Unaweza Kufundisha!
1. Kila mhubiri wa Ufalme anaweza kuwa na pendeleo gani la pekee?
1 Kumfundisha mtu kweli ni jambo lenye kufurahisha sana katika huduma. Ni jambo la kuthaminiwa unapomwona mtu akiitikia ujumbe wa Ufalme na unapomsaidia kumkaribia Mungu Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu. (Yak. 4:8) Lengo la kila mhubiri wa Ufalme linapaswa kuwa kumfundisha mtu anayetamani kuijua kweli na kumwona akianza kufanya mabadiliko makubwa katika utu, mtazamo, na mwenendo wake.—Mt. 28:19, 20.
2. Kwa nini baadhi ya wahubiri wanasita kuongoza funzo la Biblia, na ni nini kitakachowasaidia kushinda udhaifu huo?
2 Mtegemee Yehova: Baadhi ya watumishi waaminifu wa kale walitilia shaka uwezo wao wa kufanya kazi waliyogawiwa. Kwa kumtegemea Yehova Mungu, watu kama vile Musa, Yeremia, Amosi, na watu wengine wa kawaida, walishinda hisia za kutofaa au kutojiamini, nao walifanikiwa kufanya kazi muhimu. (Kut. 4:10-12; Yer. 1:6, 7; Amo. 7:14, 15) Mtume Paulo pia ‘alijipa ujasiri.’ Jinsi gani? Alisema kwamba ilikuwa “kwa njia ya Mungu wetu.” (1 The. 2:2) Bila shaka, sisi sote tunaweza kuwa na hakika kwamba Yehova atatusaidia na kutupa hekima na nguvu tunazohitaji ili kuongoza mafunzo ya Biblia yenye maendeleo.—Isa. 41:10; 1 Kor. 1:26, 27; 1 Pet. 4:11.
3, 4. Kuna mpango gani wa kutuzoeza kuwafundisha watu Neno la Mungu?
3 Kubali Kuzoezwa: Ili tuwe walimu stadi, Mfundishaji wetu Mkuu, Yehova Mungu, anatuzoeza kwa ukawaida kupitia mpango wa elimu ya kiroho. (Isa. 54:13; 2 Tim. 3:16, 17) Unakubali mazoezi haya kwa kutumia vizuri kila fursa uliyo nayo kuongeza ujuzi wako wa Biblia na kufanya maendeleo katika ustadi wako wa kuwafundisha watu kweli za Biblia. Ijapokuwa Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na Mkutano wa Utumishi umekusudiwa hasa kutuzoeza kuwafundisha watu Neno la Mungu, katika mikutano mingine pia tunazoezwa kufanya kazi hiyo.
4 Jitahidi kujifunza njia rahisi za kueleza mambo magumu ya kiroho. Kitabu Shule ya Huduma, ukurasa wa 227, kinasema hivi: “Ni lazima uelewe vizuri jambo unalozungumzia ikiwa utawasaidia wengine walielewe.” Kutoa maelezo katika mikutano hutusaidia kukumbuka mambo makuu ili tuyatumie baadaye. Kwa hiyo, jitayarishe vizuri nawe utakuwa na hakika zaidi kuhusu ustadi wako wa kufundisha.
5. Tunazoezwa kwa njia gani nyingine kutanikoni ili kuboresha uwezo wetu wa kufundisha?
5 Wahudumu Wakristo wanapoanza kazi ya kufanya wanafunzi, wao hujifunza mambo mengi kutoka kwa mmoja na mwenzake. (Luka 10:1) Ikiwezekana, wakati wa kuongoza mafunzo ya Biblia, andamana na wahubiri stadi kama vile mapainia, wazee Wakristo, na waangalizi wanaosafiri. Zingatia jinsi wanavyotumia mifano rahisi, picha, na mambo mengine yanayopatikana katika vitabu vyetu vya kujifunzia Biblia, ili kueleza kweli za Maandiko. Waombe mapendekezo kuhusu jinsi ambavyo unaweza kuboresha uwezo wako wa kufundisha. (Met. 1:5; 27:17) Ni vizuri kuthamini mazoezi haya kutoka kwa ndugu na dada kwa sababu ni maandalizi kutoka kwa Mungu.—2 Kor. 3:5.
6. Mtu anapaswa kufanya nini hasa ili awe mwalimu wa Neno la Mungu?
6 Mtegemee Yehova na unufaike na mazoezi ambayo anaandaa. Mwombe akusaidie kufanya maendeleo. (Zab. 25:4, 5) Wewe pia unaweza kupata shangwe ya kumsaidia mtu mwingine kuwa mwalimu wa Neno la Mungu kama wewe!