwa njia hiyo yeye anatimiza mengi na anaweza kuhakikisha kwamba kazi inayohitajiwa sana ya kundi inafanywa.
13 Wazee wanapasa kuwa na utaratibu mzuri wa kufuatia barua za kundi. Nyakati nyingine kazi ya kushughulika na karatasi inaweza kuvuruga na kusumbua ikiwa haijapangwa vizuri. Kwa hiyo, ni vizuri kuchukua dakika chache kwa ukawaida kupanga makaratasi yanayohitaji kuwekwa au kupitishwa kwa mtu mwingine na kutupa yale yanayoweza kuharibiwa. Ikiwa una barua ambazo zinahitaji kupitishwa kwa wazee wengine, hakikisha unazipeleka upesi. Kuchagua mahali katika mkoba wako au labda kuweka barua katika bahasha tofauti au folda kunaweza kukusaidia kufuatia barua na habari nyingine inayohitaji kuelekezewa fikira. Katika njia hii, kazi ya kushughulika na karatasi iliyo ya maana haitapotea au kukawizwa.
MPANGO—MTUMWA SI BWANA-MKUBWA
14 Baada ya kurudia ratiba yako, amua ni mpango wa kiasi gani unaohitaji. Hatutaki kuwa wataka-ukamilifu wasio na msingi, kupanga maisha yetu ya kibinafsi kupita kiasi hivi kwamba hakuna nafasi ya kufanya mabadiliko. Kumbuka, sisi sote ni watu mmoja mmoja na sisi sote tuna hali za kipekee. Wengine wetu ni waseja, wengine wameoa au kuolewa. Jambo linaloweza kufaulu kwa jamaa moja huenda lisifaulu kwa nyingine. Tunapasa kufikiria hali zetu za kibinafsi na kijamaa tunapopanga mambo ya kibinafsi. Tumia utambuzi na uwe mwenye kupindika kulingana na kanuni za Biblia ambazo zitatumika kukuongoza ili uwe na ratiba yenye mafanikio.—Ona Mnara wa Mlinzi wa Septemba 15, 1988, kurasa 28-30; Amkeni! ya Machi 8, 1989; na Amkeni! (Kiingereza) ya Desemba 22, 1965, kurasa 9-12.
15 Katika miaka ya majuzi, kurahisisha mambo kupitia kufuata kanuni zenye utaratibu mzuri kumetokeza utendaji uliofanyiwa maendeleo katika kuendesha tengenezo la Yehova la kidunia. Huenda wengine wakahisi kwamba wana njia zinazofaulu kibinafsi. Wangependa Sosaiti iwatie moyo wengine watumie njia kama hizo, lakini mara nyingine hizo zimefikiriwa na kutupiliwa mbali kwa sababu hazifai kitengenezo. Kwa masilahi ya umoja na utendaji mzuri basi, ni jambo la hekima kufuata utaratibu wa kitegenezo uliofanyiwa maendeleo, kutumia njia zinazoeleweka na zinazotumiwa na wengine ambao huenda wakaathiriwa na kazi yako.
16 Yehova ni Mungu wa utaratibu na amani. (1 Kor. 14:33, 40) Ana wakati alioweka kutimiza penzi na kusudi lake. (Mdo. 1:7) Kupitia Neno lake, ameonyesha kwa upendo yale ambayo yanapasa kutuhangaisha sisi wanadamu wasiokamilika. Kwa mwelekezo kutoka kwa Yesu Kristo kupitia “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” Yehova anaandaa maagizo yenye msaada kuhusu jinsi ya kutimiza kazi ya maana zaidi inayofanywa leo. (Mt. 24:45-47; 28:19, 20; Mhu. 12:13) Kwa hivyo kwa kufuata ombi la Kimaandiko linalopatikana katika vichapo vya Sosaiti, kutia vikumbusha vya wakati unaofaa vinavyoonyeshwa katika nyongeza hii, tunaweza kuwa na mpango mzuri wa kutimiza huduma yetu kikamili.—2 Tim. 4:5.