Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w21 Oktoba kur. 29-31
  • 1921—Miaka Mia Moja Iliyopita

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • 1921—Miaka Mia Moja Iliyopita
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2021
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • WAHUBIRI WALIO JASIRI
  • FUNZO LA KIBINAFSI NA LA FAMILIA
  • KITABU KIPYA!
  • KAZI ILIYOKUWA MBELE
  • Kufanya Yale Ambayo Yehova Anataka Huleta Baraka
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2017
  • 1922—Miaka Mia Moja Iliyopita
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2022
  • Maamuzi Ambayo Yanaongoza Kwenye Furaha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2007
  • Kuhubiri Hadharani na Kutoka Nyumba Hadi Nyumba
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2021
w21 Oktoba kur. 29-31

1921—Miaka Mia Moja Iliyopita

“KWA hiyo, ni kazi gani hususa ambayo tunatarajia kufanya mwaka huu?” Wanafunzi wa Biblia waliuliza swali hilo kwenye gazeti la Mnara wa Mlinzi la Januari 1, 1921. Ili kujibu, lilinukuu andiko la Isaya 61:1, 2, lililowakumbusha kazi yao ya kuhubiri. “BWANA amenitia mafuta, niwahubiri wanyenyekevu habari njema . . . . Kutangaza mwaka wa BWANA uliokubaliwa, na siku ya kisasi cha Mungu wetu.”

WAHUBIRI WALIO JASIRI

Ili kutimiza kazi yao ya kuhubiri, Wanafunzi wa Biblia walipaswa kuwa jasiri. Wangehitaji kutangaza “habari njema” kwa wapole, na pia kutangaza “siku ya kisasi” kwa waovu.

Ndugu J. H. Hoskin, aliyeishi nchini Kanada alitoa ushahidi kwa ujasiri licha ya upinzani. Katika kipindi cha majani kuchipuka mwaka wa 1921, alikutana na kasisi wa kanisa la Methodisti. Ndugu Hoskin alianza mazungumzo yake kwa kusema: “Tunapaswa kuwa na mazungumzo mazuri kuhusu Maandiko, na hata ikiwa hatukubaliani katika baadhi ya mambo, tunaweza kumaliza mazungumzo yetu kwa amani na kuendelea kuwa marafiki.” Lakini hilo halikutukia. Ndugu Hoskin anakumbuka hivi: “Tulizungumza kwa dakika chache tu, [kasisi huyo] alipogonga mlango kwa nguvu sana hivi kwamba nilihisi kioo chake kikubwa kingevunjika na kuanguka sakafuni.”

Kasisi huyo alizungumza kwa sauti kubwa akisema: “Kwa nini usiende kwa watu wasio Wakristo na kuzungumza nao?” Ndugu Hoskin hakujibu, lakini alipokuwa akiondoka alijiambia, ‘Nilihisi nilikuwa nikizungumza na mmoja wao!’

Siku iliyofuata kwenye mahubiri yake, kasisi huyo aliendelea na mashambulizi. Ndugu Hoskin alikumbuka hivi: “Aliwaonya wafuasi wake kunihusu, akiwaambia watu kwamba nilikuwa tapeli mbaya sana kuwahi kutokea kwenye mji huo, na kwamba nilipaswa kupigwa risasi.” Lakini Ndugu Hoskin hakuyumbishwa hata kidogo, aliendelea kuhubiri na alipata matokeo mazuri. Ndugu Hoskin alisema hivi: “Nilifurahia sana kuhubiri hapo. Baadhi ya watu hata walipaza sauti wakisema hivi, ‘Ninajua wewe ni mtu wa Mungu!’ na waliuliza ikiwa wangeweza kunisaidia na kunipatia vitu ninavyohitaji.”

FUNZO LA KIBINAFSI NA LA FAMILIA

Ili kuwasaidia watu wafanye maendeleo, Wanafunzi wa Biblia walichapisha programu ya kujifunzia Biblia kwenye gazeti The Golden Age.a Programu ya vijana ya kujifunza Biblia ilikuwa na maswali kwa ajili ya wazazi ambayo wangejadili na watoto wao. Wazazi walihitaji “kuwauliza watoto wao maswali hayo na kuwasaidia kupata majibu katika Biblia.” Baadhi ya maswali kama vile, “Kuna vitabu vingapi katika Biblia?,” yaliwafundisha mambo ya msingi. Maswali mengine kama vile, “Je, kila Mkristo wa kweli anapaswa kutarajia mateso ya aina fulani?,” yaliwatayarisha vijana wawe wahubiri jasiri.

Programu ya kujifunza zaidi katika kitabu Divine Plan of The Ages iliwapatia Wanafunzi wa Biblia waliokomaa maswali yenye kuchochea fikira yaliyotegemea buku la kwanza la kitabu Studies in the Scriptures. Maelfu ya wasomaji walinufaika kutokana na programu hizo, lakini gazeti The Golden Age la Desemba 21, 1921, lilitangaza kwamba programu hizo zote zingesitishwa. Kwa nini kulikuwa na badiliko hilo la ghafla?

KITABU KIPYA!

Kitabu The Harp of God

Kadi ikiwa na mgawo wa usomaji

Kadi zenye maswali

Ndugu waliokuwa wakiongoza walitambua kwamba Wanafunzi wapya wa Biblia walihitaji kujifunza kweli za msingi kwa utaratibu mzuri. Hivyo, kitabu The Harp of God kilitolewa Novemba 1921. Watu waliopendezwa na kukubali kitabu hicho waliandikishwa kwa ajili ya mafunzo ya Biblia ya kitabu The Harp of God. Mafunzo hayo ambayo wasomaji walijiongoza wenyewe, yaliwasaidia kutambua “mpango wa Mungu wa kuwabariki wanadamu kwa uzima wa milele.” Mafunzo hayo yalifanyikaje?

Mtu alipokubali nakala ya kitabu hicho, alipewa mgawo wa kusoma uliochapishwa kwenye kadi ndogo. Juma lililofuata, alipokea kadi yenye maswali yaliyotegemea mgawo huo. Kadi hiyo ilimalizia kwa kutoa mgawo wa usomaji kwa ajili ya juma lililofuata.

Kila juma kwa majuma 12, mwanafunzi alipokea kadi mpya kutoka kwa kikundi au kutaniko lililo karibu. Mara nyingi kadi hizo zilitumwa na ndugu na dada wenye umri mkubwa au ambao hali zao hazikuwaruhusu kufanya mengi. Kwa mfano, Anna K. Gardner, kutoka Millvale, Pennysylvania, Marekani, anakumbuka hivi: “Kitabu The Harp of God kilipotoka, kilimpatia Thayle, dada yangu aliyekuwa na tatizo la kutembea, kazi zaidi ambayo angeweza kufanya, yaani, kutuma kila juma kadi za maswali.” Mafunzo yalipokamilika, mwanafunzi alitembelewa kibinafsi ili kumsaidia aendelee na elimu yake ya Biblia.

Thayle Gardner akiwa katika kigari chake cha magurudumu

KAZI ILIYOKUWA MBELE

Mwishoni mwa mwaka huo, Ndugu J. F. Rutherford alituma barua kwa vikundi vyote. Alisema kwamba “ushahidi kuhusu Ufalme uliotolewa mwaka huu umekuwa mkubwa zaidi na wenye matokeo zaidi kuliko uliotolewa katika mwaka mwingine wowote katika kipindi cha mavuno.” Kisha aliongezea hivi: “Bado kuna kazi kubwa ya kufanya. Watieni moyo wengine wajiunge katika utumishi huu uliobarikiwa.” Ni wazi kwamba Wanafunzi wa Biblia walitumia ushauri huo. Katika mwaka wa 1922, wangeutangaza Ufalme kwa ujasiri na kwa njia ya pekee sana.

Marafiki Jasiri

Wanafunzi wa Biblia walionyesha upendo wa kindugu kwa kusaidiana. Walikuwa marafiki jasiri, ‘waliozaliwa kwa ajili ya nyakati za taabu,’ kama simulizi lifuatalo linavyoonyesha.​—Met. 17:17.

Jumanne, Mei 31, 1921, kulitokea yale yaliyokuja kujulikana kuwa mauaji maarufu ya Tulsa Race Massacre huko Tulsa, Oklahoma, Marekani, baada ya mwanamume mweusi kufungwa gerezani na kushtakiwa kwa kumshambulia mwanamke mweupe. Kikundi cha wanaume weupe zaidi ya 1,000 kilipopambana na kikundi kidogo zaidi cha wanaume weusi, mapigano hayo yalisambaa haraka hadi kwenye makazi ya watu weusi huko Greenwood, ambapo waliiba vitu na kuchoma zaidi ya nyumba na biashara 1,400. Vifo vilivyoripotiwa rasmi ni 36, lakini huenda idadi halisi ilikuwa watu 300 hivi.

Ndugu Richard J. Hill, Mwanafunzi wa Biblia aliyekuwa mweusi na mkazi wa Greenwood, alisema hivi kuhusu kilichotokea: “Siku ambayo vurugu zilitokea, kama kawaida tulikuwa katika kikundi chetu cha kujifunza Biblia. Baada ya funzo kuisha, tulisikia sauti za risasi zikipigwa huko mjini. Tulipoenda kulala bado zilikuwa zikisikika.” Kufikia Jumatano asubuhi, Juni 1, hali ilikuwa mbaya zaidi. Anasema hivi: “Baadhi ya watu walikuja na kusema kwamba ikiwa tunataka ulinzi, ni vema twende mara moja kwenye jengo la manispaa.” Hivyo, Ndugu Hill pamoja na mke na watoto wake watano walikimbilia kwenye jengo hilo la manispaa. Kwa makadirio, huko kulikuwa na wanaume na wanawake weusi 3,000 waliolindwa na jeshi la taifa, lililokuwa limeitwa kutuliza vurugu hizo.

Wakati huohuo, Ndugu Arthur Claus, aliyekuwa mweupe, alifanya uamuzi wa kijasiri. Alisema hivi: “Niliposikia kwamba vikundi vyenye vurugu vilikuwa vikifanya ghasia katika mji wote huko Greenwood, vikiiba na kuchoma moto nyumba, niliamua kwenda kumtafuta Ndugu Hill, rafiki yangu mpendwa.”

Akitumia kitabu The Harp of God, Arthur Claus alifundisha kikundi chenye watoto 14

Alipowasili kwenye nyumba ya Ndugu Hill, alimkuta jirani yake mweupe akiwa ameshika bunduki. Jirani huyo alikuwa pia rafiki ya Ndugu Hill, na alihisi kwamba Arthur alikuwa miongoni mwa wafanya ghasia. Alipaza sauti hivi: “Kwa nini uko kwenye ua wa mtu huyu?”

Arthur anakumbuka hivi: “Ikiwa nisingempa jibu linaloridhisha, angenipiga risasi. Nilimhakikishia kwamba nilikuwa rafiki ya Ndugu Hill na nilikuwa nimemtembelea nyumbani kwake mara nyingi.” Arthur na jirani huyo walifanikiwa kuilinda nyumba ya Ndugu Hill dhidi ya watu waliokuwa wakiiba vitu.

Baada ya muda mfupi, Arthur aligundua kwamba Ndugu Hill na familia yake walikuwa kwenye jengo la manispaa. Arthur aliambiwa kwamba watu weusi hawangeweza kuondoka hapo bila kibali kilichotiwa sahihi na Jenerali Barrett, aliyekuwa anasimamia. Arthur anasema hivi: “Ilikuwa vigumu sana kumwona jenerali huyo. Nilipomwambia kuhusu mipango yangu, aliniuliza: ‘Je, utailinda familia hii na kuwapatia mahitaji yao?’ Bila shaka, nilikubali kwa moyo wote.”

Akiwa na kibali mkononi mwake, Arthur alienda haraka kwenye jengo la manispaa. Akampatia kibali hicho ofisa aliyesema hivi: “Imetiwa sahihi na jenerali mwenyewe! Je, unajua kwamba wewe ni mtu wa kwanza leo kumtoa mtu katika eneo hili?” Baada ya muda mfupi, Ndugu Hill na familia yake walipatikana. Wote walijazana kwenye gari la Arthur na kuelekea nyumbani.

“Sisi sote ni sawa miongoni mwa watu wa Mungu waliojiweka wakfu”

Ndugu Claus alihakikisha kwamba Ndugu Hill na familia yake walikuwa salama. Wengine walipoona ujasiri na upendo wa kindugu wa Ndugu Claus, walivutiwa na mfano wake. Arthur anasema hivi: “Yule jirani aliyesaidia kulinda nyumba ya Ndugu Hill alivutiwa zaidi na kweli. Na watu wengine wengi walipendezwa na kweli kwa sababu waliona kwamba hatukuwa na ubaguzi wa rangi, na kwamba sisi sote ni sawa miongoni mwa watu wa Mungu waliojiweka wakfu.”

a Gazeti The Golden Age lilibadilishwa jina na kuwa Consolation mwaka wa 1937, na baadaye Amkeni! mwaka wa 1946.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki