Yehova Anatuzoeza kwa Ajili ya Kazi Hii
1. Yehova anapowapa wanadamu mgawo, yeye hufanya nini pia?
1 Yehova anapowapa wanadamu mgawo fulani, yeye huwapa pia msaada wanaohitaji ili kuutimiza. Kwa mfano, Yehova alipomwambia Noa afanye jambo ambalo hakuwa amewahi kufanya, yaani kujenga safina, alimwambia pia jinsi ya kuijenga. (Mwa. 6:14-16) Alipompa mchungaji mpole Musa mgawo wa kuwaendea wanaume wazee wa Israeli na vilevile Farao, Yehova alimhakikishia hivi: “Nitakuwa pamoja na kinywa chako nami nitakufundisha unayopaswa kusema.” (Kut. 4:12) Vivyo hivyo, Yehova pia ametufundisha jinsi ya kufanya kazi ya kuhubiri habari njema. Anatuzoeza kwa ajili ya kazi hii kupitia Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na Mkutano wa Utumishi. Tunaweza kufanya nini ili tufaidike na mazoezi hayo?
2. Tunaweza kufanya nini ili tufaidike na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi?
2 Shule ya Huduma ya Kitheokrasi: Jifunze na utayarishe kila sehemu iliyoratibiwa kabla ya kuhudhuria kila mkutano wa shule. Kisha, unapoona jinsi wanafunzi wanavyotumia habari hizo katika hotuba zao, utaboresha njia yako ya kufundisha. (Met. 27:17) Beba kitabu chako cha Shule ya Huduma. Mwangalizi wa shule anapokirejelea, fuatana naye. Tia alama mambo muhimu ambayo ungependa kutumia na utumie nafasi zilizo pambizoni kuandika maandishi ya binafsi. Hata hivyo, njia bora zaidi ya kufaidika na shule hii ni kwa kushiriki. Je, umejiandikisha? Unapopokea karatasi ya mgawo, tayarisha vizuri na utumie mashauri unayopewa. Unapokuwa katika huduma, tumia mambo ambayo umejifunza.
3. Ni nini kitakachotusaidia tufaidike na Mkutano wa Utumishi?
3 Mkutano wa Utumishi: Tutakumbuka zaidi mapendekezo tunayopata katika mkutano huu ikiwa tutajifunza habari mapema na kujitayarisha kushiriki. Tukitoa maelezo mafupi, wengi watapata nafasi ya kushiriki. Kazia uangalifu maonyesho, na utumie mapendekezo yoyote ambayo unaona yatakusaidia kuwa na matokeo zaidi katika huduma. Tunza makala za Huduma Yetu ya Ufalme ambazo unaona zitakusaidia katika utumishi wako.
4. Kwa nini tunapaswa kutumia mambo ya kitheokrasi tunayojifunza?
4 Kama migawo waliyopewa Noa na Musa, kazi yetu ya kuhubiri habari njema katika dunia yote inayokaliwa si rahisi. (Mt. 24:14) Tunaweza kufanikiwa iwapo tutamtegemea Yehova, Mfundishaji wetu Mkuu, na kutumia mambo anayotufundisha.—Isa. 30:20.