Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w21 Septemba kur. 26-31
  • Mpendwa Wako Anapomwacha Yehova

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mpendwa Wako Anapomwacha Yehova
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2021
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • EPUKA KUJILAUMU
  • MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA ILI UENDELEE KUWA NA NGUVU KIROHO
  • KUTANIKO LINAWEZA KUSAIDIA
  • USIKATE TAMAA NA ENDELEA KUMTUMAINI YEHOVA
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Jinsi ya Kushughulika na Mtu Aliyetengwa na Ushirika
    “Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu”
  • Kutenga na Ushirika Ni Mpango Wenye Upendo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2015
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2021
w21 Septemba kur. 26-31

MAKALA YA 39

Mpendwa Wako Anapomwacha Yehova

“Jinsi walivyomwasi mara nyingi . . . na kumtia uchungu.”​—ZAB. 78:40.

WIMBO 102 “Mwasaidie Walio Dhaifu”

MUHTASARIa

1. Mtu anaweza kuhisije mpendwa wake anapotengwa na ushirika?

JE, MPENDWA wako ametengwa na ushirika? Jambo hilo linaweza kuvunja moyo sana! Dada anayeitwa Hilda, anasema hivi: “Mwenzi wangu mwaminifu alipokufa baada ya miaka 41 ya ndoa, nilifikiri kwamba hilo lilikuwa jambo baya zaidi ambalo ningewahi kupitia maishani.b Lakini mwana wangu alipoliacha kutaniko, mke wake, na watoto wake, jambo hilo liliniumiza hata zaidi.”

Baba akiondoka nyumbani na sanduku lake la nguo. Mama amewakumbatia watoto wake wawili wanaolia.

Yehova anaelewa maumivu makali tunayopata mpendwa wetu anapoacha kumtumikia (Tazama fungu la 2 na 3)d

2-3. Kulingana na Zaburi 78:40, 41, Yehova anahisije watumishi wake wanapomwacha?

2 Fikiria jinsi Yehova alivyohuzunika moyoni wakati baadhi ya malaika waliokuwa sehemu ya familia yake walipomwasi! (Yuda 6) Na wazia uchungu aliohisi alipowaona Waisraeli, watu wake aliowapenda, wakimwasi tena na tena. (Soma Zaburi 78:40, 41.) Uwe na hakika kwamba Baba yetu wa mbinguni anayetupenda anahisi pia uchungu wakati mtu unayempenda anapomwacha. Anaelewa huzuni unayopitia. Kwa huruma, atakuandalia kitia moyo na utegemezo unaohitaji.

3 Katika makala hii, tutazungumzia mambo tunayoweza kufanya ili kupata msaada wa Yehova wakati mtu tunayempenda anapomwacha. Pia, tutachunguza jinsi tunavyoweza kuwasaidia wengine kutanikoni ambao wanapitia changamoto hiyo. Lakini kwanza, acheni tuzungumzie njia isiyofaa ya kufikiri ambayo ni lazima tuepuke.

EPUKA KUJILAUMU

4. Wazazi wengi wanahisije mwana au binti yao anapomwacha Yehova?

4 Mwana au binti yao mpendwa anapomwacha Yehova, ni jambo la kawaida kwa wazazi kufikiria ikiwa kuna jambo la ziada ambalo wangeweza kufanya ili kumsaidia mtoto wao abaki katika kweli. Ndugu anayeitwa Luke, alikiri hivi baada ya mwana wake kutengwa na ushirika: “Nilijilaumu. Nilikuwa nikiota ndoto mbaya kuhusu jambo hilo. Nyakati nyingine ningelia na moyo wangu ulikuwa na uchungu mwingi.” Elizabeth, dada aliyepitia hali inayofanana na hiyo, alisema hivi kwa uchungu: “Nikiwa mama nilikosea wapi? Nilihisi kwamba sikufaulu kukazia kweli moyoni mwa mwana wangu.”

5. Ni nani anayebeba lawama mtu anapomwacha Yehova?

5 Tunapaswa kukumbuka kwamba Yehova amempatia kila mmoja wetu zawadi ya uhuru wa kuchagua. Hilo linamaanisha kwamba tunaweza kuchagua ikiwa tutamtii yeye au la. Baadhi ya watoto wamelelewa na wazazi ambao hawakuwa mfano mzuri, lakini walichagua kumtumikia Yehova, na wanaendelea kuwa waaminifu kwake. Wengine ambao wazazi wao walifanya yote waliyoweza ili kuwalea kupatana na kanuni za Kimaandiko, baadaye waliiacha kweli. Mwishowe, ni lazima kila mmoja wetu aamue kibinafsi ikiwa atamtumikia Yehova. (Yos. 24:15) Hivyo, enyi wazazi mnaohuzunika, epukeni mwelekeo wa kufikiri kwamba mnalaumika kwa kilichotokea!

