Shule Inayotuzoeza Kufanya Kazi Muhimu Zaidi Maishani
1 Watu huenda shuleni kupata elimu ambayo itawasaidia kufikia miradi yao maishani. Hata hivyo, ni mradi upi unaoweza kuwa muhimu kuliko kumsifu Mpaji wa uhai na kuwasaidia wengine wajifunze makusudi yake na njia zake? Hakuna. Kusudi la Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ni kutuzoeza ili tuwafundishe wengine imani yetu. Kwa hiyo, tunapohudhuria shule hiyo kila juma, tunazoezwa kutimiza kazi muhimu zaidi maishani.
2 “Ratiba ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ya 2003” ilitiwa ndani ya Huduma Yetu ya Ufalme ya mwezi uliopita. Ratiba hiyo ina maelezo kamili kuhusu utaratibu wa kuongoza shule. Ingefaa kuweka ratiba hiyo ndani ya kitabu chako cha Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Unapaswa kuja na kitabu hicho kila juma kwenye Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. Hebu angalia baadhi ya mambo yatakayokuwa katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi mwaka wa 2003.
3 Sifa ya Usemi: Kuanzia mwezi wa Januari, Shule ya Huduma ya Kitheokrasi ya kila juma itaanza na hotuba ya dakika tano itakayozungumzia sifa moja ya usemi au habari fulani kuhusu kusoma, kujifunza, au kufundisha. Mwangalizi wa shule atatoa hotuba hii, au anaweza kumpa mzee mwingine anayestahili. Msemaji anaweza kufafanua sifa ya usemi na kueleza umuhimu wake. Kisha anapaswa kuzungumzia sifa hiyo zaidi kwa kutaja mifano ya Kimaandiko na kueleza jinsi ya kutumia sifa hiyo, akikazia hasa jinsi kutumia sifa hiyo kunavyoweza kuboresha huduma yetu ya shambani.
4 Hotuba Na. 1: Ndugu wanaopewa mgawo wa kutoa hotuba ya maagizo wanashauriwa tena waonyeshe “jinsi habari hiyo inavyoweza kutumiwa maishani.” Hilo lamaanisha kwamba wanapaswa kuonyesha kutaniko jinsi linavyoweza kutumia habari hiyo. Ukipokea mgawo huu, soma ukurasa wa 48-49 wa kitabu cha Shule ya Huduma ili upate madokezo ya kukusaidia kutayarisha. Chunguza pia kurasa nyinginezo zilizotajwa chini ya kichwa “Matumizi ya habari” kwenye faharisi.
5 Ratiba ya Usomaji wa Biblia: Ikiwa wakati uliopita hukuweza kusoma Biblia kila juma kulingana na ratiba ya shule, mbona usiazimie kufuata ratiba hiyo mwaka huu? Wale wanaofuata ratiba hiyo watamaliza kusoma Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo kufikia mwisho wa mwaka. Faida za kuanza programu ya kusoma Biblia kwa kusoma kwanza Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo zimetajwa katika fungu la 4, kwenye ukurasa wa 10 wa kitabu cha Shule ya Huduma.
6 Mambo Makuu ya Usomaji wa Biblia: Muda wa sehemu hii umeongezwa hadi dakika 10 ili wasikilizaji waweze kutoa maelezo kuhusu usomaji wa Biblia wa juma hilo. Wale waliopewa mgawo huu wasipite wakati. Sehemu hii itafanywa kila juma, kutia ndani juma la pitio la maswali na majibu. Unaposoma sura zilizoratibiwa, tafuta mambo ambayo yatakusaidia katika funzo lenu la familia, katika huduma yako, au maishani mwako. Ni sifa zipi za Yehova zinazodhihirishwa na jinsi alivyoshughulika na mtu mmoja-mmoja na mataifa? Umejifunza jambo gani ambalo limeimarisha imani yako na kukufanya umthamini Yehova zaidi? Unaweza kutoa maelezo yoyote kuhusiana na sura zilizoratibiwa, hata kutoka kwa mistari itakayosomwa na mwanafunzi wa Hotuba Na. 2, kwa kuwa ndugu huyo atasoma tu bila kufafanua mistari hiyo.
7 Hotuba Na. 2: Kila juma mwanafunzi wa kwanza atapewa mgawo wa kujizoeza kusoma mbele ya watu. Sehemu zote zitasomwa kutokana na usomaji wa Biblia wa kila juma isipokuwa usomaji wa juma la mwisho kila mwezi. Usomaji wa juma la mwisho utatoka kwa Mnara wa Mlinzi. Mwanafunzi anapaswa kusoma habari aliyogawiwa bila kutoa utangulizi wala maneno ya kumalizia. Kwa kufanya hivyo, anaweza kukazia fikira ustadi wake wa kusoma.—1 Tim. 4:13.
8 Hotuba Na. 3 na Na. 4: Baadhi ya hotuba hizi zina habari nyingi kutoka kwenye kitabu Kutoa Sababu; nyingine zina kichwa peke yake. Wale watakaopewa hotuba zenye habari chache au kichwa peke yake wanapaswa kutayarisha hotuba zao kwa kufanya utafiti katika vichapo vyetu vya Kikristo. Hivyo akina dada wataweza kutayarisha hotuba ambayo wasaidizi wao wataelewa.
9 Vikao: Kama inavyotajwa kwenye ukurasa wa 45 wa kitabu cha Shule ya Huduma, mwangalizi wa shule anaweza kukupa kikao. Dada wasipopewa kikao, wanaweza kuchagua kikao kimoja katika orodha iliyo kwenye ukurasa wa 82. Ikiwa dada anatoa hotuba moja baada ya kila miezi miwili, atatumia vikao vyote 30 baada ya muda wa miaka mitano. Dada wanaochagua Na. 30, yaani, “Kikao kingine kinachofaa eneo lenu,” wanapaswa kuandika kikao chao upande wa chini wa ukurasa wa mbele wa kikaratasi cha mgawo (S-89) au upande wa nyuma wa kikaratasi hicho. Mwangalizi wa shule ataandika tarehe ambayo mwanafunzi ametoa hotuba kando ya kikao alichotumia kwenye ukurasa wa 82 wa kitabu chake. Anaweza kufanya hivyo anapojaza fomu ya mashauri ya mwanafunzi.
10 Fomu ya Mashauri: Fomu yako ya mashauri iko ndani ya kitabu chako kwenye ukurasa wa 79-81. Kwa hiyo, utampa mwangalizi wa shule kitabu chako kila mara baada ya kutoa hotuba. Mwangalizi wa shule atahitaji kujiandikia rekodi ya mashauri ambayo mwanafunzi anafanyia kazi.
11 Pitio la Maswali na Majibu: Pitio la Shule ya Huduma ya Kitheokrasi litafanywa kwa maswali na majibu. Litafanywa kwa muda wa dakika 30 baada ya kila miezi miwili. Maswali ya pitio bado yatakuwa yakichapishwa kwenye Huduma Yetu ya Ufalme. Ikiwa juma la pitio la maswali na majibu linaangukia kusanyiko la mzunguko au ziara ya mwangalizi wa mzunguko, basi hotuba za juma linalofuata zitatolewa juma hilo na pitio litafanywa baada ya kusanyiko la mzunguko au ziara ya mwangalizi wa mzunguko.
12 Shule za Ziada: Katika makutaniko yenye wanafunzi zaidi ya 50 katika shule, wazee wanaweza kufikiria kuwa na shule za ziada. “Shule ya ziada inaweza kuwa na hotuba zote za wanafunzi au hotuba mbili tu za mwisho.” (Shule ya Huduma, uku. 285) Dokezo hilo la mwisho limetolewa ili kuyasaidia makutaniko ambayo yana akina dada wengi na ndugu wachache tu wa kufanya mgawo wa kusoma. Wazee wanapaswa kuteua ndugu wanaostahili ili waongoze shule hizo.
