MAKALA YA 12
Ni Wakati Gani Unaofaa Kuongea?
“Kuna . . . wakati wa kunyamaza na wakati wa kuongea.” —MHU. 3:1, 7.
WIMBO 124 Washikamanifu Sikuzote
MUHTASARIa
1. Andiko la Mhubiri 3:1, 7 linatufundisha nini?
BAADHI yetu tunapenda kuongea sana. Wengine ni wakimya sana. Kama andiko la msingi la makala hii linavyoonyesha, kuna wakati wa kuongea na pia wakati wa kunyamaza. (Soma Mhubiri 3:1, 7.) Ingawa hivyo, huenda tukatamani baadhi ya ndugu na dada zetu wawe wazungumzaji zaidi na wengine wasizungumze sana.
2. Ni nani aliye na haki ya kutuwekea viwango kuhusu wakati wa kuongea na jinsi tunavyopaswa kuongea?
2 Uwezo wa kuongea ni zawadi kutoka kwa Yehova. (Kut. 4:10, 11; Ufu. 4:11) Katika Neno lake, Yehova anatusaidia kujua jinsi tunavyoweza kutumia zawadi hiyo vizuri. Katika makala hii, tutazungumzia mifano ya Biblia itakayotusaidia kujua wakati wa kuongea na wakati wa kunyamaza. Pia, tutaona jinsi Yehova anavyohisi kuhusu mambo tunayowaambia wengine. Kwanza, acheni tuzungumzie kuhusu wakati tunaopaswa kuongea.
TUNAPASWA KUONGEA WAKATI GANI?
3. Kulingana na Waroma 10:14, ni wakati gani tunaopaswa kuongea?
3 Sikuzote tunapaswa kuwa tayari kuzungumza kumhusu Yehova na Ufalme wake. (Mt. 24:14; soma Waroma 10:14.) Tunapofanya hivyo tunamwiga Yesu. Mojawapo ya sababu kuu iliyomfanya Yesu aje duniani ilikuwa kuwaambia wengine ukweli kumhusu Baba yake. (Yoh. 18:37) Lakini ni lazima tukumbuke pia kwamba jinsi tunavyozungumza ni jambo linalopaswa kuchukuliwa kwa uzito. Hivyo, tunapozungumza na wengine kumhusu Yehova, ni lazima tufanye hivyo kwa “upole na heshima kubwa,” na tunapaswa kujali hisia za wengine na mambo wanayoamini. (1 Pet. 3:15) Kwa kufanya hivyo, tutatimiza mengi zaidi ya kuzungumza tu; tutafundisha na huenda hata tutagusa moyo wa tunayezungumza naye.
4. Kulingana na Methali 9:9, maneno yetu yanaweza kuwanufaishaje wengine?
4 Wazee wa kutaniko hawapaswi kusita kuongea wanapoona kwamba ndugu au dada anahitaji shauri. Bila shaka, watachagua wakati unaofaa wa kuongea naye ili wasimwaibishe. Huenda wakaamua kusubiri hadi watakapopata muda wa kuongea naye faraghani. Sikuzote wazee hujitahidi kuongea kwa njia ambayo haitamvunjia heshima yule wanayezungumza naye. Lakini bado hawataepuka kuwaonyesha wengine kanuni za Biblia zinazoweza kuwasaidia watende kwa hekima. (Soma Methali 9:9.) Kwa nini ni muhimu sana kwamba tuwe na ujasiri wa kuongea inapohitajika? Fikiria mifano miwili inayotofautiana. Katika kisa kimoja mwanamume fulani alihitaji kuwarekebisha wanawe na katika kisa kingine mwanamke fulani alihitaji kumjulisha mfalme mtarajiwa kuhusu uamuzi mbaya aliofanya.
5. Ni wakati gani ambao Kuhani Mkuu Eli alipaswa kuongea lakini hakufanya hivyo?
5 Kuhani Mkuu Eli alikuwa na wana wawili aliowapenda sana. Lakini, wana hao hawakumheshimu Yehova. Walikuwa na jukumu muhimu la kutumikia wakiwa makuhani katika hema la ibada. Lakini walitumia vibaya mamlaka yao, wakadharau sana dhabihu zilizotolewa kwa Yehova, na kufanya uasherati bila aibu. (1 Sam. 2:12-17, 22) Kulingana na Sheria ya Musa, wana wa Eli walistahili kufa, lakini Eli aliwaendekeza, akawakaripia kijuu-juu tu na kuwaruhusu waendelee kutumikia katika hema la ibada. (Kum. 21:18-21) Yehova alihisije kuhusu jinsi Eli alivyoshughulikia mambo? Alimwambia Eli hivi: “Kwa nini unaendelea kuwaheshimu wana wako kuliko mimi?” Kisha Yehova akaamua kuwaua wanaume hao wawili waovu.—1 Sam. 2:29, 34.
