Angalia Sana Jinsi Unavyotumia Wakati
1 Siku hizi ambapo kuna vyombo vinavyookoa wakati na kurahisisha kazi, watu wengi hujikuta wakiwa na mambo mengi ya kufanya na wakati mchache wa kuyafanya. Je, wewe huona ni vigumu kudumisha kawaida nzuri ya kiroho? Je, unatamani kuwa na wakati zaidi kwa ajili ya huduma? Tunaweza kutumiaje wakati wetu kwa njia nzuri zaidi?—Zab. 90:12; Flp. 1:9-11.
2 Tambua Mambo Yanayopoteza Wakati: Sisi sote tunapaswa kujichunguza mara kwa mara kuhusu jinsi tunavyotumia wakati wetu. Biblia inatuhimiza hivi: “Endeleeni kuangalia sana kwamba jinsi mnavyotembea si kama watu wasio na hekima bali kama watu wenye hekima, mkijinunulia wakati unaofaa, kwa sababu siku hizi ni zenye uovu.” (Efe. 5:15, 16) Fikiria magumu yanayotokezwa na maendeleo katika teknolojia ya habari. Ingawa kompyuta na vyombo vingine vya elektroni vina matumizi mazuri, vinaweza kuwa mtego tukishindwa kuangalia sana jinsi tunavyotumia wakati wetu.—1 Kor. 7:29, 31.
3 Kila mmoja wetu anapaswa kujiuliza: ‘Je, mimi hutumia wakati kila siku nikisoma au nikijibu ujumbe wa barua-pepe ambao ni usumbufu mtupu tu? Je, mara nyingi mimi hujishughulisha kupiga simu au kutuma ujumbe wa elektroni kuhusu mambo madogo-madogo? (1 Tim. 5:13) Je, mimi husoma-soma Intaneti bila kusudi lolote au kubadili-badili kituo cha televisheni bila lengo? Je, kujishughulisha mno na michezo ya kompyuta kumeanza kuingilia funzo langu la Neno la Mungu?’ Kufuatilia mambo hayo kunaweza kutufanya tupoteze polepole hali yetu ya kiroho.—Met. 12:11.
4 Kutumia Wakati kwa Hekima: Vyombo vya elektroni huchukua wakati na uangalifu wetu. Kijana mmoja aliyekuwa amejiingiza sana katika michezo ya kompyuta alikiri hivi: “Wakati mwingine nilipocheza kabla ya kwenda katika huduma au katika mkutano wa Kikristo, ilikuwa vigumu kukaza fikira. Nyakati zote nilikuwa nikifikiri jinsi ya kucheza mchezo kwa njia bora zaidi baada ya kufika nyumbani. Funzo langu na usomaji wangu wa Biblia viliathirika. Shangwe yangu ya kumtumikia Mungu ilianza kupungua.” Akitambua kwamba alihitaji kufanya mabadiliko, alifuta michezo yake yote ya kompyuta. Anasema, “Hilo lilikuwa jambo gumu kwelikweli. Nilikuwa nimejiingiza sana katika michezo kuliko nilivyofikiri. Lakini pia nilihisi ushindi mkubwa kwa sababu nilijua kwamba nimefanya jambo hilo kwa faida yangu mwenyewe.”—Mt. 5:29, 30.
5 Huenda ikawa lazima kuchukua hatua hizo ikiwa kuna mambo unayopaswa kufanyia marekebisho. Je, unaweza kununua nusu saa kila siku kutokana na shughuli zisizo za lazima? Huo ndio wakati unaohitaji kila siku ili kuisoma Biblia nzima katika mwaka mmoja. Hilo lingekuwa jambo lenye faida kama nini! (Zab. 19:7-11; 119:97-100) Tenga wakati hususa wa kusoma Biblia, kutayarisha mikutano, na kushiriki katika huduma ya shambani. (1 Kor. 15:58) Kufanya hivyo kutakusaidia kuzuia mambo yanayopoteza wakati na kukuwezesha ‘kuendelea kufahamu yale yaliyo mapenzi ya Yehova.’—Efe. 5:17.
[Maswali ya Funzo]
1. Watu hukabili magumu gani kila mahali leo?
2, 3. Teknolojia ya habari inatokeza magumu gani, na kila mmoja wetu anaweza kujichunguza jinsi gani?
4. Kijana mmoja alifanya mabadiliko gani, na kwa nini?
5. Tunaweza kununuaje wakati ili kufuatia mambo ya kiroho, nasi hufaidikaje kwa kufanya hivyo?