Programu Mpya ya Kusanyiko la Pekee
Kichwa cha programu ya kusanyiko la pekee la mwaka wa utumishi wa 2009 ni “Endelea Kuangalia Huduma . . . , Ili Uitimize,” ambacho kinategemea andiko la Wakolosai 4:17. Tukiwa Wakristo, tunachukua himizo hilo kwa uzito. Lengo letu ni kuitimiza huduma yetu kwa uaminifu kama Yesu alivyofanya. (Yoh. 17:4) Mtume Paulo pia alituwekea mfano mzuri sana katika jambo hilo. Aliazimia kumaliza mwendo wake katika huduma.—Mdo. 20:24.
Hotuba ya mwangalizi wa mzunguko itaonyesha jinsi wahubiri mbalimbali wanavyoshinda matatizo katika huduma yao. Halafu hotuba yenye kichwa, “Wachochee Wale Uliowahubiria Waendelee Kupendezwa” itakazia jinsi tunavyoweza kuwasaidia kikweli wale walio na “mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele.” (Mdo. 13:48) Msemaji anayezuru atazungumzia kwanza andiko la 2 Wakorintho 6:1-10, mstari kwa mstari, katika hotuba yenye kichwa “Jinsi Tunavyojipendekeza Kuwa Wahudumu.” Katika kipindi cha alasiri, atatoa hotuba yenye kichwa “Thamini Sana Huduma Yako.” Bila shaka utatiwa moyo sana na hotuba zifuatazo, “Vijana na Wazee Wanafurahia Huduma” na “Vijana Wanaotimiza Huduma Yao.” Wale wanaotaka kubatizwa kwenye kusanyiko la pekee au kusanyiko la mzunguko ili kuonyesha kwamba wamejiweka wakfu wanapaswa kumjulisha mwangalizi-msimamizi haraka iwezekanavyo. Sehemu muhimu ya makusanyiko yetu yote ni muhtasari wa Mnara wa Mlinzi. Beba nakala yako ambayo tutajifunza katika juma la kusanyiko la pekee.
Tunapoangalia huduma yetu na kuitimiza, tunajitahidi kuhakikisha kwamba mambo mengine hayatuzuii tusitimize kazi tuliyopewa na Yehova. Hotuba za Kimaandiko zenye kutia moyo ambazo zitatolewa katika kusanyiko hili la pekee zinapaswa kutusaidia sote tuelewe yale tunayopaswa kufanya ili tuwe na mtazamo unaofaa na kuichunguza tena huduma yetu ili tuitimize kwa ukamili.