Tunathamini Mapendeleo Yetu!
1 Tangu mwanadamu alipoumbwa, Yehova amewapa watumishi wake mapendeleo mbalimbali. Amewapa mapendeleo licha ya jinsia, umri, au hali yao maishani. (Luka 1:41, 42; Mdo. 7:46; Flp. 1:29) Anatupa mapendeleo gani leo?
2 Baadhi ya Mapendeleo Yetu: Tuna pendeleo la kufundishwa na Yehova. (Mt. 13:11, 15) Kumsifu Yehova kwa maelezo yetu katika mikutano ya kutaniko ni pendeleo lingine tunalothamini. (Zab. 35:18) Tunapopata fursa za kutoa maelezo, tunafanya hivyo kwa uchangamfu. Vivyo hivyo, tukiona kila pendeleo kutanikoni kuwa lenye kuheshimika, tutafanya yote tuwezayo kulitimiza. Je, sisi hutimiza kwa ukawaida pendeleo la kusafisha na kutunza Jumba la Ufalme?
3 Ingawa mamilioni ya watu hujiuliza ikiwa Mungu husikiliza sala zao, tuna pendeleo la kusikilizwa na Aliye Mkuu Zaidi katika ulimwengu wote tunaposali. (Met. 15:29) Yehova mwenyewe husikiliza sala za watumishi wake. (1 Pet. 3:12) Hatuwekei mipaka kuhusu mara ambazo tunaweza kumfikia katika sala. Pendeleo letu la kuweza kusali “kila wakati” ni lenye thamani kama nini!—Efe. 6:18.
4 “Wafanyakazi Wenzi wa Mungu”: Kuhubiri habari njema ya Ufalme wa Mungu tukiwa “wafanyakazi wenzi wa Mungu” ni mojawapo ya mapendeleo bora tuliyo nayo. (1 Kor. 3:9) Hiyo ni kazi yenye kuridhisha na kuburudisha. (Yoh. 4:34) Yehova hahitaji kutumia wanadamu kutimiza kazi hiyo, lakini ametupa mgawo huo kwa sababu anatupenda. (Luka 19:39, 40) Hata hivyo, Yehova hampi mtu yeyote tu pendeleo hilo. Wale wanaoshiriki katika huduma ya hadharani wanapaswa kutimiza na kudumisha matakwa fulani ya kiroho. (Isa. 52:11) Je, sisi huonyesha kwamba tunathamini pendeleo hilo kwa kufanya huduma iwe sehemu muhimu ya ratiba yetu ya kila juma?
5 Mapendeleo kutoka kwa Yehova hufanya maisha yetu yawe yenye kuridhisha. (Met. 10:22) Usikose kamwe kuyathamini! Tunapoonyesha kwamba tunathamini kikweli mapendeleo yetu ya utumishi, tunamfurahisha Baba yetu wa mbinguni, Mpaji wa “kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu.”—Yak. 1:17.