6. Huenda kijana akaathiriwaje mzazi wake anapomwacha Mungu?

6 Nyakati nyingine, mzazi anaiacha kweli na hata familia yake. (Zab. 27:10) Jambo hilo linaweza kuwaumiza sana watoto ambao walimheshimu mzazi wao na kufuata kielelezo chake. Esther, ambaye baba yake alitengwa na ushirika anasema hivi: “Nililia mara nyingi kwa sababu nilitambua kwamba baba hakuwa akipeperushwa tu kutoka kwenye kweli. Alikuwa akichagua kimakusudi kumwacha Yehova kabisa. Ninampenda baba yangu, hivyo alipotengwa na ushirika mara nyingi nilikuwa na wasiwasi kuhusu hali yake. Hata nilianza kupata mishtuko ya ghafla kwa sababu ya hofu.”

7. Yehova anahisije kuhusu kijana ambaye mzazi wake ametengwa na ushirika?

7 Enyi vijana, ikiwa mmoja wa wazazi wenu ametengwa na ushirika, mioyo yetu inaumia pamoja nanyi! Tafadhali muwe pia na hakika kwamba Yehova anaelewa vizuri maumivu yenu. Anawapenda na anathamini ushikamanifu wenu, na sisi ndugu na dada zenu tunahisi vivyo hivyo. Pia, kumbuka kwamba wewe si wa kulaumiwa kwa maamuzi ya mzazi wako. Kama ilivyotajwa awali, Yehova amempa kila mwanadamu uhuru wa kuchagua. Na ni lazima kila mtu aliyejiweka wakfu na kubatizwa ‘aubebe mzigo wake mwenyewe wa wajibu.’​—Gal. 6:5, maelezo ya chini.

8. Washiriki wa familia walio waaminifu wanaweza kufanya nini wanaposubiri mpendwa wao amrudie Yehova? (Tazama pia sanduku “Mrudie Yehova.”)

8 Mtu unayempenda anapomwacha Yehova, inaeleweka kwamba unakuwa na tumaini kuwa siku moja atamrudia. Unaweza kufanya nini kwa sasa? Unaweza kutunza afya yako ya kiroho. Kwa kufanya hivyo, utawawekea mfano mzuri washiriki wengine wa familia na labda hata aliyetengwa na ushirika. Pia, utapata nguvu unazohitaji ili kukabiliana na maumivu yako ya kihisia. Acheni tuzungumzie baadhi ya hatua hususa unazoweza kuchukua.

Mrudie Yehova

Kwa upendo mchungaji amembeba mwanakondoo kifuani pake.

Mama mmoja anasema hivi: “Tumaini langu kwa mwana wangu aliyetengwa na ushirika linaelezwa vizuri katika maneno ya Isaya 55:7: ‘Na arudi kwa Yehova, ambaye atamwonyesha rehema, kwa Mungu wetu, kwa maana atasamehe kwa njia kubwa.’” Ikiwa umemwacha Yehova, kadiri utakavyomrudia haraka, ndivyo utakavyokuwa na furaha zaidi. Unapotazama matukio ya ulimwengu, unaona wazi kwamba Har–Magedoni inakaribia kwa kasi na inaweza kufika wakati wowote. Pia, maisha katika mfumo huu ni mafupi na hayana uhakika. Hakuna yeyote kati yetu anayeweza kujua ikiwa atakuwa hai kesho.—Yak. 4:13, 14.

Broshua Mrudie Yehovac inasema hivi: “Uwe na hakika kwamba Yehova atakutegemeza unapojitahidi kumrudia. Atakusaidia kukabiliana na mahangaiko, kuondoa maumivu ya kihisia, na kupata amani ya akili na moyo kwa sababu ya kuwa na dhamiri safi. Kisha unaweza kuchochewa kumtumikia tena Yehova pamoja na waabudu wenzako.”—1 Pet. 2:25.

c Imechapishwa na Mashahidi wa Yehova na inapatikana katika lugha nyingi kwenye tovuti ya jw.org.

MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA ILI UENDELEE KUWA NA NGUVU KIROHO

9. Unaweza kujipatia nguvu kutoka kwa Yehova kwa njia zipi? (Tazama pia sanduku “Maandiko Yenye Kufariji Ikiwa Mpendwa Wako Amemwacha Yehova.”)

9 Shikamana na ratiba nzuri ya kiroho. Ni muhimu uendelee kujiimarisha mwenyewe na washiriki wengine wa familia. Unaweza kufanyaje hivyo? Jipatie nguvu kutoka kwa Yehova kwa kudumisha ratiba nzuri ya kusoma Neno la Mungu, kulitafakari, na pia kuhudhuria mikutano ya Kikristo. Joanna, ambaye baba na dada yake waliiacha kweli, anasema hivi: “Ninapata utulivu ninaposoma kuhusu wahusika wa Biblia kama vile Abigaili, Esta, Ayubu, Yosefu, na Yesu. Mifano yao hujaza moyo na akili yangu mawazo mazuri yanayotuliza maumivu yangu. Pia, nimetambua kwamba nyimbo zetu zilizotungwa zinanitia moyo sana.”

Maandiko Yenye Kufariji Ikiwa Mpendwa Wako Amemwacha Yehova

  • Zaburi 30:10

  • Zaburi 34:4, 6, 18, 19

  • Zaburi 39:12

  • Zaburi 61:1, 2

  • Zaburi 94:17-19

  • Waefeso 3:20

  • Wafilipi 4:6, 7

10. Zaburi 32:6-8 inafunua nini kuhusu jinsi ya kukabiliana na hisia zenye kutaabisha?

10 Mweleze Yehova mahangaiko yako. Unapokabili hisia zenye kukutaabisha usiache kusali kwake. Msihi Mungu wetu mwenye upendo akusaidie kuona mambo kwa njia yake na kukupa “ufahamu na kukufundisha njia unayopaswa kufuata.” (Soma Zaburi 32:6-8.) Ni kweli kwamba huenda ukahisi maumivu sana unapomweleza Yehova jinsi unavyohisi kikweli. Lakini Yehova anaelewa kikamili maumivu ya moyo wako. Anakupenda sana na anakusihi ummiminie moyo wako.​—Kut. 34:6; Zab. 62:7, 8.

11. Kulingana na Waebrania 12:11, kwa nini tunapaswa kuitumaini nidhamu ya Yehova yenye upendo? (Tazama pia sanduku “Kutenga na Ushirika​—Nidhamu ya Yehova Yenye Upendo.”)

11 Unga mkono uamuzi uliofanywa. Kutenga na ushirika ni sehemu ya mpango wa Yehova. Rekebisho lake la upendo ni kwa faida ya kila mmoja wetu, kutia ndani mkosaji. (Soma Waebrania 12:11.) Inaelekea maelezo yoyote yanayochambua jinsi kisa cha kihukumu kilivyoshughulikiwa na wazee, huanzishwa na mtu ambaye hakutaka kutaja mambo mabaya yaliyofanywa na mkosaji. Kwa ufupi, sisi hatuna habari kamili. Hivyo, ni jambo la hekima kutumaini kwamba wazee walioshughulikia kisa hicho cha hukumu walifanya kila jitihada ili kufuata kanuni za Kimaandiko na kuhukumu “kwa ajili ya Yehova.”​—2 Nya. 19:6.

Kutenga na Ushirika​—Nidhamu ya Yehova Yenye Upendo

Mpango wa kutenga na ushirika unaonyeshaje upendo wa Mungu?

  1. 1. Upendo unawachochea wazee wa kutaniko wafanye yote wawezayo ili kumsaidia mkosaji. Mkristo hutengwa na ushirika wakati tu mambo haya mawili yanapotukia pamoja: Ametenda dhambi nzito, na anakataa kutubu.​—Ebr. 12:7, 9-11.

  2. 2. Kutenga na ushirika hulilinda kutaniko. Mkosaji asiyetubu ni kama mtu mwenye ugonjwa unaosababishwa na kirusi kinachoenea kwa kasi sana, ambaye anahitaji kutengwa ili kuwalinda wengine dhidi ya ugonjwa huo.​—1 Kor. 5:6, 7, 11-13.

  3. 3. Kutengwa na ushirika kunaweza kumchochea mkosaji atubu. Wengi waliotengwa na ushirika waliweza kurudiwa na fahamu na baadaye kumrudia Yehova.​—Luka 15:11-24.

  4. 4. Mkosaji aliyetubu anapomrudia Yehova, mbinguni wanashangilia na kutaniko linamkaribisha tena.​—Luka 15:7.