6. Tunajifunza nini kutoka kwa Eli?
6 Tunajifunza somo muhimu kutoka kwa Eli. Tukigundua kwamba rafiki au mtu wa ukoo amevunja sheria ya Mungu, tunapaswa kumweleza na kumkumbusha viwango vya Yehova. Kisha lazima tuhakikishe kwamba anapata msaada anaohitaji kutoka kwa wawakilishi wa Yehova. (Yak. 5:14) Hatungependa kamwe kuwa kama Eli kwa kumheshimu rafiki au mtu wa ukoo zaidi ya tunavyomheshimu Yehova. Tunahitaji ujasiri ili kumshauri mtu anayehitaji kurekebishwa, lakini jitihada hizo si za bure. Ona tofauti iliyopo kati ya mfano wa Eli na ule wa mwanamke Mwisraeli aliyeitwa Abigaili.
Abigaili alituwekea mfano mzuri wa kuchagua wakati unaofaa wa kuongea (Tazama fungu la 7 na 8)d
7. Kwa nini Abigaili alizungumza na Daudi?
7 Abigaili alikuwa mke wa Nabali, mwanamume tajiri aliyemiliki ardhi. Daudi na wanaume wake walipokuwa wakimkimbia Mfalme Sauli, walikaa kwa muda fulani pamoja na wachungaji wa Nabali na walilinda mifugo ya Nabali ili isishambuliwe na vikosi vya wavamizi. Je, Nabali alithamini msaada wao? Hapana. Daudi alipomwomba Nabali awaandalie wanaume wake chakula na maji, Nabali alikasirika na kuwatukana. (1 Sam. 25:5-8, 10-12, 14) Hivyo, Daudi aliamua kwamba angemuua kila mwanamume wa nyumba ya Nabali. (1 Sam. 25:13, 22) Msiba huo ungeweza kuepukwaje? Abigaili alitambua kwamba huo ulikuwa wakati wa kuongea, hivyo kwa ujasiri alienda kukutana na wanaume 400 waliojihami kwa silaha na waliokuwa na njaa na hasira ili azungumze na Daudi.
8. Tunajifunza nini kutokana na mfano wa Abigaili?
8 Abigaili alipokutana na Daudi aliongea kwa ujasiri, kwa heshima, na kwa ushawishi. Ingawa Abigaili hakupaswa kulaumiwa kwa sababu ya hali hiyo mbaya, alimwomba Daudi msamaha. Abigaili alijua kwamba Daudi alikuwa mtu mzuri na angetenda kwa njia inayofaa; pia Abigaili alimtegemea Yehova ili amsaidie. (1 Sam. 25:24, 26, 28, 33, 34) Kama Abigaili, tunahitaji kuwa na ujasiri wa kuzungumza tunapoona mtu ameanza kufuata njia iliyo hatari. (Zab. 141:5) Ni lazima tuzungumze naye kwa heshima, lakini pia ni lazima tuwe jasiri. Tunapompa mtu kwa upendo shauri analohitaji, tunathibitisha kwamba sisi ni marafiki wa kweli.—Met. 27:17.
9-10. Wazee wanapaswa kukumbuka nini wanapowashauri wengine?
9 Kihususa, ni lazima wazee wawe na ujasiri wa kuzungumza na wale ambao wamechukua hatua isiyofaa kutanikoni. (Gal. 6:1) Kwa unyenyekevu, wazee hutambua kwamba wao pia si wakamilifu na huenda siku moja wakahitaji shauri. Lakini wazee hawaruhusu jambo hilo liwazuie kuwakaripia wale wanaohitaji nidhamu. (2 Tim. 4:2; Tito 1:9) Wanapomshauri mtu, wanajitahidi kutumia zawadi yao ya usemi ili kumfundisha kwa ustadi na kwa subira. Wanawapenda ndugu zao, na upendo huo huwachochea kuwasaidia. (Met. 13:24) Lakini jambo kuu wanalohangaikia ni kumheshimu Yehova kwa kutetea viwango vyake na kulilinda kutaniko ili lisiathiriwe.—Mdo. 20:28.
10 Kufikia sasa tumezungumza kuhusu wakati tunaopaswa kuongea. Hata hivyo, kuna nyakati ambazo hatupaswi kamwe kuongea chochote. Huenda tukakabili changamoto gani nyakati kama hizo?
TUNAPASWA KUNYAMAZA WAKATI GANI?
11. Yakobo alitumia mfano gani, na kwa nini unafaa?
11 Inaweza kuwa vigumu kwetu kudhibiti maneno yetu. Mwandikaji wa Biblia Yakobo alitumia mfano mzuri unaofafanua changamoto hiyo. Alisema hivi: “Ikiwa yeyote hajikwai katika neno, huyo ni mtu mkamilifu, anayeweza kuuongoza kwa lijamu mwili wake wote pia.” (Yak. 3:2, 3) Lijamu huwekwa kichwani na kiasi fulani huwekwa ndani ya kinywa cha farasi. Kwa kuvuta kamba mpanda-farasi anaweza kumwongoza farasi au kumfanya asimame. Mpanda-farasi akishindwa kushikilia kamba hizo vizuri, farasi anaweza kukimbia kwa fujo na kujiumiza au kumuumiza mpandaji. Vivyo hivyo, tukishindwa kudhibiti maneno yetu, tunaweza kusababisha madhara makubwa. Acheni tuzungumzie baadhi ya nyakati ambazo tunahitaji “kuvuta kamba” kwa njia ya mfano na kujizuia kuzungumza.
12. Tunapaswa “kuvuta kamba” wakati gani ili kujizuia kuzungumza?
12 Wewe hutendaje ndugu au dada anapokuwa na habari ambazo zinapaswa kuwa siri? Kwa mfano, unapokutana na ndugu anayeishi katika nchi ambayo kazi yetu imepigwa marufuku, je, unashawishika kumuuliza kuhusu jinsi kazi yetu inavyofanywa katika nchi hiyo? Bila shaka una nia nzuri. Tunawapenda ndugu zetu na tunahangaikia hali wanayopitia. Pia, tunataka kusali kihususa kuhusu hali wanazokabili. Hata hivyo, huo ndio wakati tunaopaswa “kuvuta kamba” na kujizuia kuzungumza. Tukimshinikiza ndugu yetu atueleze habari za siri, tunakosa kumwonyesha upendo yeye pamoja na ndugu na dada wanaotegemea kwamba hatafunua habari kuhusu utendaji wao. Kwa kweli, hakuna yeyote kati yetu ambaye angependa kuwaongezea matatizo ndugu na dada zetu wanaoishi katika nchi ambazo kazi yetu imepigwa marufuku. Vivyo hivyo, hakuna ndugu au dada yeyote anayetumikia katika nchi hizo ambaye angependa kufunua habari kuhusu jinsi Mashahidi wanaoishi huko wanavyoendeleza huduma yao au utendaji wao wa Kikristo.
13. Kama inavyotajwa kwenye Methali 11:13, ni lazima wazee wafanye nini, na kwa nini?
13 Kihususa, ni lazima wazee watumie kanuni ya andiko la Methali 11:13 kwa kutunza habari za siri. (Soma.) Jambo hilo linaweza kuwa changamoto hasa ikiwa mzee wa kutaniko ameoa. Wenzi wa ndoa huimarisha uhusiano wao kwa kuzungumza pamoja kwa ukawaida na kufunua fikira na hisia zao za ndani kabisa na pia mambo yanayowahangaisha. Lakini mzee anatambua kwamba hapaswi kufunua “mazungumzo ya siri” ya wengine kutanikoni. Ikiwa atafunua siri zao, ndugu na dada hawatamtumaini na jambo hilo litaharibu sifa yake. Wale waliowekwa rasmi kusimamia kutaniko hawapaswi kuwa “wenye ndimi mbili,” au wasiosema kwa unyoofu. (1 Tim. 3:8; maelezo ya chini) Yaani, hawapaswi kuwa wenye hila au wenye kupenda kupiga porojo. Ikiwa mzee anampenda mke wake, hatamlemea kwa kumtwika mzigo wa habari ambazo hahitaji kujua.
14. Mke wa mzee wa kutaniko anaweza kumsaidiaje mume wake adumishe sifa nzuri?
14 Mke anaweza kumsaidia mume wake adumishe sifa nzuri kwa kutomshinikiza kuzungumzia habari ambazo zinapaswa kuwa siri. Mke anapotumia ushauri huo, hamuungi tu mkono mume wake bali pia anawaheshimu wale ambao wamemweleza mume wake mambo yao ya siri. Na jambo muhimu hata zaidi ni kwamba anamfurahisha Yehova kwa sababu anachangia amani na umoja kutanikoni.—Rom. 14:19.
YEHOVA ANAHISIJE KUHUSU MAMBO TUNAYOSEMA?
