Msaada kwa Familia
1. Familia za Waisraeli zilinufaikaje kutokana na Sabato ya kila juma?
1 Maadhimisho ya Sabato yalikuwa maandalizi yenye upendo kutoka kwa Yehova, ambayo yalizinufaisha familia. Waisraeli walipumzika kutokana na kazi zao za kawaida na wakawa na wakati wa kutafakari juu ya uzuri wa Yehova na uhusiano wao pamoja naye. Wazazi wangeweza kutumia fursa hiyo kukazia Sheria katika mioyo ya watoto wao. (Kum. 6:6, 7) Sabato iliwapa nafasi watu wa Yehova kuzingatia hali yao ya kiroho kila juma.
2. Sabato inatufunza nini kumhusu Yehova?
2 Yehova haamuru familia zishike Sabato leo. Hata hivyo, sheria hiyo inatufunza jambo fulani kumhusu Mungu wetu. Sikuzote anapendezwa na hali njema ya kiroho ya watu wake. (Isa. 48:17, 18) Leo, njia moja ambayo Yehova anaonyesha kwamba anapendezwa na hali yetu ya kiroho ni kupitia jioni ya Ibada ya Familia.
3. Kusudi la jioni ya Ibada ya Familia ni nini?
3 Kusudi la Jioni ya Ibada ya Familia Ni Nini? Tangu Januari 2009, Funzo la Kitabu la Kutaniko lilianza kufanywa wakati mmoja na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na Mkutano wa Utumishi. Sababu moja ya badiliko hilo ilikuwa kuzisaidia familia kupata nafasi ya kuimarisha uhusiano wao pamoja na Yehova kwa kupanga jioni hususa kila juma kwa ajili ya ibada ya familia. Kila familia ilitiwa moyo, ikiwezekana, ifanye funzo lao la familia jioni iliyotumiwa hapo awali kwa ajili ya funzo la kitabu, nao watumie wakati huo kuwa na mazungumzo ya Biblia yasiyo ya haraka na funzo linalokusudiwa kushughulikia mahitaji ya familia.
4. Je, ni lazima familia itumie saa moja tu katika mazungumzo yao? Eleza.
4 Ili kuhudhuria Funzo la Kitabu la Kutaniko, tulihitaji wakati wa kuvaa, kusafiri, na kadhalika. Kwa wengi wetu, ili kuhudhuria mkutano huo wa saa moja, tulihitaji kutumia muda mwingi. Tukiwa na badiliko hilo katika ratiba yetu ya mikutano, sasa tunatumia jioni hiyo kumwabudu Yehova tukiwa familia. Kwa hiyo, si lazima tutumie saa moja tu katika jioni ya Ibada ya Familia. Badala yake, tunapaswa kufikiria mahitaji na uwezo wa familia zetu na kuweka wakati kulingana na hali.
5. Je, ni lazima familia iwe pamoja muda wote wa funzo? Eleza.
5 Je, Ni Lazima Familia Iwe Pamoja Muda Wote wa Funzo? Wenzi wa ndoa pamoja na familia zenye watoto zinapozungumzia habari za Kimaandiko zikiwa pamoja, zinatiana moyo. (Rom. 1:12) Familia inakuwa na uhusiano wa karibu. Hivyo, jioni ya Ibada ya Familia inapaswa kuzingatia hasa mazungumzo ya Kimaandiko. Hata hivyo, kila mshiriki wa familia anaweza pia kutumia wakati fulani kufanya funzo la kibinafsi. Kwa mfano, baada ya mazungumzo pamoja na familia nzima, familia inaweza kubaki pamoja huku kila mmoja akiendelea kujifunza kivyake, labda kumalizia matayarisho yake kwa ajili ya mikutano au kusoma magazeti yetu. Familia fulani huamua kutotazama televisheni hata kidogo jioni hiyo.
6. Mazungumzo yanaweza kuongozwa jinsi gani?
6 Mazungumzo Hayo Yanaweza Kuongozwa Jinsi Gani? Si lazima sikuzote yawe mazungumzo ya maswali na majibu. Ili kufanya jioni ya Ibada ya Familia iwe yenye kuchangamsha na kupendeza, familia nyingi zina programu inayofanana na ya mikutano yetu ya katikati ya juma. Wao hugawanya mazungumzo yao kwa sehemu kadhaa na kuzishughulikia kwa njia mbalimbali. Kwa mfano, wanaweza kusoma Biblia pamoja, kutayarisha sehemu fulani ya mikutano, na kufanya mazoezi kwa ajili ya huduma. Ukurasa wa 6 una mapendekezo kadhaa.
7. Wazazi wanapaswa kuzingatia hali gani?
7 Wazazi Wanapaswa Kuzingatia Hali Gani? Familia yako itajifunza vizuri zaidi kukiwa na upendo na hali zenye kustarehesha. Nyakati nyingine mnaweza kujifunzia nje ikiwa hali ya hewa inaruhusu. Jihisi huru kupumzika kidogo ikihitajiwa. Familia fulani huwa na viburudisho baada ya funzo lao. Ingawa wazazi wataepuka kutumia jioni ya Ibada ya Familia kuwagombeza au kuwaadhibu watoto, huenda wakahitaji kutumia wakati fulani kuzungumzia mwelekeo au tatizo fulani ambalo wametambua. Hata hivyo, huenda ikafaa zaidi kuzungumza na mtoto mambo ya kibinafsi faraghani wakati mwingine katika juma hilo, ili kuepuka kumwaibisha mbele ya ndugu na dada zake. Jioni ya Ibada ya Familia haipaswi kuwa wakati wenye kuchosha au usiovutia bali unapaswa kuwa wakati wenye furaha kwa sababu tunamwabudu Mungu mwenye furaha.—1 Tim. 1:11.
8, 9. Vichwa vya familia wanapaswa kufanya matayarisho gani?
8 Kichwa cha Familia Anaweza Kufanya Matayarisho Gani? Familia itanufaika zaidi ikiwa kichwa cha familia atafanya mipango mapema kwa ajili ya kila jioni ya Ibada ya Familia kwa kuamua mambo watakayozungumzia na jinsi watakavyoyashughulikia. (Met. 21:5) Ni vizuri mume ashauriane na mke wake kuhusu mambo hayo. (Met. 15:22) Vichwa vya familia, kwa nini mara kwa mara msiwaulize watoto wenu maoni yao pia? Mkifanya hivyo, mtaelewa zaidi mambo yanayowapendeza na yanayowahangaisha.
9 Mara nyingi kichwa cha familia hatahitaji kutumia muda mwingi sana akifanya matayarisho. Yaelekea familia itafurahia kuwa na jambo fulani hususa kila juma, naye kichwa cha familia hatahitaji kutayarisha programu mpya kabisa kila wakati. Huenda akaona inafaa kufanya matayarisho baada ya kila funzo akiwa angali na mahitaji ya kiroho ya familia yake akilini. Vichwa fulani vya familia huandika kifupi ratiba ya mambo watakayozungumzia na kuitundika mahali ambapo wote katika familia wanaweza kuiona, kama vile kwenye friji. Kufanya hivyo huamsha upendezi na kuipa familia nafasi ya kutayarisha ikihitajika.
10. Wale wanaoishi peke yao wanaweza kutumiaje jioni ya Ibada ya Familia?
10 Namna Gani Ikiwa Niko Peke Yangu Katika Familia? Wale wanaoishi peke yao wanaweza kutumia jioni ya Ibada ya Familia kufanya funzo la kibinafsi. Programu nzuri ya funzo la kibinafsi inapaswa kuhusisha kusoma Biblia, kutayarisha mikutano, na kusoma magazeti ya Mnara wa Mlinzi na Amkeni! Wahubiri fulani huhusisha pia utafiti fulani au mradi wa kusoma mojawapo ya vitabu vyetu katika funzo lao la kibinafsi. Wakati mwingine, wanaweza kuamua kumwalika mhubiri au familia fulani kujiunga nao katika mazungumzo yenye kujenga ya Kimaandiko.
11, 12. Baadhi ya manufaa ya kuwa na jioni ya Ibada ya Familia kwa ukawaida ni yapi?
11 Kuna Faida Gani za Kuwa na Jioni ya Ibada ya Familia kwa Ukawaida? Wale wanaomwabudu Yehova kwa moyo wote humkaribia zaidi. Isitoshe, familia zinazoabudu pamoja huimarisha uhusiano wao. Wenzi fulani wa ndoa waliandika hivi kuhusu baraka ambazo wamefurahia: “Tukiwa mapainia wasio na watoto, sisi hutazamia kwa hamu jioni ya Ibada ya Familia. Uhusiano wetu wenyewe unaimarika na tunamkaribia Baba yetu wa mbinguni zaidi. Tunapoamka asubuhi ya siku ambayo tumepanga kujifunza pamoja, tunaambiana: ‘Hebu wazia, leo ni siku ya Ibada ya Familia!’”
12 Pia, mpango wa kuwa na jioni ya ibada ya familia huzisaidia familia zenye shughuli nyingi. Mama mmoja asiye na mwenzi, mwenye wana wawili na ambaye ni painia wa kawaida aliandika: “Zamani, ilikuwa shida kuwa na funzo la familia. Kwa sababu ya uchovu, halikuwa la kawaida na tulilifanya kiholela. Nilishindwa kulipangia vizuri. Kwa hiyo, ninawaandikia kuwashukuru sana kwa jioni ya Ibada ya Familia. Tumefanikiwa kuwa na funzo la familia kwa ukawaida na tumenufaika sana.”
13. Manufaa ambayo familia yenu itapata kutokana na mpango huo yanategemea nini?
13 Kama Sabato ilivyokuwa, jioni ya Ibada ya Familia ni zawadi kutoka kwa Baba yetu wa mbinguni, inayoweza kuzisaidia familia. (Yak. 1:17) Manufaa ya kiroho ambayo familia za Waisraeli walipata yalitegemea jinsi walivyotumia Sabato hizo. Vivyo hivyo, manufaa ambayo familia yetu itapata yanategemea jinsi tunavyotumia jioni ambayo tumepewa kwa ajili ya ibada ya familia. (2 Kor. 9:6; Gal. 6:7, 8; Kol. 3:23, 24) Kwa kuutumia mpango huo vizuri, familia yako inaweza kusema kama alivyosema mtunga-zaburi: “Lakini mimi, kumkaribia Mungu ni kwema kwangu. Nimeweka kimbilio langu katika Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova.”—Zab. 73:28.
[Blabu katika ukurasa wa 5]
Jioni ya Ibada ya Familia haipaswi kuwa wakati wenye kuchosha au usiovutia bali unapaswa kuwa wakati wenye furaha kwa sababu tunamwabudu Mungu mwenye furaha
[Picha katika ukurasa wa 6]
TUNZA
Madokezo ya Mambo ya Kufanya Wakati wa Jioni ya Ibada ya Familia
Biblia:
• Someni pamoja sehemu ya usomaji wa Biblia wa kila juma. Masimulizi mengine yameandikwa kwa njia ambayo mtu mmoja anaweza kusoma simulizi lenyewe, na wengine wasome maneno ya wahusika tofauti wanaozungumziwa.
• Igiza sehemu fulani ya usomaji wa Biblia.
• Mgawie mapema kila mshiriki wa familia sura za Biblia zilizoteuliwa atakazosoma, na aandike swali moja au mawili kuhusiana na sura hizo. Kisha fanyeni utafiti wa maswali ya kila mmoja.
• Kila juma, tengenezeni kadi iliyoandikwa andiko fulani na mjaribu kulikariri na kulieleza. Tengenezeni kadi nyingi na mjaribu kuzipitia kila juma kuona ni maandiko mangapi mnayoweza kukumbuka.
• Sikilizeni na kufuatana na usomaji wa Biblia uliorekodiwa.
Mikutano:
• Tayarisheni pamoja sehemu fulani ya mikutano.
• Jizoezeni kuimba nyimbo za Ufalme za juma linalofuata.
• Ikiwa mmoja wenu ana hotuba katika Shule ya Huduma ya Kitheokrasi au ana onyesho katika Mkutano wa Utumishi, zungumzieni jinsi inavyoweza kutolewa, au afanye mazoezi mbele ya familia.
Mahitaji ya Familia:
• Shughulikieni habari katika kitabu Vijana Huuliza au Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu.
• Fanyeni mazoezi ya jinsi ya kushughulikia hali ambayo inaweza kutokea shuleni.
• Fanyeni mazoezi ambayo wazazi wanaigiza sehemu za watoto na watoto wanaigiza sehemu za wazazi. Watoto wanafanya utafiti kuhusu habari fulani kisha wanaijadili na wazazi.
Huduma:
• Fanyeni mazoezi kwa ajili ya utumishi wa shambani wa mwisho wa juma.
• Zungumzieni miradi inayofaa ambayo familia inaweza kujiwekea ili kushiriki zaidi katika huduma wakati wa majira ya Ukumbusho au wakati wa likizo.
• Mpe kila mmoja katika familia dakika chache za kufanya utafiti kuhusu jinsi ya kujibu maswali tofauti yanayoweza kutokea katika huduma, kisha mfanye mazoezi.
Madokezo Zaidi:
• Someni pamoja makala kutoka katika magazeti ya karibuni.
• Mwombe kila mshiriki wa familia asome mapema makala inayomfurahisha katika magazeti ya karibuni, kisha atoe ripoti kuhusu makala hiyo wakati wa jioni ya ibada familia.
• Mara kwa mara mnaweza kumwalika mhubiri au wenzi fulani wa ndoa wajiunge nanyi wakati wa jioni ya Ibada ya Familia na labda mnaweza kuwaomba wawaeleze mambo fulani yaliyoonwa.
• Tazameni na mzungumzie moja ya video zetu.
• Zungumzieni habari yenye kichwa “Vijana Huuliza” au “Mazungumzo ya Familia” katika gazeti la Amkeni!
• Zungumzieni habari yenye kichwa “Wafundishe Watoto Wako” au “Kwa Ajili ya Vijana” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi.
• Someni na mzungumzie sehemu katika Kitabu cha Mwaka cha karibuni au kimoja cha vitabu tulivyopokea katika kusanyiko la wilaya lililopita.
• Baada ya kuhudhuria kusanyiko, pitieni mambo makuu.
• Chunguzeni uumbaji wa Yehova na mzungumzie mambo ambayo unatufunza kumhusu Yehova.
• Fanyeni mradi fulani pamoja, kama vile kutengeneza mfano wa kitu fulani, kuchora ramani, au chati.