MAISHA YA MKRISTO
Jaribu Kuelewa Maoni ya Mungu
Tunataka kumfurahisha Yehova katika mambo yote tunayofanya. (Met 27:11) Ili tufanye hivyo, tunahitaji kufanya maamuzi yanayopatana na maoni yake hata ikiwa hakuna sheria au amri hususa ya kutuongoza. Ni nini kinachoweza kutusaidia kufanya hivyo?
Dumisha ratiba nzuri ya kujifunza Biblia. Kila mara tunaposoma Biblia, ni kana kwamba tunatumia wakati pamoja na Yehova. Tunaweza kujifunza njia ya Yehova ya kufikiri kwa kuchunguza jinsi alivyoshughulika na watu wake na kwa kuchunguza mifano ya wale waliotenda mema au mabaya machoni pake. Tunapohitaji kufanya uamuzi, roho takatifu inaweza kutusaidia kukumbuka masomo na kanuni muhimu ambazo tumejifunza katika Neno la Mungu.—Yoh 14:26.
Fanya utafiti. Unapohitaji kufanya uamuzi, jiulize, ‘Ni mistari au masimulizi gani katika Biblia yanayoweza kunisaidia kuelewa jinsi Yehova anavyohisi kuhusu jambo hili?’ Sali upate msaada wa Yehova, na utumie vifaa vya utafiti vya kitheokrasi vinavyopatikana katika lugha yako ili upate na kutumia kanuni za Biblia zinazopatana na hali yako.—Zb 25:4.
TAZAMENI VIDEO YENYE KICHWA LAZIMA “TUKIMBIE KWA UVUMILIVU”—KULA CHAKULA CHENYE LISHE, KISHA MJIBU MASWALI YAFUATAYO:
Dada katika video hiyo alishinikizwa kwa njia gani mbalimbali?
Unaweza kutumiaje vifaa vya utafiti kupata msaada unaposhinikizwa kwa njia mbalimbali kama hizo?
Tunanufaikaje tunapotumia wakati kufanya utafiti na pia funzo la kibinafsi linaloweza kutusaidia kufanya maamuzi mazuri?—Ebr 5:13, 14