15. Yehova alihisije kuhusu marafiki watatu wa Ayubu, na kwa nini?
15 Tunaweza kujifunza mengi katika kitabu cha Ayubu kuhusu jinsi ya kuzungumza na wakati wa kuzungumza. Baada ya Ayubu kukumbwa na mfululizo wa misiba yenye kuhuzunisha, wanaume wanne walienda kumfariji na kumshauri. Wanaume hao walikaa kimya kwa muda mrefu. Lakini maneno yaliyosemwa baadaye na wanaume hawa watatu, yaani, Elifazi, Bildadi, na Sofari, yanaonyesha wazi kwamba hawakutumia kipindi hicho kutafakari jinsi ambavyo wangemsaidia Ayubu. Badala yake, walikuwa wakifikiria kuhusu jinsi ambavyo wangethibitisha kwamba Ayubu alikuwa amefanya jambo fulani baya. Mambo fulani waliyosema yalikuwa sahihi, lakini mambo mengi waliyosema kumhusu Ayubu na Yehova hayakuwa yenye fadhili au ya kweli. Walimhukumu Ayubu kwa ukali. (Ayu. 32:1-3) Yehova alitendaje? Hasira yake iliwaka dhidi ya wanaume hao watatu. Aliwaita wanaume hao wapumbavu na akawaambia wamwombe Ayubu asali kwa ajili yao.—Ayu. 42:7-9.
16. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano mbaya wa Elifazi, Bildadi, na Sofari?
16 Tunajifunza mambo kadhaa kutokana na mfano mbaya wa Elifazi, Bildadi, na Sofari. Kwanza, hatupaswi kuwahukumu ndugu zetu. (Mt. 7:1-5) Badala yake, tunapaswa kuwasikiliza kwa makini kabla ya kuzungumza. Tukifanya hivyo, ndipo tu tutakapoweza kuelewa hali zao. (1 Pet. 3:8) Pili, tunapozungumza ni lazima tuhakikishe kwamba maneno yetu ni yenye fadhili na mambo tunayosema ni sahihi. (Efe. 4:25) Na tatu, Yehova anachukulia kwa uzito mambo tunayowaambia wengine.
17. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Elihu?
17 Mwanamume wa nne aliyemtembelea Ayubu ni Elihu, mtu wa ukoo wa Abrahamu. Alikuwa akisikiliza wakati Ayubu na wale wanaume wengine watatu walipozungumza. Ni wazi alisikiliza kwa makini mambo waliyosema kwa sababu alimpa Ayubu shauri la moja kwa moja na lenye fadhili lililomsaidia arekebishe njia yake ya kufikiri. (Ayu. 33:1, 6, 17) Jambo kuu ambalo Elihu alihangaikia lilikuwa kumtukuza Yehova, wala si kujitukuza mwenyewe au mwanadamu mwingine. (Ayu. 32:21, 22; 37:23, 24) Mfano wa Elihu unatufunza kwamba kuna wakati wa kunyamaza na kusikiliza. (Yak. 1:19) Pia, tunajifunza kwamba tunapowashauri wengine lengo letu kuu linapaswa kuwa kumletea Yehova heshima, wala si kujitukuza wenyewe.
18. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunathamini zawadi ya usemi?
18 Tunaweza kuonyesha kwamba tunathamini zawadi ya usemi kwa kufuata ushauri wa Biblia kuhusu wakati wa kuongea na jinsi ya kuongea. Mfalme Sulemani mwenye hekima aliongozwa na roho takatifu kuandika hivi: “Kama matofaa ya dhahabu yaliyonakshiwa kwenye vyombo vya fedha ndivyo lilivyo neno linalosemwa wakati unaofaa.” (Met. 25:11) Tunapowasikiliza wengine kwa makini na kutafakari kabla ya kuongea, maneno yetu yatakuwa kama matofaa hayo ya dhahabu—yatakuwa yenye thamani na yenye kupendeza. Kisha, iwe sisi ni wazungumzaji au la, maneno yetu yatawajenga wengine, na Yehova atatuonea fahari. (Met. 23:15; Efe. 4:29) Kwa kweli, hakuna njia nyingine bora zaidi ya kuonyesha kwamba tunathamini zawadi hiyo kutoka kwa Mungu!
WIMBO 82 “Acheni Nuru Yenu Iangaze”
a Neno la Mungu lina kanuni zinazoweza kutusaidia kujua wakati wa kuongea na wakati wa kunyamaza. Tunapojua na kufuata mambo ambayo Biblia inasema, maneno yetu yatampendeza Yehova.
b MAELEZO YA PICHA: Dada anaona uhitaji wa kutoa ushauri wenye hekima.
c MAELEZO YA PICHA: Ndugu akitoa mapendekezo kuhusu usafi.
d MAELEZO YA PICHA: Kwa wakati unaofaa, Abigaili alimsihi Daudi, na matokeo yakawa mazuri.
e MAELEZO YA PICHA: Wenzi wa ndoa wanajizuia kufunua habari kuhusu kazi yetu katika eneo ambalo imepigwa marufuku.
f MAELEZO YA PICHA: Mzee anajihadhari ili jambo fulani la siri kuhusu kutaniko lisisikiwe na mtu mwingine yeyote.