Vichwa vya Familia—Dumisheni Ratiba Nzuri ya Kiroho
1 Licha ya kuishi kwa miaka mingi katika jiji la Babiloni lililojaa ibada ya sanamu na ufisadi, Danieli alijulikana kwa kumtumikia Yehova “daima.” (Dan. 6:16, 20) Alidumishaje hali nzuri ya kiroho? Masimulizi ya Biblia yaonyesha kwamba alikuwa na ratiba nzuri ya kufanya mambo yaliyohusiana na ibada ya kweli. Kwa mfano, alikuwa na desturi ya kusali mara tatu kwa siku akiwa katika chumba chake cha juu. (Dan. 6:10) Bila shaka, alikuwa pia amesitawisha utaratibu wa kufanya mambo mengine ya kiroho, kama vile kusoma Sheria. Hivyo, alipokabiliwa na jaribu lililohatarisha uhai wake, Danieli hakuyumbayumba katika ujitoaji wake kwa Yehova, naye akakombolewa kimuujiza.—Dan. 6:4-22.
2 Vivyo hivyo leo, lazima ‘tufulize kuwa macho kwa udumifu wote.’ (Efe. 6:18) Tunaishi katika ulimwengu ambao “unakaa katika nguvu ya mwovu.” (1 Yoh. 5:19) Upinzani au majaribu yanaweza kutupata ghafula na kujaribu imani yetu. Wakati wa dhiki kubwa, watumishi wa Mungu watakuwa shabaha kubwa ya shambulizi la Gogu wa Magogu, na itaonekana kana kwamba hawawezi kuponyoka. Hiyo itahitaji tumtumaini Yehova kabisa.—Eze. 38:14-16.
3 ‘Jambo moja muhimu ni kufanya kusoma, kujifunza, na kuzungumzia Biblia vizuri mkiwa familia kuwe sehemu ya maisha yenu.’ Ndivyo ulivyosema utangulizi wa drama ya kusanyiko la wilaya la 1998 yenye kichwa “Familia—Fanyeni Usomaji wa Biblia Kila Siku Uwe Njia Yenu ya Maisha!” Utangulizi huo uliendelea kusema: ‘Familia zifuatapo programu kwa ukawaida na kwa namna ambayo hufanya Biblia ichangamshe, kawaida hii ya kutegemea Biblia yaweza kusaidia sana familia. Hiyo huongeza ujuzi wetu. Huimarisha imani yetu. Nayo hutuandalia mifano ya kuigwa, yaani, wanaume na wanawake wa nyakati za kale, ambao wanaweza kutuchochea, kutusukuma tushikilie kweli.’ Tunapochunguza sehemu mbalimbali za ratiba nzuri ya kiroho, vichwa vya familia watafute njia moja au mbili za kuboresha programu ya kiroho ya familia yao.
4 Chunguzeni Neno la Mungu Kila Siku: “Ufalme wa Mungu utawalapo bila kupingwa na mapenzi yake kufanywa duniani kama yafanywavyo mbinguni, hakuna wanadamu wakatili—wala hata wanyama—‘watakaodhuru wala kuharibu.’ (Isa. 11:9; Mt. 6:9, 10)” Hayo yalikuwa maelezo ya Septemba 11 katika kijitabu Kuyachunguza Maandiko Kila Siku—2001. Kikumbusha hicho kilifariji kama nini! Ukiwa kichwa cha familia, je, ni kawaida yako kuchunguza andiko la Biblia na maelezo yake pamoja na familia yako? Jambo hilo linanufaisha sana. Ikiwa haiwezekani kufanya hivyo asubuhi, labda mnaweza kufanya hivyo baadaye siku hiyo. Baba mmoja alisema hivi: “Mlo wa jioni umekuwa wakati mzuri kwetu sisi kuzungumzia andiko la Biblia la kila siku.”
5 Ikiwa tayari mna ratiba nzuri ya kuzungumzia andiko la kila siku mkiwa familia, mnapongezwa. Labda mnaweza kunufaika zaidi kwa kusoma sehemu fulani ya Biblia wakati huo. Wengine wamezoea kusoma sura nzima inayohusu andiko la siku. Wengine nao hufuata utaratibu wa kusoma hatua kwa hatua kitabu kimoja cha Biblia. Kusoma Biblia kila siku kutasaidia familia isitawishe hofu inayofaa ya kutompendeza Yehova na kutachochea tamaa yao ya kufanya mapenzi yake.—Kum. 17:18-20.
6 Programu ya familia yenu ya usomaji wa Biblia na kuchunguza andiko la kila siku itawanufaisha hata zaidi kama mnaweza kutumia dakika chache kuzungumzia jinsi mnavyoweza kutumia habari hizo maishani. Kitabu Shule ya Huduma kinatoa dokezo hili kwenye ukurasa wa 60: “Unaweza kuchagua maandiko machache ya usomaji wa Biblia ambayo yameratibiwa juma hilo, uzungumzie maana yake, kisha uulize maswali kama haya: ‘Kanuni hii inatupatia mwongozo gani? Tunaweza kutumiaje maandiko haya katika huduma? Yanafunua nini kuhusu jinsi Yehova anavyofanya mambo, na hilo linajengaje uthamini wetu kwake?’” Mazungumzo hayo ya kiroho yatawasaidia wote katika nyumba yako ‘kuendelea kufahamu mapenzi ya Yehova ni nini.’—Efe. 5:17.
7 Funzo la Familia: Kuongoza funzo la familia kwa ukawaida kila juma ni njia nzuri ya kuonyesha watoto kwamba mambo ya kiroho yanapaswa kutangulizwa. Mwanamume mmoja kijana akumbuka hivi: ‘Nyakati nyingine baba angekuwa amechoka sana alipotoka kazini hivi kwamba hangejizuia kusinzia. Hata hivyo funzo lilifanywa, na jambo hilo lilitusaidia tuthamini uzito wake.’ Watoto pia wanaweza kufanya mpango huo ufanikiwe. Familia moja yenye watoto tisa waliamka saa kumi na moja asubuhi ili wawe na funzo lao la familia kwa sababu hawangeweza kufanya hivyo wakati mwingine wowote.
8 Ili funzo la familia lifanikiwe, lazima vichwa vya familia ‘wakaze uangalifu kwa kufundisha kwao.’ (1 Tim. 4:16) Kitabu Shule ya Huduma kinasema hivi kwenye ukurasa wa 31 na 32: “Kwa kweli inaweza kusemwa kwamba kuchunguza kwa makini hali ya familia yako ndiyo njia ya kwanza ya kuwa na funzo zuri la familia. Familia yako inaendeleaje kiroho? . . . Mkiwa katika huduma ya shambani pamoja na watoto wako, je, wanajitambulisha kwa urahisi kwa vijana wenzao kwamba wao ni Mashahidi wa Yehova? Je, wanafurahia usomaji wa Biblia na funzo lenu la familia? Je, kweli wanafuata njia ya Yehova maishani mwao? Ukiwa mzazi, uchunguzi wa makini utakuonyesha kile ambacho unahitaji kufanya ili kutia sifa za kiroho katika kila mmoja wa familia yako na kuzikuza.”
9 Mikutano ya Kutaniko: Kutayarisha na kuhudhuria mikutano ya kutaniko kwapaswa kuwe sehemu ya maana ya ratiba yenu ya kila juma. (Ebr. 10:24, 25) Nyakati nyingine, mnaweza kutayarisha baadhi ya mikutano mkiwa familia. Badala ya kungoja hadi dakika ya mwisho, je, mwaweza kupanga kujitayarisha mapema? Ratiba nzuri itafanya utayarishe vizuri na kufaidika sana na mikutano.—Mit. 21:5.
