Tumia Sehemu Mbalimbali za Kitabu Biblia Inafundisha kwa Ustadi
Kadiri mwanafunzi wa Biblia anavyojifunza mambo ambayo Biblia inafundisha hasa na kuyatumia maishani, atakua na kutokeza matunda ya kiroho. (Zab. 1:1-3) Tunaweza kumsaidia mwanafunzi wa Biblia afanye maendeleo ikiwa tutatumia kwa ustadi sehemu mbalimbali za kitabu Biblia Inafundisha.
Maswali ya Utangulizi: Mwanzoni mwa kila sura kuna maswali yanayojibiwa katika sura hiyo. Unaweza kuuliza maswali hayo bila kutazamia majibu ili kuamsha upendezi wa mwanafunzi kwa mazungumzo yatakayofuata. Au unaweza kumwomba aeleze maoni yake kifupi kwa kila swali. Ikiwa ataeleza jambo ambalo si sahihi, hakuna haja ya kumrekebisha wakati huo. Maelezo yake yatakusaidia kutambua mambo unayohitaji kukazia.—Met. 16: 23; 18:13.
Nyongeza: Ikiwa mwanafunzi anaelewa na anakubaliana na habari mnayozungumzia, unaweza kumtia moyo asome kwa wakati wake habari inayozungumzia jambo hilo kwa kina katika nyongeza. Katika funzo linalofuata, unaweza kutumia dakika chache kuhakikisha ikiwa ameelewa. Hata hivyo, ikiwa kuna uhitaji, zungumzia habari zilizo kwenye nyongeza au sehemu ya habari hizo kwa kusoma mafungu na kuuliza maswali ambayo ulitayarisha mapema.
Sanduku la Pitio: Sanduku la pitio lililo mwishoni mwa kila sura lina maelezo ambayo yanajibu maswali yaliyo mwanzoni mwa kila sura. Unaweza kutumia sehemu hiyo kuhakikisha kwamba mwanafunzi anaelewa na anaweza kueleza mambo makuu. Someni pamoja kwa sauti kila sentensi na maandiko yaliyo katika sentensi hiyo. Kisha mwombe mwanafunzi athibitishe maelezo hayo kwa kutumia andiko au maandiko yaliyo katika sentensi hiyo.—Mdo. 17:2, 3.