12. Baadhi ya ndugu na dada wamepata manufaa gani kwa sababu ya kuunga mkono mpango wa Yehova wa kutia nidhamu?

12 Unapounga mkono uamuzi wa wazee wa kumtenga na ushirika mpendwa wako, unaweza kumsaidia amrudie Yehova. Elizabeth, aliyenukuliwa awali anakiri hivi: “Ilikuwa vigumu sana kukata mawasiliano na mwana wetu aliyekuwa mtu mzima. Lakini baada ya kumrudia Yehova, mwana wetu alikiri kwamba alistahili kutengwa na ushirika. Baada ya muda, alieleza kwamba alithamini mambo aliyojifunza. Nami nikaja kuithamini nidhamu ya Yehova.” Mark, mume wa Elizabeth, anaongezea hivi: “Baada ya muda fulani, mwana wetu alituambia kwamba sababu moja iliyomfanya atake kumrudia Yehova ni kwamba tulifanya kile tulichopaswa kufanya. Ninafurahi sana kwamba Yehova alitusaidia tumtii.”

13. Ni nini kinachoweza kukusaidia kukabiliana na maumivu ya kihisia?

13 Zungumza na rafiki anayeelewa jinsi unavyohisi. Shirikiana na Wakristo wakomavu wanaoweza kukusaidia kudumisha mtazamo unaofaa. (Met. 12:25; 17:17) Joanna, aliyetajwa awali, anasema hivi: “Moyoni nilihisi niko peke yangu. Lakini kuzungumza na marafiki wanaotumainika kulinisaidia kukabiliana na hali hiyo.” Unaweza kufanya nini ikiwa inaonekana kana kwamba baadhi ya ndugu na dada kutanikoni wanasema mambo ambayo yanakufanya ujihisi vibaya hata zaidi?

14. Kwa nini tunahitaji ‘kuendelea kuvumiliana na kusameheana kwa hiari’?

14 Waonyeshe subira ndugu na dada zako. Kihalisi, hatuwezi kutarajia kwamba nyakati zote watu wataitikia kwa njia bora. (Yak. 3:2) Sisi sote si wakamilifu, hivyo usishangae ikiwa baadhi ya watu hawajui waseme nini au hata bila kukusudia wanasema jambo linalokuumiza. Kumbuka himizo hili la mtume Paulo: “Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari hata ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine.” (Kol. 3:13) Dada fulani ambaye mtu wake wa ukoo alitengwa na ushirika anaeleza hivi: “Yehova amenisaidia kuwasamehe akina ndugu ambao walijitahidi kufanya kilicho sawa, lakini kwa njia isiyo kamilifu.” Kutaniko linaweza kufanya nini ili kuwasaidia washiriki wa familia walio waaminifu?

KUTANIKO LINAWEZA KUSAIDIA

15. Ni nini kinachoweza kuwasaidia washiriki wa familia ambao mpendwa wao ametengwa na ushirika hivi karibuni?

15 Wakaribishe kwa uchangamfu washiriki wa familia walio waaminifu. Dada anayeitwa Miriam anakiri kwamba alikuwa na wasiwasi kuhusu kwenda mikutanoni baada ya ndugu yake kutengwa na ushirika. Anasema hivi: “Niliogopa kusikia mambo ambayo watu wangesema. Lakini kulikuwa na ndugu na dada wengi ambao walihuzunika pamoja nami, bila kusema jambo lolote lisilofaa kumhusu ndugu yangu aliyekuwa ametengwa na ushirika. Ninashukuru kwamba kwa sababu yao, sikujihisi mpweke nilipokuwa na huzuni.” Dada mwingine anakumbuka hivi: “Baada ya mwana wangu kutengwa na ushirika, ndugu na dada zangu wapendwa walikuja kutufariji. Baadhi yao walikiri kwamba hawakujua waseme nini. Walilia pamoja nami au kuniandikia ujumbe. Mambo waliyofanya yalinisaidia sana!”

16. Kutaniko linaweza kuendeleaje kuwafariji na kuwasaidia wale ambao mpendwa wao ametengwa na ushirika?

16 Endeleeni kuwategemeza washiriki wa familia walio waaminifu. Wanahitaji upendo na kitia moyo chenu sasa kuliko wakati mwingine wowote. (Ebr. 10:24, 25) Nyakati nyingine, washiriki wa familia wa mtu aliyetengwa na ushirika wamehisi kwamba baadhi ya watu kutanikoni hawashirikiani nao kama awali. Usiruhusu jambo hilo litokee! Vijana ambao wazazi wao wameiacha kweli wanahitaji hasa kupongezwa na kutiwa moyo. Maria, ambaye mume wake alitengwa na ushirika na kuiacha familia yake anasema hivi: “Baadhi ya marafiki wangu walikuja nyumbani na kupika chakula na walijiunga nami katika funzo letu la familia. Walihisi maumivu yangu na kulia pamoja nami. Walinitetea wakati porojo zisizo za kweli zilipoenezwa. Kwa kweli, walinitia moyo sana!”​—Rom. 12:13, 15.

