Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 11/15 kur. 27-31
  • ‘Tuendelee Kutembea kwa Utaratibu Katika Kawaida li Hii’

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • ‘Tuendelee Kutembea kwa Utaratibu Katika Kawaida li Hii’
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kuendelea Kusitawi
  • Kawaida ya Utaratibu
  • Uwe mfano katika usemi na mwenendo
  • Kufanya bidii katika kusoma, kuonya, na kufundisha
  • Usidharau zawadi ya utumishi
  • Jitihada Yenye Kuendelea Inaleta Baraka
  • Fanya Maendeleo Yako Yawe Wazi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
  • Vijana—Fanyeni Maendeleo Yenu Yawe Wazi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2009
  • Dhihirisha Maendeleo Yako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Uwe Mwenye Maendeleo
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 11/15 kur. 27-31

‘Tuendelee Kutembea kwa Utaratibu Katika Kawaida li Hii’

“Kwa kadiri tulivyofanya maendeleo, na tuendelee kutembea kwa utaratibu katika kawaida ii hii.”​—WAFILIPI 3:16, New World Translation.

1, 2. (a) Vijana walio mfano mwema ni chanzo chenye kutia moyo jinsi gani? (b) Lakini, ni maswali gani yanayowahusu ambayo yanakuja akilini?

ALISA alipokuwa amepita kidogo miaka miwili, alifurahisha kila mtu kwa kuweza kutaja-taja majina ya vitabu vyote 66 vya Biblia, kurudia majina ya wale mitume 12, na kueleza kwa ishara matunda tisa ya roho ya Mungu. (Mathayo 10:2-4; Wagalatia 5:22, 23) Alipokuwa katika darasa la tano shuleni, alikuwa akiongoza funzo la Biblia la kila juma na msichana aliyekuwa darasa la tatu, ambaye, naye, aliweza kufanya nduguye mkubwa apendezwe na Biblia. Alisa na rafikiye mdogo wamejiwekea mradi. Wanatazamia kuwa wenzi katika kazi ya kuhubiri wakati wote wakiwa mapainia wa pekee muda si muda.

2 Hakika, ingependeza ye yote wetu kujua watoto kama hao, na inaelekea sana unajua wengine wa namna hiyo. Lakini, wakati uo huo, tunajiuliza: Watakuwaje watakapokua? Je! wataendeleza usitawi wao wa kiroho mpaka wafikie mradi wao? Au je, watavutwa kando na mambo mengine na kuanguka njiani?

Kuendelea Kusitawi

3. Ni nani wanaohitaji kufanya maendeleo?

3 Kwa wazi vijana wa jinsi hiyo wanahitaji kusitawi sana kabla hawajafikia mradi wao. Lakini je, ni vijana na wapya tu wanaohitaji kufanya maendeleo? Kwa kweli, je, maendeleo ni ya lazima mpaka tu mtu anapofikia kukomaa kwa Kikristo au anapokuwa anastahili pendeleo fulani? Hata kidogo. Fikiria mtume Paulo. Badala ya kuridhika na aliyokuwa ametimiza, alisema katika barua yake aliyowaandikia Wafilipi: “Si kwamba nimekwisha kufika, au nimekwisha kuwa mkamilifu; la! bali nakaza mwendo ili nipate kulishika lile ambalo kwa ajili yake nimeshikwa na Kristo Yesu.”​—Wafilipi 3:12.

4. Ni “mradi” gani ambao mtume Paulo alikuwa akifuatia?

4 Kwa wazi, Paulo hakuwa akizungumza juu ya kufikia kukomaa, kwa maana hakukuwa shaka kwamba yeye tayari alikuwa Mkristo aliyekomaa. Hata hivyo alisema alikuwa ‘anakaza mwendo ili apate’ jambo fulani ambalo alikuwa bado ‘kulishika.’ Lilikuwa nini? Paulo aliendelea kueleza hivi: “Ninafuatia kuelekea mradi wa zawadi ya mwito wa juu wa Mungu kwa njia ya Kristo Yesu.” (Wafilipi 3:14, NW) Mradi aliokuwa akifuatia haukuwa ukomavu wa Kikristo tu au kustahili cheo fulani tu, bali lilikuwa jambo kubwa zaidi. Kwake yeye na Wakristo wapakwa mafuta wenzake, ulikuwa ni “mwito wa juu,” tumaini la uzima wa kimbingu kupitia ufufuo.

