Jinsi ya Kukomboa Wakati
1 Kuwa na mengi ya kufanya katika utumishi wa Yehova hutushughulisha! (1 Kor. 15:58) Twatambua uhitaji wa kujifunza kibinafsi na tukiwa familia, kuisoma Biblia kila siku, kutayarisha na kuhudhuria mikutano ya kutaniko, na kushiriki kwa ukawaida katika huduma ya shambani. Waangalizi wana madaraka ya uchungaji, nao hushughulikia wajibu mwingine mbalimbali wa kutaniko. Watu fulani wana madaraka mazito ya familia au unamna-namna wa wajibu kwa wengine. Ili kufanya mambo yote ifaavyo, kila mtu ahitaji usawaziko na utaratibu mzuri wa kibinafsi.
2 Weka Mambo ya Kutangulizwa: Mafanikio katika ‘kukomboa wakati’ yategemea ufahamu na uamuzi wetu mzuri. (Efe. 5:15, 16) Ni lazima tuamue “mambo yaliyo ya maana zaidi” na kuyaweka kwanza katika orodha yetu ya mambo ya kutangulizwa. (Flp. 1:10) Wenzi fulani waliifafanua nyumba yao ya kitheokrasi kwa njia hii: “Twajaza ile kweli maishani mwetu . . . Kweli si sehemu ya maisha yetu, ndiyo maisha yetu. Kila jambo jingine huizunguka.” Kutanguliza ibada na utumishi wa Yehova maishani mwa mtu ni jambo la maana.
3 Tambua Mambo Yapotezayo Wakati: Kuna muda wa saa 168 katika juma moja, nasi twahitaji kutumia kwa hekima wakati tulio nao. Ili kuwa na wakati wa kutosha kwa ajili ya utendaji mbalimbali wa kitheokrasi, twahitaji kutambua na kupunguza mambo yapotezayo wakati. Uchunguzi mmoja ulifunua kwamba mtu mzima wa kawaida katika Marekani hutumia muda wa saa zaidi ya 30 kwa juma akitazama televisheni! Katika jumuiya ya Afrika Mashariki, kutazama vidio kumekuja kupendwa na watu wengi. Kwa wengine, wakati mwingi hutumiwa wakisoma fasihi za kilimwengu. Huenda watu fulani wakaona kwamba wao hutoa kiasi kingi mno cha wakati kwa utendaji mbalimbali wa kijamii, shughuli za kujifurahisha, tafrija, na aina fulani ya utendaji wa kompyuta. Huenda tukahitaji kuchunguza kwa ukaribu utaratibu wetu wa kila siku ili tuone jinsi tuwezavyo kutumia wakati wetu vizuri zaidi. Hekima hutaka kwamba tuwekee mipaka kadiri ya wakati turuhusuyo kwa utendaji usio wa maana.
4 Sitawisha Utaratibu Mzuri: Hali zetu za kibinafsi ziwe zipi, kila mmoja wetu aweza kukomboa wakati kwa ajili ya ufuatiaji mbalimbali wa kiroho. Watu fulani wamepata kwamba kuamka mapema zaidi kila siku huwasaidia kutimiza zaidi. Ikiwa sisi hutumia wakati mwingi kusafiri kwenda kazini au kuwangojea wengine, twaweza kutumia kiasi cha wakati huo kwa usomaji wa Biblia, kutayarishia mikutano, au kusikiliza habari inayoandaliwa na Sosaiti katika kaseti. Familia hufaidika sana kwa kuweka kando wakati hususa, wa kawaida ili kujifunza pamoja. Ikiwa kila mshiriki wa familia anawahi anapohudhuria funzo la familia, kila mmoja afaidika kwa kutopoteza wakati.
5 Kila siku ipitayo, twapaswa kuzidi kutambua kwa makini kwamba “muda ubakio si mwingi.” (1 Kor. 7:29) Uhai wetu wategemea jinsi tutumiavyo wakati wenye thamani ubakio. Tutabarikiwa tukikomboa wakati ili tuweze kutanguliza masilahi ya Ufalme!—Mt. 6:33.