Fulizeni Kutembea kwa Maendeleo Katika Kawaida Yenye Utaratibu
1 Mtume Paulo alikuwa na shauku ya pekee kwa kutaniko la Filipi, ambalo yeye alitumika kulianzisha. Alishukuru kwa maandalizi yao ya vitu vya kimwili yenye fadhili naye akasema juu yao kuwa kielelezo chema.—2 Kor. 8:1-6.
2 Barua ya Paulo kwa Wafilipi ilichochewa na upendo wenye kina kirefu. Kitabu Insight, Buku la 2, ukurasa 631, charipoti: “Katika barua yote yeye analitia moyo kutaniko la Filipi liendelee na mwendo wao mzuri—wakitafuta uelewevu mwingi na kushika kwa uhakika Neno la uhai, imani yenye nguvu, na tumaini katika tuzo ijayo.” Waliitikia kwa uchangamfu, wakiunganisha kwa imara kifungo cha upendo miongoni mwao na mtume huyu. Maneno ya Paulo yana maana ya pekee kwetu sisi leo, yakitupa sababu nzuri ya kufikiria kwa uangalifu onyo lake la upole, hasa yaliyoandikwa katika Wafilipi 3:15-17.
3 Mtazamo Mkomavu wa Akilini Ni Muhimu: Kwenye Wafilipi 3:15, Paulo aliandika akiwa mwanamume mwenye maarifa ya miaka mingi. Alitambua maendeleo ya kiroho ya Wafilipi, akiwasihi wakiwa Wakristo wakomavu wenye mwelekeo ufaao wa akilini. Kwa kuwa mwelekeo wao wa akilini ulionyesha unyenyekevu na uthamini ulioonyeshwa na Yesu, wangeendelea kuwa ‘wana wa Mungu wasio na lawama, wala udanganyifu . . . , wakishika neno la uzima.’ (Flp. 2:15, 16) Tunaposoma maneno ya Paulo, twapaswa kuhisi kwamba yeye anaongea nasi. Hivyo twatamani kuwa na mwelekeo huohuo wa akilini ambao Yesu alikuwa nao, tukionyesha uthamini mnyenyekevu kwa mapendeleo yetu. Twaendelea kumsihi Yehova kupitia sala, tukiomba msaada kwa jambo hili na mambo mengine.—Flp. 4:6, 7.
4 Kama vile Wafilipi 3:16 huonyesha, sisi sote twapaswa kujitahidi kufanya maendeleo. Neno “maendeleo” lamaanisha “kusonga mbele, kuendelea mbele.” Watu wenye kufanya maendeleo ‘wanapendezwa na mawazo mapya, utafiti, au fursa mpya.’ Paulo alitaka Wafilipi waelewe kwamba Ukristo hausimami kamwe bila kusonga na wale wanaoudai lazima wafulize kusonga mbele. Roho yao ya kufanya maendeleo ingeonyeshwa na utayari wao wa kujichunguza wenyewe, kutambua udhaifu wao, na kufikia fursa za kufanya mengi zaidi au kuboresha yale wanayofanya sasa. Leo tengenezo la Yehova la kidunia lafuliza kusonga mbele kwa maendeleo, likipanua daima eneo la utendaji walo na uelewevu walo wa Neno la Mungu. Kila mmoja wetu apaswa kwenda sambamba nalo, akitumia kwa manufaa maandalizi yalo yote na kushiriki kikamili katika kazi yalo.
5 Maendeleo Yahitaji Kawaida Yenye Utaratibu: Paulo aliendelea kwa kuwasihi ndugu zake ‘waendelee kutembea kwa utaratibu katika kawaida hiyohiyo.’ (Flp. 3:16, NW) Kuwa wenye utaratibu hututaka tuweke watu au vitu mahali panapovipasa katika uhusiano wavyo na tuwe na tabia njema. Wakristo katika Filipi walijiweka mahali pao palipowafaa, wakikaa karibu na tengenezo la Yehova na mtu na mwenzake. Maisha yao yaliongozwa na sheria ya upendo. (Yn. 15:17; Flp. 2:1, 2) Paulo aliwasihi ‘waenende kama inavyoipasa Injili.’ (Flp. 1:27) Uhitaji wa utaratibu na mwenendo mzuri vilevile ni muhimu kwa Wakristo leo.
6 Kawaida ni mfanyizo wa kimazoea wa utaratibu uliowekwa. Hivyo inahusiana sana na njia ya kidesturi ya kufanya mambo. Kuwa na kawaida kwaweza kuwa kwa manufaa yetu kwa sababu si lazima tutue na kuwazia tunapofanya maamuzi juu ya hatua yetu itakayofuata—tayari tumesitawisha kigezo kilichowekwa tunachofuata kwa kulazimishwa na zoea.
7 Kawaida ya kitheokrasi yenye utaratibu huwa na mazoea na desturi ambazo ni za maana, zenye kunufaisha, za kimungu—zikiwa na lengo la kutujenga wenyewe kiroho, kuwasaidia wengine, na, ikiwezekana, kufanya mengi zaidi katika utumishi wa Yehova. Mafanikio katika kufikia miradi hii yahitaji kuweka na kudumisha kawaida inayotia ndani funzo la kibinafsi, kuhudhuria mikutano kwa ukawaida, na kushiriki katika kazi ya kuhubiri.
8 Mambo Muhimu Yanayotiwa Katika Kawaida Yenye Utaratibu: Jambo moja muhimu ni “ujuzi sahihi na ufahamu kamili.” (Flp. 1:9, NW) Funzo la kibinafsi huongeza kina cha imani yetu, hutia nguvu uthamini wetu kwa ile kweli, na hutuchochea kwa kazi njema. Hata hivyo, watu fulani wameona kuwa jambo gumu kupatana katika mazoea yao ya kujifunza. Sababu moja iliyo kuu inayotolewa ni ukosefu wa wakati.
9 Manufaa za kusoma Biblia kila siku haziwezi kutiliwa mkazo kupita kiasi. Mafundisho yayo ni yenye ‘kufaa’ kwa kila njia. (2 Tim. 3:16, 17) Twaweza kupataje wakati kwa ajili ya funzo la Biblia katika kawaida yetu ya kila siku? Wengine wameona kwamba wanaweza kufanya hivyo kwa kuamka dakika chache mapema asubuhi, ilhali akili yao ikiwa tayari. Wengine wanaona ikiwa vema wanaposoma dakika chake kabla hawajaenda kulala usiku. Wake walio nyumbani wakati wa mchana huenda wakaweza kuweka kando wakati mchache alasiri kabla wengine hawajafika nyumbani kutoka kazini au shuleni. Kwa kuongezea kusoma Biblia kwa ukawaida, wengine wametia ndani kusoma kile kitabu Proclaimers (Wapiga-Mbiu) katika kawaida yao ya kila juma ya kujifunza.
10 Tunapositawisha mazoea mapya, kuna uwezekano hasa kwamba yatahitilafiana na mazoea ya zamani. Zamani huenda tulikuwa na mwelekeo wa kuruhusu utendaji usiokuwa na maana uchukue wakati uliopo. Kuacha kigezo hicho si rahisi. Hakuna mtu atakayetuamuru juu ya mazoea yetu ya kujifunza; wala hatutozwi hesabu kwa yale tunayofanya kuhusu jambo hili. Kudumisha mazoea yetu ya kujifunza kwategemea sana uthamini wetu kwa “mambo yaliyo ya maana zaidi” na utayari wetu wa kununua “wakati unaofaa” ili kunufaika kutokana nazo.—Flp. 1:10; Efe. 5:16, NW.
11 Mikutano ya Kikristo hutimiza sehemu muhimu katika maendeleo yetu ya kiroho, yakiandaa mafundisho na kitia-moyo kinachohitajiwa. Hivyo, kuhudhuria mikutano ni sehemu nyingine muhimu ya utaratibu wa kawaida yetu. Paulo alikazia umaana walo. Si uchaguzi unaoamuliwa na mapendezi.—Ebr. 10:24, 25.
12 Utaratibu waweza kuonyeshwaje tunapopanga ratiba yetu ya kila juma ya utendaji? Wengine hupanga nyakati hususa kushughulikia mambo ya kibinafsi kisha wanajaribu kusogeza mikutano kwenye nafasi zozote zinazopatikana, lakini yapasa kuwa kinyume cha hivyo. Mikutano yetu ya kila juma yapasa kupewa nafasi ya kwanza, nao utendaji ule mwingine upangiwe wakati uliobaki.
13 Uhudhuriaji wa mikutano wa kawaida wahitaji upangaji mzuri na ushirikiano wa familia. Wakati wa siku za katikati ya juma wengi wetu tuna ratiba yenye shughuli sana ambayo hutuacha tumebanwa na wakati. Hili lamaanisha kwamba, ikiwezekana, chakula cha jioni chapasa kuratibiwa mapema vya kutosha ili familia iwe na wakati wa kutosha kula, kujitayarisha, na kufika mkutanoni kabla haujaanza. Kwa upande huo washiriki wa familia waweza kushirikiana kwa njia tofauti-tofauti.
14 Utumishi wa shambani wa kawaida si wa kupuuzwa ikiwa tutaendelea kutembea kwa maendeleo katika kawaida yenye utaratibu. Sisi sote twatambua waziwazi daraka letu zito la kuhubiri ujumbe wa Ufalme. Hilo ndilo hutufanya tuwe Mashahidi wa Yehova. (Isa. 43:10) Kwa kuwa ndio kazi yenye uharaka sana na yenye manufaa zaidi inayofanywa leo, hatuwezi kwa vyovyote kuiona kama sehemu ya kushtukia tu ya kawaida yetu ya kila siku. Kama vile Paulo alivyoshauri: “Na tumpe Mungu dhabihu ya sifa daima, yaani, tunda la midomo iliungamayo jina lake.”—Ebr. 13:15.
15 Tunapopangia utendaji wetu kila juma, nyakati hususa zapasa kuwekwa kando kwa ajili ya utumishi wa shambani. Yamkini kutaniko lina mikutano kwa ajili ya utumishi inayopangwa nyakati kadhaa kila juma, na ni jambo tu la kuamua ni ipi tunayoweza kuiunga mkono. Ingekuwa vizuri kushiriki kila sehemu ya utumishi, kama vile mahubiri ya nyumba kwa nyumba tukiwa na magazeti na fasihi nyinginezo, kufanya ziara za kurudia, na kuongoza mafunzo ya Biblia. Tunaweza hata kupanga mapema kutoa ushahidi wa vivi-hivi kwa kubeba fasihi na kuwa chonjo kwa fursa za kuanzisha mazungumzo. Kwa kuwa kwa kawaida sisi hutoka na wengine, twahitaji kuuliza juu ya ratiba yao ili tuweze kufanya mipango ambayo itatufaa sote.
16 Kawaida yetu ya kuhubiri yapasa kusitawishwa kujapokuwa kutojali kunakoonekana katika eneo. Twajua mapema kwamba ni wachache tu watakaoitikia vizuri. (Mt. 13:15; 24:9) Ezekieli aliagizwa ahubirie watu ‘waasi, wakaidi, na wenye mioyo migumu.’ Yehova aliahidi kumsaidia Ezekieli kwa kufanya ‘kipaji cha uso chake kigumu kama vipaji vya nyuso vyao,’ yaani, “kama almasi ilivyo ngumu kuliko gumegume.” (Eze. 2:3, 4; 3:7-9) Kwa hiyo kawaida ya kila mara kwa utumishi wa shambani yahitaji udumifu.
17 Vielelezo Vyema vya Kuiga: Wengi wetu hufanya vema katika utumishi wa shambani kunapokuwa na mtu wa kuongoza. Paulo na waandamani wake waliweka kielelezo chema, naye aliwasihi wengine wamwige. (Flp. 3:17) Kawaida yake ilitia ndani mambo yote muhimu ya kumwendeleza awe mwenye nguvu kiroho.
18 Leo pia, tumebarikiwa kuwa na vielelezo vyema. Kwenye Waebrania 13:7, Paulo alisihi hivi: “Wakumbukeni wale waliokuwa wakiwaongoza, . . . tena, kwa kuchunguza sana mwisho wa mwenendo wao, iigeni imani yao.” Bila shaka, Kristo ni Kielelezo chetu, lakini twaweza kuiga imani iliyozoewa na wale wanaoongoza. Kama vile Paulo, wazee wapaswa kuhangaikia uhitaji wa kuwa vielelezo vyema kwa wengine. Ijapokuwa hali zao huenda zikatofautiana, kila mmoja apaswa kuweza kuonyesha kuwa anasitawisha utaratibu wa kawaida kwa kuweka masilahi ya Ufalme kwanza. Hata wakiwa na wajibu wa kimwili na wa familia, wazee wapaswa kuwa na mazoea mazuri yaliyowekwa ya funzo la kibinafsi, hudhurio la mikutano, na kuongoza katika utumishi wa shambani. Wazee wanapothibitisha kwamba ‘wanasimamia nyumba zao vema,’ wote katika kutaniko watatiwa moyo waendelee kufanya kazi kwa kawaida yenye utaratibu.—1 Tim. 3:4, 5.
19 Miradi kwa Mwaka Mpya wa Utumishi: Mwanzo wa mwaka mpya wa utumishi ni wakati ufaao wa kuangalia kawaida yetu ya kibinafsi. Pitio la utendaji wetu wa mwaka uliopita waonyesha nini? Tuliweza kudumisha, au kufanyia maendeleo, kiwango chetu cha utendaji? Huenda ikawa tulikuwa wenye bidii katika funzo letu la kibinafsi. Huenda tulihudhuria mikutano kwa ukawaida mzuri au tuliongeza utumishi wetu wa shambani kwa kujiandikisha tukawa mapainia-wasaidizi. Labda tunaweza kutaja vitendo hususa vya fadhili vya Kikristo tulivyofanya kwa niaba ya wengine katika kutaniko letu au familia yetu. Ikiwa ndivyo, tuna sababu ya kufurahi kwamba tumetembea katika njia impendezayo Mungu, nasi tuna sababu nzuri ya “kuzidi sana.”—1 The. 4:1.
20 Vipi ikiwa kawaida yetu ilikuwa tuseme isiyo ya kufuatana au isiyo na utaratibu? Tuliathiriwaje kiroho? Maendeleo yetu yalicheleweshwa kwa sababu fulani? Kufanya maendeleo huanza kwa kuomba Yehova msaada. (Flp. 4:6, 13) Zungumzia mahitaji yako pamoja na familia yote, ukiomba msaada wao katika kurekebisha sehemu zinazohusu kawaida yako. Ikiwa una matatizo, waombe wazee msaada. Tukifanya jitihada yenye bidii na kukubali mwelekezo wa Yehova, twaweza kuwa na uhakika kwamba tutaepuka kuwa “ama wasiotenda ama wasiozaa matunda.”—2 Pet. 1:5-8, NW.
21 Kutembea katika kawaida yenye utaratibu kwaongoza kwenye baraka zinazofanya jitihada zako zistahiki. Unapoazimia kutembea kwa kuendelea katika kawaida yenye utaratibu, ‘si kwa ulegevu; ukiwa na juhudi katika roho yako; ukimtumikia Bwana [“Yehova,” NW].’ (Rum. 12:11)—Kwa uchunguzaji zaidi wa habari hii, ona Mnara wa Mlinzi wa Novemba 15, 1985, kurasa 27-31.