Mama na watoto wake wawili wakiwakaribisha wazee wawili wa kutaniko waliowatembelea nyumbani.

Kutaniko linaweza kuwategemeza kwa upendo washiriki wa familia walio waaminifu (Tazama fungu la 17)e

17. Wazee wa kutaniko wanaweza kuwategemezaje kwa huruma washiriki wa familia walio waaminifu?

17 Enyi wazee wa kutaniko, tumieni fursa zinazopatikana ili kuwaimarisha washiriki wa familia walio waaminifu. Mna wajibu wa pekee wa kuwafariji waabudu wenzenu ambao wapendwa wao wamemwacha Yehova. (1 The. 5:14) Chukueni hatua ya kwanza kuwatia moyo kabla na baada ya mikutano ya Kikristo. Watembeleeni nyumbani na kusali pamoja nao. Hubirini pamoja nao katika huduma, au nyakati nyingine waalike wajiunge nanyi kwenye ibada yenu ya familia. Wachungaji wa kiroho wanahitaji kuwaonyesha kondoo wa Yehova wanaohuzunika huruma, upendo, na kuwakazia fikira.​—1 The. 2:7, 8.

USIKATE TAMAA NA ENDELEA KUMTUMAINI YEHOVA

18. Kulingana na 2 Petro 3:9, Mungu anataka wale walioacha kumtumikia wafanye nini?

18 Yehova “hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.” (Soma 2 Petro 3:9.) Ingawa huenda mtu akafanya dhambi nzito, bado uhai wake ni wenye thamani machoni pa Mungu. Fikiria gharama kubwa ambayo Yehova alilipa​—dhabihu ya fidia ya Mwana wake mpendwa—kwa ajili ya wanadamu watenda dhambi. Kwa huruma, Yehova anawasaidia watu kama hao wamrudie. Anatumaini kwamba watachagua kufanya hivyo, kama tunavyoona kwenye mfano wa Yesu wa mwana mpotevu. (Luka 15:11-32) Baadaye, watu wengi walioacha kweli, walimrudia Baba yao wa mbinguni mwenye upendo. Na kutaniko liliwakaribisha kwa mikono miwili. Elizabeth, aliyenukuliwa awali, alipata shangwe ya kumwona mwana wake akirudishwa kutanikoni. Anapokumbuka jambo hilo anasema hivi: “Ninawashukuru sana wale waliotutia moyo tusikate tamaa.”

19. Kwa nini tunaweza kuendelea kumtumaini Yehova?

19 Sikuzote tunaweza kumtumaini Yehova. Kamwe hatupatii miongozo inayoweza kutudhuru. Yeye ni Baba mkarimu na mwenye huruma ambaye anawapenda sana wale wote wanaompenda na kumwabudu. Uwe na hakika kwamba Yehova hatakuacha unapotaabika. (Ebr. 13:5, 6) Mark, aliyetajwa awali, anasema hivi: “Yehova hatatutupa kamwe. Hayuko mbali nasi tunapopitia hali ngumu.” Yehova ataendelea kutupatia “nguvu zinazopita zile za kawaida.” (2 Kor. 4:7) Naam, unaweza kuendelea kuwa mwaminifu na mwenye tumaini hata mpendwa wako anapomwacha Yehova.

UMEJIFUNZA NINI KATIKA MAANDIKO YAFUATAYO?

  • Zaburi 78:40, 41

  • Zaburi 32:6-8

  • Waebrania 12:11

WIMBO 44 Sala ya Mtu wa Hali ya Chini

a Ni jambo lenye kuhuzunisha sana mpendwa wetu anapomwacha Yehova! Makala hii itazungumzia jinsi Mungu wetu anavyohisi jambo hilo linapotokea. Na itazungumzia mambo hususa ambayo washiriki wa familia walio waaminifu wanaweza kufanya ili kukabiliana na maumivu wanayopitia, na kuendelea kuwa na nguvu kiroho. Pia, makala hii itazungumzia jinsi wote kutanikoni wanavyoweza kuifariji na kuitegemeza familia inayopitia hali hiyo.

b Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.

d MAELEZO YA PICHA: Ndugu anapoiacha familia yake na Yehova, mke na watoto wake huteseka.

e MAELEZO YA PICHA: Wazee wawili wanaitembelea familia ili kuwatia moyo.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki