“Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu
1. Tutajifunza kitabu gani katika Funzo la Biblia la Kutaniko kuanzia juma la Machi 14?
1 Kuanzia juma la Machi 14, 2011, tutaanza kujifunza kitabu “Kutoa Ushahidi Kamili” Kuhusu Ufalme wa Mungu, katika Funzo la Biblia la Kutaniko. Kitabu hiki kinazungumzia kitabu cha Matendo kwa njia inayomsaidia msomaji kuwazia akilini mfululizo wa matukio yaliyoandikwa katika kitabu cha Matendo. Badala ya kuchanganua kitabu cha Matendo mstari kwa mstari, kitabu Kutoa Ushahidi kina mafundisho yanayotegemea kitabu cha Matendo na kinatusaidia kuona jinsi tunavyoweza kutumia mafundisho hayo kibinafsi.—Rom. 15:4.
2. Eleza baadhi ya mambo yaliyo katika kitabu Kutoa Ushahidi.
2 Yaliyomo: Utangulizi ulio katika ukurasa wa 2 ni barua yenye kutia moyo sana kutoka kwa Baraza Linaloongoza inayoonyesha jinsi wanavyotaka tunufaike kutokana na kitabu hicho. Kuanzia sura ya 2, kuna maelezo mafupi yanayoonyesha mambo ambayo yanazungumziwa katika kila sura na mistari ya kitabu cha Matendo inayozungumziwa. Sura nyingi zina masanduku yaliyo na habari zaidi kuhusu watu, mahali, au matukio. Pambizoni kuna nafasi ya kuandika mambo muhimu. Kitabu hiki kina picha zinazoonyesha kinaganaga mandhari za Biblia. Picha hizo zinatusaidia kupiga picha akilini matukio muhimu, na katika ukurasa wa mwisho kuna fahirisi ya picha inayoeleza mambo yanayozungumziwa katika picha mbalimbali. Upande wa ndani wa jalada la mbele na la nyuma kuna ramani zinazotusaidia kuona maeneo ambayo waabudu wenzetu wa karne ya kwanza walitembelea walipokuwa wakieneza habari njema “mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.”—Mdo. 1:8.
3. Kujifunza kitabu cha Matendo kutatusaidia kupata majibu ya maswali gani muhimu?
3 Majibu ya Maswali Muhimu: Kujifunza kitabu cha Matendo kutatusaidia kufahamu kabisa majibu ya maswali muhimu kuhusu huduma ya Kikristo. Kwa mfano, ni kazi na ujumbe gani unaowatambulisha wafuasi wa kweli wa Yesu Kristo? Ni nani anayeongoza kazi hii ya kuhubiri ulimwenguni pote, na anafanyaje hivyo? Wahudumu hupata fursa zipi wanapokabili mateso na upinzani? Roho takatifu ina fungu gani katika huduma yetu?
4. Tunaweza kunufaikaje kikamili kwa kujifunza kitabu hiki?
4 Ili ufaidike kikamili, soma habari hiyo mapema, na ujitayarishe kushiriki wakati wa funzo kutanikoni. Hudhuria mikutano yote, na uonyeshe jinsi unavyoweza kutumia habari unazojifunza katika huduma yako. Acheni kujifunza kitabu hiki chenye kusisimua kutuchochee kutoa ushahidi kamili kuhusu Ufalme wa Mungu!—Mdo. 28:23.