Jifunzeni Neno la Mungu kwa Ukawaida Mkiwa Familia
“Binadamu lazima aishi, si kwa mkate pekee, bali kwa kila tamko linalokuja kupitia kinywa cha Yehova.”—MATHAYO 4:4.
1. Biblia husema nini kuhusu daraka la vichwa vya familia la kufundisha watoto wao njia za Yehova?
YEHOVA MUNGU alikumbusha vichwa vya familia mara nyingi kuhusu daraka lao la kufundisha watoto wao. Maagizo hayo yangewaandaa watoto kwa ajili ya maisha ya sasa na pia yangeweza kuwatayarisha kwa ajili ya maisha ya baadaye. Malaika akimwakilisha Mungu alimkazia Abrahamu daraka lake la kufundisha jamaa yake ili iweze ‘kushika njia ya BWANA.’ (Mwanzo 18:19) Wazazi Waisraeli walitakiwa wawaeleze watoto wao jinsi Mungu alivyowaokoa Waisraeli kutoka Misri na jinsi alivyowatolea Sheria kwenye Mlima Sinai, huko Horebu. (Kutoka 13:8, 9; Kumbukumbu la Torati 4:9, 10; 11:18-21) Vichwa vya familia walio Wakristo wanashauriwa walee watoto wao “katika nidhamu na rekebisho la akilini la Yehova.” (Waefeso 6:4) Hata ikiwa ni mzazi mmoja tu anayemtumikia Yehova, yeye apaswa kujitahidi kuwafundisha watoto wake njia za Yehova.—2 Timotheo 1:5; 3:14, 15.
2. Je, funzo la familia linahitajika ikiwa hakuna watoto nyumbani? Eleza.
2 Hilo halimaanishi kwamba funzo la familia la Neno la Mungu ni kwa ajili ya jamaa zenye watoto tu. Mume na mke huonyesha uthamini mzuri wa mambo ya kiroho wanapokuwa na funzo la familia hata ikiwa hakuna watoto nyumbani.—Waefeso 5:25, 26.
3. Kwa nini funzo la familia la kawaida ni muhimu?
3 Ili yawe na matokeo mazuri zaidi, maagizo yapasa kutolewa kwa ukawaida, kupatana na somo ambalo Yehova aliwafundisha Waisraeli nyikani: “Mwanadamu haishi kwa mkate tu, bali huishi kwa kila litokalo katika kinywa cha BWANA.” (Kumbukumbu la Torati 8:3) Kwa kutegemea hali za familia, huenda jamaa fulani zikapanga kujifunza kila juma; nyingine zikajifunza kwa vipindi vifupi-vifupi kila siku. Hata iwe mtachagua mpango gani, msikose kuratibu wakati kwa ajili ya funzo. ‘Nunueni wakati’ kwa ajili ya funzo. Kujidhabihu ili kupata wakati huo ni jambo linalonufaisha sana. Uhai wa washiriki wa familia yako umo hatarini.—Waefeso 5:15-17; Wafilipi 3:16.
Malengo ya Kukumbukwa
4, 5. (a) Ni nini ambacho Yehova aliwatolea wazazi kupitia Musa kiwe lengo muhimu katika kuwafundisha watoto wao? (b) Hilo lahusisha nini leo?
4 Unapoongoza funzo la familia, litanufaisha zaidi ukikumbuka kuwa na malengo hususa. Chunguza malengo kadhaa.
5 Kwenye kila funzo, jaribu kusitawisha upendo kwa Yehova Mungu. Waisraeli walipokusanyika kwenye uwanda wa Moabu, kabla ya kuingia katika Bara Lililoahidiwa, Musa alikaza fikira zao kwenye ile ambayo baadaye Yesu Kristo angeitambulisha kuwa “amri kubwa zaidi sana katika ile Sheria.” Amri gani? “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.” (Mathayo 22:36, 37; Kumbukumbu la Torati 6:5) Musa aliwahimiza Waisraeli wakaze amri hiyo katika mioyo yao wenyewe na kuwafundisha watoto wao kuihusu. Jambo hilo lingehitaji kurudia-rudia, kuvuta fikira kwenye sababu za kumpenda Yehova, kushughulika na mitazamo na mwenendo uwezao kuzuia kuonyeshwa kwa upendo huo, na kuonyesha upendo wao kwa Yehova katika maisha yao wenyewe. Je, watoto wetu wanahitaji maagizo ya aina hiyo? Ndiyo! Nao pia wanahitaji msaada ili ‘kutahiri mioyo yao,’ yaani, kuondoa chochote ambacho kingewazuia wasimpende Mungu. (Kumbukumbu la Torati 10:12, 16; Yeremia 4:4) Huenda baadhi ya vizuizi hivyo vikawa tamaa ya vitu vya ulimwengu na fursa za kujitia katika shughuli zake. (1 Yohana 2:15, 16) Upendo kwa Yehova wapaswa kuwa hai, dhahiri, ukitusukuma tufanye mambo yampendezayo Baba yetu wa kimbingu. (1 Yohana 5:3) Ili funzo la familia yako liwe na manufaa ya kudumu, kila kipindi chapasa kuongozwa katika njia inayoimarisha upendo huo.
6. (a) Ni nini kihitajiwacho ili kutoa ujuzi sahihi? (b) Maandiko yanakaziaje umuhimu wa ujuzi sahihi?
6 Toa ujuzi sahihi juu ya matakwa ya Mungu. Hilo lahusisha nini? Lahusisha mengi zaidi ya uwezo wa kusoma na kutoa majibu kutoka kwa gazeti au kitabu. Kwa kawaida lahitaji mazungumzo ili kuhakikisha kwamba maneno muhimu na mawazo makuu yanaeleweka vizuri. Ujuzi sahihi ni muhimu katika kuvaa utu mpya, katika kuzingatia mambo yaliyo ya maana hasa unaposhughulika na matatizo maishani, na vilevile, katika kufanya yale yampendezayo Mungu kikweli.—Wafilipi 1:9-11; Wakolosai 1:9, 10; 3:10.
7. (a) Familia yaweza kusaidiwa kutumia maishani habari inayojifunza kwa kutumia maswali gani? (b) Maandiko yanakaziaje thamani ya kuwa na lengo kama hilo?
7 Saidia washiriki wa familia watumie maishani mambo wanayojifunza. Ukiwa na lengo hilo akilini, uliza hivi wakati wa kila funzo la familia: ‘Habari hii inapaswa iathirije maisha yetu? Je, yahitaji tufanye mabadiliko yoyote katika maisha yetu ya sasa? Kwa nini tutake kufanya mabadiliko?’ (Mithali 2:10-15; 9:10; Isaya 48:17, 18) Kuwa waangalifu vya kutosha kutumia maishani mambo mnayojifunza kwaweza kuchangia ukuzi wa kiroho wa washiriki wa familia.
Tumia Vifaa vya Kufundishia kwa Hekima
8. Jamii ya mtumwa imeandaa vifaa gani vya kujifunzia Biblia?
8 “Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” ametoa vifaa vingi vinavyoweza kutumiwa kujifunza. Gazeti la Mnara wa Mlinzi, la kutumia pamoja na Biblia, linapatikana katika lugha 131. Kuna vitabu vya kujifunzia Biblia katika lugha 153, broshua katika lugha 284, kaseti za kusikilizia Biblia katika lugha 61, kaseti za vidio katika lugha 41, hata programu ya kompyuta ya kufanya utafiti wa Biblia katika lugha 9!—Mathayo 24:45-47.
9. Tunaweza kutumiaje mashauri katika maandiko yaliyoonyeshwa kwenye fungu hili tunapokuwa na funzo la familia la Mnara wa Mlinzi?
9 Jamaa nyingi hutumia wakati wa funzo la familia ili kujitayarisha kwa ajili ya Funzo la kutaniko la Mnara wa Mlinzi. Kufanya hivyo kwaweza kusaidia kama nini! Gazeti la Mnara wa Mlinzi lina chakula muhimu cha kiroho ambacho huandaliwa ili kuimarisha watu wa Yehova ulimwenguni pote. Mnapojifunza Mnara wa Mlinzi mkiwa familia, fanyeni zaidi ya kusoma mafungu na kujibu maswali yaliyochapwa. Jitahidini sana kuelewa mambo. Chukueni wakati kusoma maandiko yaliyotajwa bila kunukuliwa. Waombe washiriki wa familia waeleze jinsi mambo hayo yanavyohusiana na yale yaliyotajwa katika fungu linalozungumziwa. Husisha moyo.—Mithali 4:7, 23; Matendo 17:11.
10. Ni nini kiwezacho kufanywa ili kuhusisha watoto katika funzo na kulifanya liwafurahishe?
10 Ikiwa kuna watoto katika jamaa yako, unaweza kufanya nini ili funzo lisiwe desturi tu ya familia, bali liwe lenye kujenga, lenye kupendeza, na lenye furaha? Jitahidi sana kushirikisha kila mmoja katika njia ifaayo ili fikira zikazwe kwenye habari inayozungumziwa. Inapowezekana, panga kila mtoto awe na Biblia yake mwenyewe na gazeti mnalojifunza. Kwa kuiga uchangamfu ulioonyeshwa na Yesu, huenda mzazi akataka mtoto mchanga aketi karibu sana naye, labda akimkumbatia mtoto huyo kwa mkono mmoja. (Linganisha Marko 10:13-16.) Huenda kichwa cha familia akataka kijana aeleze picha fulani katika habari wanayozungumzia. Mtoto mchanga aweza kupewa mgawo mapema wa kusoma andiko fulani. Mtoto mwingine mwenye umri mkubwa zaidi aweza kupewa mgawo wa kutaja fursa mbalimbali za kutumia habari wanayojifunza.
11. Ni vifaa gani vingine vya kujifunzia ambavyo vimeandaliwa, navyo vyaweza kutumiwaje kwa manufaa kuhusiana na funzo la familia mahali vinapopatikana?
11 Ingawa huenda ukawa unatumia Mnara wa Mlinzi kuwa msingi wa mazungumzo yako, usisahau vifaa vingine vya kujifunzia ambavyo vyapatikana katika lugha nyingi. Ikiwa habari au ufafanuzi wahitajiwa ili kuelewa usemi fulani wa Biblia, kichapo Insight on the Scriptures chaweza kuutoa. Maswali mengine yaweza kujibiwa kwa kurejezea Watch Tower Publications Index au kwa kutumia programu ya kompyuta ya kufanya utafiti ambayo imeandaliwa na Sosaiti. Kujifunza kutumia vifaa hivi, ikiwa vinapatikana katika lugha yako, kwaweza kuwa sehemu yenye manufaa ya funzo la familia. Ukiwa na lengo la kuchochea upendezi wa wachanga, pia huenda ukatenga sehemu ya wakati wako wa funzo ili kutazama sehemu fulani ya vidio za Sosaiti zenye maagizo au kusikiliza sehemu ya drama kwenye kaseti, kisha kuizungumzia. Kutumia ifaavyo vifaa hivi vya kujifunzia kutasaidia kufanya funzo la familia yako liwe lenye kupendeza na lenye kunufaisha familia nzima.
Rekebisha Funzo Lifae Mahitaji ya Familia Yako
12. Funzo la familia laweza kutimizaje fungu katika kushughulikia mahitaji muhimu ya famillia?
12 Huenda ikawa kwa kawaida familia yako hujifunza somo la Mnara wa Mlinzi la kila juma. Lakini fahamu matatizo na maoni ya msingi ya familia. Ikiwa si lazima mama afanye kazi ya kuajiriwa, anaweza kutumia wakati pamoja na watoto kila siku wanapokuja nyumbani kutoka shuleni. Hali fulani zaweza kushughulikiwa wakati huo; huenda nyingine zikahitaji uangalifu zaidi. Kunapokuwa na mahitaji muhimu ya familia, usiyapuuze. (Mithali 27:12) Huenda hayo yakahusisha hali nyinginezo mbali na matatizo shuleni. Teua habari ifaayo, na uijulishe familia mapema kuhusu kile mtakachojifunza.
13. Kwa nini mazungumzo ya familia kuhusu jinsi ya kukabiliana na umaskini yaweza kunufaisha?
13 Kwa mfano, sehemu kubwa ya dunia imekumbwa na umaskini; hivyo katika mahali pengi, huenda ikahitajika kuzungumzia jinsi ya kukabiliana na hali hiyo. Je, jamaa yako ingenufaika na funzo la familia linalokazia hali halisi maishani na kanuni ya Biblia?— Mithali 21:5; Mhubiri 9:11; Waebrania 13:5, 6, 18.
14. Ni hali gani zaweza kufanya mazungumzo ya familia juu ya maoni ya Yehova kuhusu jeuri, vita, na kutokuwamo kwa Kikristo yafae?
14 Jeuri ni habari nyingine inayohitaji kuzungumziwa. Sote twahitaji kukazia kikiki maoni ya Yehova katika akili na mioyo yetu. (Mwanzo 6:13; Zaburi 11:5) Funzo la familia juu ya habari hiyo laweza kuandaa hali ya kuzungumzia jinsi ya kushughulika na wachokozi shuleni, kama watoto watajifunza mbinu za karate, na jinsi ya kuchagua tafrija ifaayo. Mapambano yenye jeuri yamekuwa mengi; karibu kila nchi imekumbwa na vita vya wenyewe kwa wenyewe, ugomvi wa kisiasa au wa kikabila, au vita vya magenge. Tokeo likiwa kwamba, familia yako huenda ikahitaji kuzungumza juu ya kudumisha mwenendo wa Kikristo ingawa wamezungukwa na vikundi vyenye kupigana.—Isaya 2:2-4; Yohana 17:16.
15. Maagizo juu ya ngono na ndoa yapasa yatoleweje kwa watoto?
15 Watoto wanapokua, wanahitaji maagizo yanayofaa umri wao juu ya ngono na ndoa. Katika tamaduni fulani wazazi walio wengi hawazungumzii ngono kamwe pamoja na watoto wao. Watoto wasio na habari waweza kupata maoni yaliyopotoka kutoka kwa vijana wengine, na matokeo yaweza kuwa yenye msiba. Je, haingekuwa afadhali kumwiga Yehova, ambaye hutoa shauri moja kwa moja, lakini kwa busara kuhusu jambo hilo katika Biblia? Shauri la Mungu litawasaidia watoto wetu wadumishe hali ya kujistahi na kuwatendea kwa heshima wale wa jinsia tofauti. (Mithali 5:18-20; Wakolosai 3:5; 1 Wathesalonike 4:3-8) Hata ikiwa tayari umezungumzia mambo haya, usisite kufanya hivyo tena. Hali mpya zitokeapo, ni muhimu kurudia mambo hayo.
16. (a) Funzo la familia hufanywa lini katika jamaa mbalimbali? (b) Umeshughulikiaje vizuizi ili kuwa na funzo la familia la kawaida?
16 Funzo la familia laweza kufanywa wakati gani? Kwa kuiga familia za Betheli duniani pote, jamaa nyingi zimeratibu kufanya funzo la familia Jumatatu jioni. Nyingine zina ratiba tofauti. Huko Argentina familia yenye watu 11, kutia ndani watoto 9, iliamka kwa ukawaida saa 11 kila alfajiri ili kufanya funzo lao la familia. Kwa sababu ya ratiba za kazi zilizokuwa tofauti, hawangeweza kufanya funzo hilo wakati mwingine. Haikuwa rahisi, lakini kufanya hivyo kulikaza katika akili na mioyo ya watoto hao umuhimu wa funzo la familia. Nchini Filipino mzee mmoja alifanya funzo la familia la kawaida pamoja na mke wake na watoto wao watatu walipokuwa wakikua. Katikati ya juma wazazi pia walijifunza kibinafsi na kila mtoto ili kila mmoja wao afanye kweli kuwa mali yake mwenyewe. Huko Marekani, dada mmoja ambaye mume wake si Shahidi hutembea na watoto wake kila asubuhi hadi kwenye basi la shule. Wanapongojea basi hilo, wao hutumia takriban dakika kumi pamoja wakisoma na kuzungumzia habari ifaayo ya kujifunza itegemeayo Maandiko, kisha mama huyo hutoa sala fupi kabla ya watoto kupanda basi. Katika Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo, mwanamke mmoja ambaye mume wake asiyeamini aliiacha familia hulazimika kujitahidi kujifunza kwa sababu hana elimu ya kutosha. Mwana wake aliye mtu mzima husaidia kwa kuitembelea familia hiyo kila juma ili kuongoza funzo linalotia ndani mama yake na ndugu zake wachanga. Mama huyo huweka kielelezo kizuri kwa kujitayarisha kwa bidii. Je, kuna hali inayofanya iwe vigumu kuwa na funzo la familia la kawaida katika jamaa yako? Usikate tamaa. Jitahidi sana kupata baraka ya Yehova juu ya jitihada zako za kuwa na funzo la Biblia la kawaida.—Marko 11:23, 24.
Thawabu Zinazotokana na Kustahimili
17. (a) Ni nini kinachohitajiwa ili kuwa na funzo la familia la kawaida? (b) Ni jambo gani lililoonwa ambalo latoa kielelezi juu ya umuhimu wa kuagiza familia kwa ukawaida kuhusu njia za Yehova?
17 Kupanga kunahitajiwa. Kustahimili kunatakiwa pia. Lakini manufaa zinazotokana na funzo la familia la kawaida zinafanya funzo hilo listahili. (Mithali 22:6; 3 Yohana 4) Huko Ujerumani, Franz na Hilda walilea watoto 11 katika familia yao. Miaka kadhaa baadaye, binti yao Magdalena alisema hivi: “Ninachofikiria kuwa muhimu zaidi leo ni kwamba hakuna hata siku moja iliyopita bila sisi kupokea mafundisho fulani ya kiroho.” Wakati roho ya utukuzo wa taifa ilipochacha wakati wa Adolf Hitler, baba ya Magdalena alitumia Biblia kutayarisha familia yake kwa ajili ya majaribu ambayo aling’amua yalikuwa yanakuja. Baada ya muda, washiriki wa familia waliokuwa wachanga zaidi walikamatwa na kupelekwa kwenye shule ya kuadibisha; wengine katika familia wakakamatwa, wakatiwa katika gereza na kambi za mateso. Wengine wakauawa. Wote walidumisha imani thabiti—siyo tu wakati wa mnyanyaso huo mkali bali pia, kwa waokokaji, katika miaka iliyofuata.
18. Jitihada za wazazi wasio na wenzi zimethawabishwaje?
18 Wazazi wengi wasio na wenzi na pia wale ambao wenzi wao wana imani tofauti, hali kadhalika wamewatolea watoto wao maagizo ya Biblia kwa ukawaida. Mama mmoja, mjane huko India, alijitahidi sana kufundisha watoto wake wawili kumpenda Yehova. Hata hivyo, alivunjika moyo mwana wake alipojitenga na watu wa Yehova. Alimwomba Yehova amsamehe makosa yoyote aliyofanya alipokuwa akimzoeza mwana wake. Lakini mwana huyo hakuwa amesahau kabisa yale aliyokuwa amejifunza. Baada ya muda wa zaidi ya miaka kumi, alirudi, akafanya maendeleo ya kiroho, akawa mzee wa kutaniko. Sasa yeye na mke wake wanatumikia wakiwa wahudumu mapainia wa wakati wote. Wamekuwa wenye shukrani kama nini wazazi wale ambao wamezingatia moyoni shauri la Yehova na tengenezo lake kuhusu kutoa maagizo ya Biblia kwa ukawaida katika familia! Je, unatumia shauri hilo katika jamaa yako?
Je, Waweza Kueleza?
◻ Kwa nini funzo la familia la kawaida ni muhimu?
◻ Malengo yetu yapasa kuwa nini wakati wa kila funzo la familia?
◻ Ni vifaa gani vya kufundishia ambavyo vimetolewa kwa ajili yetu?
◻ Funzo laweza kurekebishwaje lifae mahitaji ya familia?
[Picha katika ukurasa wa 15]
Malengo hususa yataboresha funzo la familia yako