13 Mshauri Msaidizi: Kama ratiba ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi inavyosema, baraza la wazee linapaswa kumteua mshauri msaidizi ili awashauri faraghani wazee na watumishi wa huduma wanaoshughulikia mambo makuu ya usomaji wa Biblia na hotuba za maagizo. Mgawo huu unapaswa kupewa ndugu mwenye uzoefu ambaye shauri lake litaheshimiwa na wazee wengine. Anapaswa kutoa mashauri yenye kujenga, na kuwapongeza wasemaji wanaoongea na kufundisha kwa ustadi na kuwapa dokezo moja au mawili ya kufanyia kazi. Hakuna haja ya kumshauri kila mara ndugu ambaye hutoa hotuba mara nyingi. Hata hivyo, ndugu aliyepewa jukumu la kutoa mashauri anapaswa kufahamu kwamba hata akina ndugu ambao sasa wanatoa hotuba za watu wote wanaweza kusaidiwa kufanya maendeleo zaidi.—1 Tim. 4:15.
14 Mambo Ambayo Mshauri Anapaswa Kuangalia: Ni nini kinachoweza kumsaidia mshauri kuchanganua hotuba? Sanduku la tatu katika sura nyingi kati ya zile sura 53 za kitabu cha Shule ya Huduma lina muhtasari wa mambo ambayo mshauri anapaswa kuangalia. Mwangalizi wa shule anapaswa pia kuangalia hoja nyingine au madokezo yaliyo katika kitabu hicho ambayo yatamsaidia kuchanganua haraka jinsi hotuba inavyotiririka na jinsi inavyotolewa. Kwa mfano, tazama maswali yaliyo mwanzoni mwa ukurasa wa 55 na hoja zilizo katika fungu la mwisho kwenye ukurasa wa 163.
15 Jaza Nafasi Zilizo Tupu: Kitabu cha Shule ya Huduma kina nafasi pana pambizoni na nafasi nyingi tupu ambamo unaweza kuandika mambo fulani wakati wa funzo lako la binafsi na unapohudhuria Shule ya Huduma ya Kitheokrasi. (Ona ukurasa wa 77, 92, 165, 243, 246, na 250.) Hakikisha kwamba unabeba kitabu chako kila juma. Ambatana na msemaji anapotoa hotuba ya kwanza. Acha kitabu chako wazi wakati wa shule. Sikiliza madokezo yanayotolewa na mwangalizi wa shule. Uwe makini kuhusu mbinu za ufundishaji zinazotumiwa, maswali yanayoulizwa, mifano, tamathali za usemi, vielezi, vielelezo, na kuona jinsi wasemaji wanavyopambanua mambo. Kuandika mambo muhimu kutakusaidia kukumbuka na kutumia mambo mengi mazuri unayojifunza shuleni.
16 Yesu Kristo alijua kwamba kuhubiri habari njema za Ufalme wa Mungu ndilo pendeleo kubwa zaidi ambalo mtu anaweza kupewa. Alitumwa kwa kusudi hilo. (Marko 1:38) Alisema hivi: “Ni lazima nitangaze habari njema ya Ufalme wa Mungu, kwa sababu kwa ajili ya hili nilitumwa.” (Luka 4:43) Sisi pia tunahubiri habari njema kwa bidii kwa sababu tumekubali mwaliko wa kumfuata Yesu, na tunajitahidi daima kuboresha ‘dhabihu yetu ya sifa.’ (Ebr. 13:15) Ili kufikia mradi huo, na tuazimie kushiriki kwa ukawaida katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, shule ambayo itatuzoeza kufanya kazi muhimu zaidi maishani.