10 Ubora na ukawaida ndizo sifa zinazofanya ratiba ya kiroho iwe yenye matokeo. Vipi hali zikifanya iwe vigumu kwako kutayarisha mikutano yote? Kitabu Shule ya Huduma kinadokeza hivi kwenye ukurasa wa 31: “Epuka mtego wa kusoma habari mbio-mbio mradi tu umesoma, au vibaya zaidi, kutosoma chochote kabisa eti kwa sababu huwezi kutayarisha mambo yote. Badala yake, angalia kiasi ambacho unaweza kujifunza, na ujifunze vizuri. Fanya hivyo kila juma. Baada ya muda, jaribu kufanya hivyo na mikutano mingine.”
11 Familia zifikapo mapema mikutanoni, hiyo huwasaidia kutayarisha akili zao ili wamsifu Yehova na kufaidika na mafundisho yake. Je, familia yako imezoea kufanya hivyo? Kila mmoja katika familia anahitaji kuwa na mpango mzuri na mwenye ushirikiano. Ikiwa mara nyingi familia yako huharakisha na huwa na mkazo wakati wa kwenda mikutanoni, je, mwaweza kurekebisha ratiba yenu? Je, kuna mambo ambayo mnaweza kuyashughulikia mapema? Ikiwa mmoja amelemewa na kazi nyingi, je, wengine wanaweza kumsaidia? Je, mkazo ungepungua ikiwa kila mtu angejitayarisha mapema kidogo kwa ajili ya mkutano? Utaratibu mzuri hufanya kuwe na amani katika familia na katika kutaniko.—1 Kor. 14:33, 40.
12 Utumishi wa Shambani: Kupanga saa za kwenda katika huduma ni sehemu nyingine ya kuwa na ratiba nzuri ya kiroho. Mwanamume kijana anayeitwa Jayson akumbuka hivi: “Familia yetu ilishiriki utumishi wa shambani kila Jumamosi asubuhi. Jambo hilo lilinisaidia kwa kuwa kadiri nilivyoshiriki katika huduma, ndivyo nilivyozidi kuona manufaa yake na kuifurahia zaidi.” Watu wengi waliolelewa katika familia za Mashahidi wana maoni yaleyale kwamba kuwa na wakati hususa wa kushiriki katika huduma kila juma kuliwasaidia wafanye maendeleo wakiwa wahudumu Wakristo.
13 Ratiba nzuri pia yaweza kusaidia kufanya wakati ambao familia yenu inatumia katika utumishi wa shambani ufurahishe na uwe wenye matokeo. Hilo laweza kufanywaje? Gazeti la Mnara wa Mlinzi la Julai 1, 1999 lilidokeza hivi kwenye ukurasa wa 21: “Je, wewe mara kwa mara hutumia wakati wa funzo la familia ili kusaidia washiriki wa jamaa yako wajitayarishe kwa ajili ya utumishi wa shambani? Kufanya hivyo kwaweza kuwa na manufaa [kubwa]. (2 Timotheo 2:15) Kwaweza kusaidia kufanya utumishi wao uwe wenye maana na wenye matokeo. Mara kwa mara, huenda ukatenga kipindi chote cha funzo kwa ajili ya kujitayarisha huko. Huenda ukashughulikia mara nyingi zaidi sehemu za huduma ya shambani katika mazungumzo mafupi-mafupi mwishoni mwa kila funzo la familia au wakati mwingineo katika juma.” Je, familia yako imejaribu kufanya hivyo?
14 Endeleeni Kufanya Maendeleo: Kulingana na mambo ambayo tumechunguza, je, umeona sehemu ambazo familia yako inafanya vizuri? Wapongeze, na ujitahidi kuboresha sehemu hizo. Ukiona sehemu kadhaa zinazohitaji kuboreshwa, fanyia kazi sehemu moja au mbili kwanza. Zinapokuwa sehemu ya ratiba yenu ya kiroho, endelea kufanyia kazi sehemu nyingine moja au zaidi. Uwe na mtazamo mzuri na kiasi. (Flp. 4:4, 5) Kuwekea familia yako ratiba nzuri ya kiroho huhitaji jitihada nyingi, lakini kuna manufaa, kwa kuwa Yehova anatuhakikishia hivi: “Yeyote anayedumu katika njia yangu huyo ndiye mimi nitakayemwokoa.”—Zab. 50:23, Biblia Habari Njema.