Jinsi Shule ya Huduma ya Kitheokrasi Inavyotunufaisha
1 Watu wa Yehova wana pendeleo la pekee la kufundishwa naye. (Isa. 54:13; Yoh. 6:45) Hata hivyo, tunahitaji hasa kuwa wenye bidii ili kunufaika na mafundisho hayo. Je, unaweza kutambua jinsi Shule ya Huduma ya Kitheokrasi inavyokunufaisha kiroho?
2 Maelezo Yanayofaa: Waangalizi wengi wa shule wamesema kwamba kujifunza kwa makini sifa za usemi kumesaidia makutaniko yao katika huduma ya shambani. Isitoshe, mwangalizi mmoja wa shule alisema kwamba mpango wa kuwashirikisha wasikilizaji kutoa maelezo kuhusu mambo makuu ya usomaji wa Biblia, umefanya wengi waanze kufuata ratiba ya usomaji wa Biblia. Kuhusu Hotuba Na. 2, ndugu wengi wanasema kwamba kuna manufaa ya kuzingatia habari wanayosoma tu bila kutayarisha utangulizi na umalizio. Sasa wale wanaopewa hotuba hiyo huzingatia zaidi kuboresha usomaji wao.—1 Tim. 4:13.
3 Wote Wanaweza Kunufaika: Kutoa maelezo kwenye mikutano kunaweza kuwa jambo lenye kufurahisha. (Met. 15:23) Kupata pitio la maswali na majibu mapema hutuwezesha kujitayarisha na kutoa maelezo bila shida. Isitoshe, kuanzia toleo la Januari 1, 2004, mara kwa mara gazeti la Mnara wa Mlinzi limekuwa na makala zinazozungumzia mambo makuu kutoka katika vitabu vya Biblia, ambazo zinalingana na usomaji wetu wa Biblia katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Makala hizo zimewasaidia wengi kutoa maelezo yenye kujenga wakati wa kuzungumzia mambo makuu katika Biblia.
4 Yeyote aliyejiandikisha katika shule hiyo ana pendeleo la pekee la kutayarisha na kutoa hotuba. Sote tunaweza kunufaika na maelezo yenye kujenga ya mwangalizi wa shule. Wanafunzi wanaweza kunufaika zaidi kutokana na ushauri ambao huenda mwangalizi huyo akatolea kila mmoja wao baada ya mkutano. Mazoezi kuhusu sifa za usemi yanayopatikana mwishoni mwa kila sura ya kitabu, Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, yanatusaidia pia.
5 Wakati wa shule na baada ya shule, unaweza kuelezwa mambo fulani ya Kimaandiko, yanayofaa. Yaandike mambo hayo kwenye nakala yako ya kitabu Shule ya Huduma. Tafakari mambo ambayo umejifunza, na ufikirie jinsi kufundishwa na Mungu kunavyokujenga kiroho.