5. (a) Ni kwa sababu gani ukuzi wenye kuendelea ni wa lazima? (b) ‘Kusahau mambo yaliyo nyuma’ kungeweza kutia nini ndani?

5 Jambo hilo linatusaidia tuone sababu ya kuendelea kukua na kusitawi kiroho hata iwe tumekuwa katika ukweli muda gani. Ikiwa mtu angefanya maendeleo kufikia mahali anapoonwa kuwa amekomaa, au kufikia tu mahali ambapo anastahili pendeleo fulani la pekee, kungekuwa na faida gani ya kudumu kwake? Kukomaa na mapendeleo ya pekee si uhakikisho kwamba tutafikia mradi wetu wa mwisho​—uzima wa milele. Badala yake, ni lazima tufanye kama alivyofanya mtume Paulo: ‘Kusahau mambo yaliyo nyuma na kujinyoosha kufikia mambo yaliyo mbele.’ (Wafilipi 3:13, NW) Si kwamba tu tunapaswa kuacha nyuma mambo yasiyo ya faida ambayo huenda tukawa tuliyafanya kabla ya kupata maarifa ya ukweli bali pia tunapaswa kuwa waangalifu tusiridhike na yale ambayo tumefanya; tangu wakati huo. Yaani, shauri ni kutotosheka na tuliyokwisha kufanya bali kukaza mwendo mbele bila kuacha. Je! wewe unafanya hivyo, au je, wewe, kwa sababu hii au hii, unapunguza mwendo?​—Ona 1 Wakorintho 9:26.

6. Kwa kulinganisha Wafilipi 3:12 na 3:15, ni mambo gani ambayo yangeweza kusemwa juu ya kufanya maendeleo?

6 Akiwa anafikiria uwezekano huo, Paulo anaendelea kusema: “Acheni, basi, kwa kadiri wengi wetu walivyokomaa, na tuwe wenye huo mwelekeo wa akili; na ikiwa mna maelekeo ya akili tofauti kwa njia yo yote, Mungu atawafunulia mwelekeo huo ulio juu.” (Wafilipi 3:15, NW) Mapema, katika mstari wa 12, Paulo alionyesha kwamba hakujifikiria kuwa ‘amekwisha kuwa mkamilifu.’ Lakini ndipo anaposema “kwa kadiri wengi wetu walivyokomaa,” au, “wakamilifu.” (Union Version) Huko si kupingana. Badala yake, inaonyesha jambo la kwamba hata Wakristo waliokomaa kama Paulo wanapaswa kukumbuka kwamba hawajafikia mradi wa mwisho, na ni lazima waendelee kufanya maendeleo ili waufikie. Ndiyo sababu alimalizia hilo kwa njia hii: “Kwa vyo vyote, kwa kadiri tulivyofanya maendeleo, na tuendelee kutembea kwa utaratibu katika kawaida ii hii.”​—Wafilipi 3:16.

Kawaida ya Utaratibu

7. Paulo alikuwa akiwasihi Wakristo wafuate “kawaida” gani?

7 Paulo alipowatia moyo Wakristo ‘waendelee kutembea kwa utaratibu katika kawaida ii hii,’ je, alikuwa anawaambia wapange kielelezo fulani cha utendaji na kukifuata mpaka wakati wa kupokea thawabu yao ufike? Kufanya hivyo kungekuwa kufanya kama mtumwa wa mfano wa Yesu aliyefukia talanta moja aliyopewa na bwana yake kisha akangoja tu bwana arudi. (Mathayo 25:14-30) Hata ingawa mtumwa huyo hakupoteza talanta yake wala kuacha utumishi wake, yeye aliitwa “mubaya na mulegevu” (ZSB) akakataliwa na bwana yake. Hakika Paulo hakuwa akituambia tushikilie tu tuliyo nayo tusije tukayapoteza. Alikuwa akisema juu ya kufanya maendeleo. Kwa “kawaida” bila shaka Paulo alikuwa akifikiria mwendo wa kusonga mbele uliowekwa, kama askari ambaye hajasimama mahali pamoja wima bali anapiga hatua kwenda mbele.

8. Tunapaswa kujishughulisha na nini kuhusiana na utumishi wa Mungu?

8 Shauri la Paulo linapasa kutusaidia tutambue umaana wa kutia jitihada zenye kuendelea na za bidii ili kusonga mbele, kufanya maendeleo na kujifanya bora katika utumishi wa Yehova. “Kwa kadiri tulivyofanya maendeleo,” tuwe tu wazee, watumishi wa huduma, mapainia, au wahubiri, hangaikio letu kubwa lapasa liwe ni kufanya utumishi wetu uwe bora zaidi, na, ikiwezekana kuongeza wingi wa utumishi wetu. Tunapaswa kuwa waangalifu tusiwe na nia ile ile kama Waisraeli waasi wa siku za Malaki ambao walifikiri si kitu wakitoa dhabihu zisizofaa kwa Yehova. Lakini Yehova alionaje jambo hilo? Alisema, “Nanyi mmeileta [sadaka yenye kilema na ugonjwa].” Halafu akaongeza hivi: “Je! mimi naweza kuikubali mkononi mwenu?”​—Malaki 1:13, NW.

9. Shauri la Paulo katika Warumi 12:6-8, 11 linahusianaje na kufanya maendeleo?

9 Tofauti na hilo, tunapaswa kuuchukua utumishi wetu kwa Mungu kwa uzito. Kama Paulo alivyowakumbusha Waroma, pendeleo lo lote la utumishi tulilopewa, tunapaswa “tuwemo,” “kwa bidii” wala ‘tusiwe walegevu [“wenye kuranda-randa,” NW].’ (Warumi 12:6-8, 11) Kuranda-randa ni kuzubaa-zubaa bila lengo lo lote, bila mwendo wo wote wa kusonga mbele kuelekea mradi fulani wo wote. Tunaagizwa ‘tuwe na juhudi kwa roho’ na ‘kumtumikia Yehova’! Ni nini kinachoweza kutusaidia tufanye hivyo?

10. Ni kwa sababu gani tunapaswa kupendezwa sana na shauri la Paulo kwa Timotheo katika 1 Timotheo 4:12-16?

10 Katika 1 Timotheo 4:12-16 mtume Paulo alieleza kirefu mambo ambayo Timotheo alipaswa kufanya ili maendeleo yake yaweze kuwa “dhahiri kwa watu wote.” Wakati huo, mwanafunzi Timotheo hakuwa kijana wala mpya. Kwa kweli, kufikia wakati huo alikuwa amefanya kazi kwa ukaribu na Paulo kwa miaka zaidi ya kumi na alikuwa amepewa madaraka na mamlaka kubwa katika kundi la Kikristo. Bila shaka alikuwa amepewa hayo kwa sababu ya maendeleo aliyokuwa tayari amekwisha kufanya kufikia hapo. Hata hivyo, Paulo bado alimpa Timotheo mashauri hayo. Kwa wazi, sisi sote tunapaswa kuangalia kwa uangalifu aliyosema Paulo.

Uwe mfano katika usemi na mwenendo

11, 12. (a) Ni sehemu gani ya kwanza tunayopaswa kushughulikia katika kufanya maendeleo? (b) Kwa sababu gani jambo hilo ni la maana zaidi ya kufanya maendeleo katika maarifa au ustadi?

11 Kwanza, katika mstari wa 12, Paulo alisema: “Mtu awaye yote asiudharau ujana wako, bali uwe kielelezo kwao waaminio katika usemi na mwenendo, na katika upendo na imani na usafi.” Orodha hiyo inatukumbusha juu ya “tunda la roho,” ambalo Paulo alieleza kirefu katika Wagalatia 5:22, 23. Ni nani anayeweza kukanusha aseme kwamba kila mmoja wetu hahitaji kuzaa matunda hayo kwa kadiri kubwa zaidi maishani mwetu? Wengi wetu tunatia jitihada kubwa ili tujifunze na kuweza kutaja-taja yale matunda tisa ya roho, na kuwafundisha vijana na wapya wafanye hivyo. Lakini je, tunatia jitihada angalau ya kadiri iyo hiyo ili tuyasitawishe? Paulo alitaja kwamba wale waliokomaa wanapaswa kuwa mfano mwema katika mambo hayo. Hakika, hiyo ni sehemu moja maishani mwetu ambayo sisi sote tunaweza kufanya maendeleo kwa urahisi.

12 Labda, kwa njia moja, sifa hizo zinaonyesha maendeleo yetu ya kiroho zaidi na inavyoonyeshwa na maarifa na ustadi, kwa sababu sifa hizo za kwanza ni mazao ya roho ya Mungu, hali hizi nyingine mara nyingi zinahusiana na karama za kuzaliwa za mtu na elimu. Waandishi na Mafarisayo wa siku za Yesu walijua vizuri Maandiko, nao walikuwa waangalifu sana kushika mambo madogo madogo ya Torati. Lakini, Yesu aliwalaani, akasema: “Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! kwa kuwa mnalipa zaka za mnanaa na bizari na jira, lakini mmeacha mambo makuu ya sheria, yaani, adili, na rehema, na imani.” (Mathayo 23:23) Ni jambo la maana kama nini tuendelee kufanya maendeleo katika kusitawisha hayo “mambo makuu” maishani mwetu!

Kufanya bidii katika kusoma, kuonya, na kufundisha

13. Waangalizi waliowekwa rasmi wanaweza kufaidikaje na shauri la Paulo katika 1 Timotheo 4:13?

13 Halafu, Paulo alimwagiza Timotheo aendelee kufanya “bidii katika kusoma na kuonya na kufundisha.” (1 Timotheo 4:13) Mahali pengine-pengine katika barua zake, Paulo alimsifu sana Timotheo kuwa mhudumu mwenye uwezo na mwaminifu. (Wafilipi 2:20-22; 2 Timotheo 1:4, 5) Lakini bado alimshauri Timotheo aendelee kukazia fikira madaraka hayo ya lazima kwa mwangalizi. Ikiwa wewe ni mwangalizi aliyewekwa rasmi katika kundi, je, wewe unaendelea kufanya “bidii” katika mambo hayo? Kwa mfano, je, wewe unachukua kwa uzito mapendekezo yanayotolewa katika Kiongozi cha Shule ya Huduma ya Kitheokrasi na kufanyia maendeleo upungufu wako, au je, unahisi kwamba mashauri hayo ni ya wapya tu? Je! wewe unajifunza Biblia na vichapo vya Sosaiti kwa uangalifu ili uweze kutia “moyo, kwa ustahimili wote na ustadi wa kufundisha”?​—2 Timotheo 4:2, NW; Tito 1:9.

Usidharau zawadi ya utumishi

14. Tunaweza kuonyeshaje maendeleo katika huduma yetu ya shambani?

14 Ingawa ni wachache peke yao wanaowekwa rasmi wafundishe katika kundi, Wakristo wote wamepewa mgawo na Yesu Kristo washiriki katika kazi ya kutoa ushuhuda wa Ufalme na ya kufanya wanafunzi. (Mathayo 24:14; 28:19, 20) Hiyo inatia ndani kufundisha wenye mioyo minyofu ukweli wa Biblia, kuwatia moyo wafanye mabadiliko maishani mwao na kuchukua msimamo wao upande wa Yehova. Je! wewe unaendelea kutia “bidii” ufanyie maendeleo ustadi wako wa kuwa mhudumu? Je! unadhamiria kutumia mapendekezo yanayotolewa katika Huduma ya Ufalme Yetu na Mkutano wa Utumishi wa kila juma ili ‘ufanye kazi ya mwevanjeli, ukitimiza kwa ukamili huduma yako’?​—2 Timotheo 4:5, NW.

15. “Karama” ya Timotheo ilikuwa nini, na namna gani leo?

15 Hapo mbele, Paulo alikuwa amempa Timotheo kikumbusho hiki: “Usiache kuitumia karama ile iliyomo ndani yako, uliyopewa kwa unabii na kwa kuwekewa mikono ya wazee.” (1 Timotheo 4:14) Inaonekana kwamba kupitia utendaji wa roho takatifu, Timotheo alikuwa amekusudiwa afanye utumishi fulani wa pekee katika kundi la Kikristo na kwa sababu hiyo akawekwa rasmi. (1 Timotheo 1:18; 2 Timotheo 1:6) Hali moja, leo kuna wengi katika tengenezo ambao wamesitawisha uwezo waliopewa na Mungu, na matokeo yakawa kuwekwa rasmi kwao wawe waangalizi wasafirio, wamisionari, mapainia wa kawaida au wa pekee, wazee, na kadhalika. Ingawa hakuna utabiri wa kipekee au kuwekelewa mikono kunakohusika, shauri hili “usiache kuitumia karama ile iliyomo ndani yako” linahusika kwa mkazo ule ule.

16. Ni nini kinachoweza kutuzuia tusidharau “karama” yetu?

16 Kulingana na kamusi, kudharau kitu kunamaanisha kukikazia fikira chache au kukiacha ovyo-ovyo kikiwa hakijakamilishwa. Kitu kinapoonwa kuwa cha kawaida tu, ni rahisi kukidharau. Jambo hilo linaweza kutokea tukiacha kufanya maendeleo, au kusonga mbele, na kuichukua migawo yetu kuwa jambo la vivi hivi tu. Kwa hiyo, tunaweza kufaidika na aliyosema Paulo katika Wakolosai 3:23, 24: “Lo lote mfanyalo, lifanyeni kwa moyo, kama kwa [Yehova], wala si kwa wanadamu, mkijua ya kuwa mtapokea kwa [Yehova] ujira wa urithi. Mnamtumikia Bwana Kristo.”

Jitihada Yenye Kuendelea Inaleta Baraka

17. Ni kwa jinsi gani tu tutaona matokeo ya jitihada zetu?

17 Tukikazia fikira za uangalifu mambo yaliyozungumzwa juu, tunaweza kuwa na uhakika kwamba hatutaanguka katika mtego wa kuchukua mambo vivi hivi au kuridhika na tulivyo. “Uyatafakari hayo; ukae katika hayo; ili kuendelea kwako kuwe dhahiri kwa watu wote,” alisema Paulo. (1 Timotheo 4:15) Bila shaka “kuendelea” huko si kwa kusudi la kujionyesha au kuvutia wengine. Wakati sisi, vijana na wazee, tunapokua na kusitawi kiroho, tunawaletea furaha na kitia moyo wote wanaoshirikiana na sisi, kama vile Alisa mchanga na rafikiye, waliotajwa mapema katika makala hii.

18. Ni baraka gani maradufu zilizo mbele yetu tukifuata shauri la Paulo kwa bidii?

18 Baraka maradufu ziko mbele yetu tukifuata shauri la Paulo kwa bidii. “Jitunze nafsi yako, na mafundisho yako,” alisema Paulo. “Dumu katika mambo hayo; maana kwa kufanya hivyo utajiokoa nafsi yako na wale wakusikiao pia.” (1 Timotheo 4:16) Ndiyo, kwa kujichunguza wenyewe daima juu ya kama tunafanya yale tunayofundisha wengine wafanye, yaani, kufanya maendeleo, kukua, na kusitawisha hali ya kiroho, tutaepuka msiba wa ‘kukataliwa kwa njia fulani.’ (1 Wakorintho 9:27, NW) Badala yake, sisi na wale pia tulio na pendeleo lenye furaha la kuwasaidia, tumehakikishiwa taraja lenye furaha la uzima katika Utaratibu Mpya wa Mungu ulioahidiwa. Kwa hiyo, ili iwe baraka yetu na baraka ya wengine, na ili iwe sifa kwa Yehova Mungu: ‘Endeleeni kutembea kwa utaratibu katika kawaida ii hii’!—Wafilipi 3:16, NW.

Je! Unakumbuka?

◻ “Mradi” wa mwisho tunaopaswa kuwa nao akilini ni nini? Ni jinsi gani tunaweza kuufuatia? (Wafilipi 3:12, 13)

◻ Ni “kawaida” gani ambayo tunapaswa kutembea ndani yake? (Wafilipi 3:16)

◻ Ni kwa sababu gani tunapaswa kuzidi kufanya maendeleo katika mwenendo na usemi wa Kikristo? (1 Timotheo 4:12)

◻ Wazee, watumishi wa huduma, na wengine wanaweza kufanyaje maendeleo katika ustadi wao wa kufundisha? (1 Timotheo 4:13)

◻ Tunapaswa kufanya nini ili tusidharau “karama” tuliyopewa iwe amana? (1 Timotheo 4:14)

[Picha katika ukurasa wa 28]

Alisa na mwanafunzi wake wa Biblia wana mradi wa huduma ya wakati wote

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki