Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w22 Desemba kur. 2-7
  • Tunaweza Kuishi Milele

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Tunaweza Kuishi Milele
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2022
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • YEHOVA ANAISHI MILELE
  • TULIUMBWA ILI TUISHI MILELE
  • KUSUDI LA YEHOVA HALIJABADILIKA
  • WAKATI UJAO MZURI UKO KARIBU
  • Unapaswa Kufanya Nini Ili Uishi Milele?
    Maswali ya Biblia Yajibiwa
  • Je, Kweli Uhai Udumuo Milele Wawezekana?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Kuishi Milele Si Ndoto Tu
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Njia ya Kuishi Milele
    Kumsikiliza Mwalimu Mkuu
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2022
w22 Desemba kur. 2-7

MAKALA YA 49

Tunaweza Kuishi Milele

“Uzima wa milele ndio huu.”​—YOH. 17:3.

WIMBO 147 Uzima wa Milele Umeahidiwa

MUHTASARIa

1. Kutafakari ahadi ya Yehova ya uzima wa milele kuna matokeo gani?

YEHOVA anaahidi kwamba wale wanaomtii watapata “uzima wa milele.” (Rom. 6:23) Tunapotafakari ahadi ambayo Yehova anatupatia, kwa hakika upendo wetu kwake unaimarika. Hebu fikiria jambo hili: Baba yetu wa mbinguni anatupenda sana hivi kwamba hatutatenganishwa kamwe naye.

2. Tumaini la uzima wa milele linatusaidiaje?

2 Ahadi ya Mungu ya uzima wa milele hutusaidia kuvumilia majaribu tunayokabili sasa. Hata adui zetu wakitishia kutuua, hatutalegeza msimamo wetu. Kwa nini? Sababu moja ni kwamba tunajua ikiwa tutakufa tukiwa waaminifu kwa Yehova, atatufufua tukiwa na tumaini la kuishi bila kufa. (Yoh. 5:28, 29; 1 Kor. 15:55-58; Ebr. 2:15) Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba inawezekana kwetu kuishi milele? Fikiria sababu zifuatazo.

YEHOVA ANAISHI MILELE

3. Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova anaweza kutusaidia tuendelee kuishi milele? (Zaburi 102:12, 24, 27)

3 Tunajua kwamba Yehova anaweza kutusaidia tuishi milele kwa sababu yeye ndiye Chanzo cha uhai, naye anaishi milele. (Zab. 36:9) Fikiria baadhi ya mistari ya Biblia inayothibitisha kwamba sikuzote Yehova amekuwepo na sikuzote ataendelea kuwepo. Andiko la Zaburi 90:2 linasema kwamba Yehova ni wa “tangu milele hadi milele.” Zaburi 102 inataja jambo kama hilo pia. (Soma Zaburi 102:12, 24, 27.) Na nabii Habakuki aliandika hivi kuhusu Baba yetu wa mbinguni: “Je, wewe si wa tangu milele, Ee Yehova? Ee Mungu wangu, Mtakatifu wangu, wewe hufi.”​—Hab. 1:12.

4. Je, tunapaswa kuwa na wasiwasi ikiwa hatuelewi wazo la kwamba Yehova amekuwepo sikuzote? Eleza.

4 Je, ni vigumu kwako kuelewa wazo la kwamba Yehova amekuwepo kwa “umilele wote”? (Isa. 40:28) Ni jambo la kawaida kuhisi hivyo. Elihu alisema hivi kumhusu Mungu: “Idadi ya miaka yake haiwezi kufahamika.” (Ayu. 36:26) Lakini ikiwa hatuelewi jambo fulani, hilo halimaanishi kwamba jambo hilo si la kweli. Kwa mfano, ingawa hatuelewi kikamili jinsi mwangaza unavyofanya kazi, je, hilo linamaanisha kwamba mwangaza haupo? Hapana! Vivyo hivyo, sisi wanadamu huenda tusiweze kamwe kuelewa kikamili jinsi ambavyo Yehova amekuwepo sikuzote na sikuzote ataendelea kuwepo. Lakini hilo halimaanishi kwamba Mungu haishi milele. Ukweli kumhusu Muumba hautegemei mambo tunayoweza au tusiyoweza kuelewa. (Rom. 11:33-36) Na alikuwepo kabla ya ulimwengu kuwepo, kutia ndani vyanzo vya mwangaza kama vile jua. Tuna uhakika kwamba Yehova ndiye “Muumba wa dunia kwa nguvu zake.” Naam, alikuwepo kabla ‘hajazitandaza mbingu.’ (Yer. 51:15; Mdo. 17:24) Ni sababu gani nyingine inayotuthibitishia kwamba tunaweza kuishi milele?

TULIUMBWA ILI TUISHI MILELE

5. Adamu na Hawa walikuwa na tumaini gani?

5 Vitu vyote vilivyo hai ambavyo Yehova aliviumba mwishowe vingekufa, isipokuwa wanadamu. Aliwapatia tumaini la pekee la kutokufa kamwe. Hata hivyo, Yehova alimwonya hivi Adamu: “Kuhusu mti wa ujuzi wa mema na mabaya, usile matunda yake, kwa maana siku utakapokula matunda yake hakika utakufa.” (Mwa. 2:17) Ikiwa Adamu na Hawa wangemtii Yehova, hawangekufa. Inapatana na akili kufikia mkataa kwamba hatimaye Yehova angewaruhusu wale matunda kutoka kwenye “mti wa uzima.” Hilo lingemaanisha walikuwa na uhakikisho kutoka kwake kwamba ‘wangeishi milele.’b​—Mwa. 3:22.

Neno “Milele” Katika Biblia

Neno la Kiebrania ambalo mara nyingi hutafsiriwa kuwa “milele” ni ʽoh·lamʹ. Kama linavyotumiwa kwenye Biblia, linaweza kumaanisha kitu ambacho kilikuwepo kwa muda mrefu wakati uliopita au kitakachokuwepo kwa muda mrefu wakati ujao, bila kutaja mwanzo wala mwisho wake. (Yos. 24:2; Zab. 24:7, 9) Pia, linaweza kurejelea kitu ambacho kamwe hakina mwisho. Yehova ni wa milele katika maana hiyo. (Zab. 102:12, 24, 27) Biblia ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inatafsiri neno hilo la Kiebrania kwa kutumia maneno kama vile “milele,” “-dumu,” au “zamani za kale.” Muktadha ndio unaoamua neno litakalotumiwa.

6-7. (a) Ni nini kingine kinachoonyesha kwamba wanadamu hawakupaswa kufa? (b) Unatazamia kufanya mambo gani? (Tazama picha.)

6 Inasisimua kwamba baadhi ya watafiti wanataja uthibitisho wa kisayansi kwamba ubongo wetu una uwezo wa kuhifadhi habari nyingi zaidi kuliko zile tunazoweza kukusanya katika kipindi cha miaka ambayo tunaishi kwa sasa. Mwaka wa 2010, makala moja katika chapisho la Scientific American Mind ilisema kwamba kadirio moja la uwezo wa ubongo wetu kuhifadhi habari lilikuwa gigabyte milioni 2.5 hivi, kiwango kinacholingana na saa milioni tatu (yaani, zaidi ya miaka 300) ya vipindi vya televisheni vilivyorekodiwa. Na inawezekana kwamba hilo ni kadirio dogo. Ingawa hivyo, hilo linaonyesha kwamba Yehova aliubuni ubongo wetu uhifadhi habari nyingi zaidi ya zile tunazopokea katika miaka 70 au 80 tu.​—Zab. 90:10.

7 Pia, Yehova ametuumba tukiwa na tamaa kubwa ya kuendelea kuishi. Kuhusu wanadamu, Biblia inasema kwamba Mungu “ameweka umilele katika moyo wao.” (Mhu. 3:11) Hiyo ni sababu moja inayofanya tuone kifo kuwa adui. (1 Kor. 15:26) Tunapokuwa wagonjwa sana, je, tunakaa tu na kusubiri tufe? Hapana. Kwa kawaida, sisi huenda kumwona daktari na labda tunatumia dawa ili kutibu ugonjwa huo. Kwa kweli, sisi hufanya yote tunayoweza ili kuepuka kifo. Na mtu tunayempenda anapokufa, iwe ni kijana au mzee, sisi hupatwa na maumivu makali ya kihisia yanayodumu. (Yoh. 11:32, 33) Kwa kweli, Muumba wetu mwenye upendo hangetupatia tamaa na uwezo wa kuendelea kuishi, isipokuwa iwe kwamba kusudi lake lilikuwa wanadamu waendelee kuishi. Lakini tuna sababu nyingine zaidi za kuamini kwamba tunaweza kuishi bila kufa. Acheni tuchunguze baadhi ya matendo ya Yehova ya zamani na ya sasa yanayothibitisha kwamba hajabadili kusudi lake la mwanzoni.

Mkusanyo wa picha: Ndugu mwenye umri mkubwa akiwa ameketi kwenye meza yenye dawa za aina mbalimbali, anasoma Biblia na kuwazia mambo ambayo ataweza kufanya baada ya kupata nguvu tena katika ulimwengu mpya. 1. Anaendesha mashua. 2. Anachora picha. 3. Anatembea kando ya maporomoko ya maji.

Kwa kuwa tuna tumaini la kuishi milele, tunafurahia kuwazia mambo ambayo tutafanya wakati ujao (Tazama fungu la 7)c

KUSUDI LA YEHOVA HALIJABADILIKA

8. Kuhusu kusudi la Yehova kutuelekea, tunapata uhakikisho gani kwenye Isaya 55:11?

8 Ingawa Adamu na Hawa walifanya dhambi na kuwaletea watoto wao kifo, Yehova hakubadili maoni yake kuhusu kusudi lake. (Soma Isaya 55:11.) Bado kusudi lake ni kwamba wanadamu waaminifu waishi milele. Tunaona jambo hilo tunapochunguza mambo ambayo Yehova amesema na kufanya ili kutimiza kusudi lake.

9. Mungu ameahidi nini? (Danieli 12:2, 13)

9 Yehova ameahidi kwamba atawafufua wafu na kufanya iwezekane kwao kuishi milele. (Mdo. 24:15; Tito 1:1, 2) Mwanamume mwaminifu Ayubu alikuwa na uhakika kwamba Yehova anatamani sana kuwafufua waliokufa. (Ayu. 14:14, 15) Nabii Danieli alijua kwamba wanadamu wana tumaini la kufufuliwa na kupata nafasi ya kuishi milele. (Zab. 37:29; soma Danieli 12:2, 13.) Wayahudi katika siku za Yesu walijua pia kwamba Yehova angeweza kuwapatia watumishi wake waaminifu “uzima wa milele.” (Luka 10:25; 18:18) Yesu mwenyewe alizungumzia tena na tena ahadi hiyo, na yeye mwenyewe alifufuliwa na Baba yake.​—Mt. 19:29; 22:31, 32; Luka 18:30; Yoh. 11:25.

Mjane wa Sarefathi anampokea kwa shangwe mwana wake aliyefufuliwa na nabii Eliya.

Ufufuo ambao Eliya alifanya unakuhakikishia jambo gani? (Tazama fungu la 10)

10. Ufufuo uliofanywa zamani unathibitisha nini? (Tazama picha.)

10 Yehova ndiye Mpaji-Uhai naye ana nguvu za kuwafanya watu wawe hai tena. Alimwezesha nabii Eliya amfufue mwana wa mjane wa Sarefathi. (1 Fal. 17:21-23) Baadaye, kwa msaada wa Mungu, nabii Elisha alimfufua mwana wa mwanamke Mshunamu. (2 Fal. 4:18-20, 34-37) Masimulizi hayo na mengine ya ufufuo yanathibitisha kwamba Yehova ana nguvu za kuwafufua wafu. Yesu alipokuwa duniani, alithibitisha kwamba Baba yake alikuwa amempatia nguvu hizo. (Yoh. 11:23-25, 43, 44) Sasa Yesu yuko mbinguni naye amepewa “mamlaka yote mbinguni na duniani.” Hivyo, anaweza kutimiza ahadi kwamba “wote walio katika makaburi ya ukumbusho” watafufuliwa wakiwa na tumaini la kuendelea kuishi milele.​—Mt. 28:18; Yoh. 5:25-29.

11. Fidia inafanyaje iwezekane kwetu kuishi milele?

11 Kwa nini Yehova aliruhusu Mwana wake mpendwa afe kifo chenye maumivu makali? Yesu alifunua sababu aliposema hivi: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yoh. 3:16) Kwa kumtoa Mwana wake awe fidia ili kufunika dhambi zetu, Mungu anafanya iwezekane kwetu kupata uzima wa milele. (Mt. 20:28) Mtume Paulo alifafanua sehemu hiyo muhimu ya kusudi la Mungu alipoandika hivi: “Kwa kuwa kifo kilikuja kupitia mwanadamu, ufufuo wa wafu pia unakuja kupitia mwanadamu. Kwa maana kama vile katika Adamu wote wanakufa, vivyo hivyo pia katika Kristo wote watafanywa kuwa hai.”​—1 Kor. 15:21, 22.

12. Ufalme utasaidiaje kutimiza kusudi la Mungu kwa ajili yetu?

12 Yesu aliwafundisha wafuasi wake wasali kwamba Ufalme wa Mungu uje na mapenzi ya Mungu yatendeke duniani. (Mt. 6:9, 10) Kusudi la Mungu linatia ndani wanadamu kuishi milele duniani. Ili kutimiza hilo, Yehova amemweka rasmi Mwana wake awe Mfalme wa Ufalme wa Kimasihi. Mungu amekuwa akiwakusanya watu 144,000 kutoka duniani wafanye kazi pamoja na Yesu ili kutimiza mapenzi ya Mungu.​—Ufu. 5:9, 10.

13. Yehova anafanya nini sasa, nawe unahusikaje?

13 Sasa Yehova anakusanya “umati mkubwa” wa watu na kuwazoeza ili wawe raia wa Ufalme wake. (Ufu. 7:9, 10; Yak. 2:8) Licha ya kuishi katika ulimwengu uliogawanyika kwa sababu ya woga na vita, wale wanaofanyiza kikundi hicho wanajitahidi kushinda chuki ya kitaifa, kikabila, na kibinafsi. Kwa njia ya mfano, tayari wanafua panga zao ziwe majembe ya plau. (Mika 4:3) Badala ya kushiriki katika vita vinavyosababisha vifo vingi, wanawasaidia watu wapate “uzima ulio wa kweli” kwa kuwafundisha kumhusu Mungu wa kweli na makusudi yake. (1 Tim. 6:19) Huenda watu wa familia zao wakawapinga au huenda wakapoteza pesa kwa sababu wanaunga mkono Ufalme wa Mungu, lakini Yehova anahakikisha kwamba wanapata mahitaji yao. (Mt. 6:25, 30-33; Luka 18:29, 30) Mambo hayo yanatuhakikishia kwamba Ufalme wa Mungu ni halisi na kwamba utaendelea kutimiza kusudi la Yehova.

WAKATI UJAO MZURI UKO KARIBU

14-15. Hatimaye ahadi ya Mungu ya kuondoa kifo milele itatimizwaje?

14 Sasa Yesu ni Mfalme mbinguni na atatimiza ahadi ambazo Yehova ametoa. (2 Kor. 1:20) Tangu mwaka wa 1914, Yesu amekuwa akiwatiisha maadui wake. (Zab. 110:1, 2) Hivi karibuni, akiwa pamoja na watawala wenzake, watakamilisha ushindi wao na kuwaangamiza waovu.​—Ufu. 6:2.

15 Wakati wa Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Yesu, wafu watafufuliwa na wanadamu watiifu watafanywa kuwa wakamilifu. Baada ya jaribu la mwisho, wale ambao Yehova atawahukumu kuwa waadilifu “wataimiliki dunia, nao wataishi humo milele.” (Zab. 37:10, 11, 29) Tunafurahi kujua kwamba ‘adui wa mwisho kifo ataangamizwa.’​—1 Kor. 15:26.

16. Ni sababu gani kuu inayopaswa kutuchochea kumtumikia Yehova?

16 Kama ambavyo tumeona, tumaini letu la kuishi milele linategemea kabisa Neno la Mungu. Tumaini hilo linaweza kutusaidia kuendelea kuwa washikamanifu katika siku hizi ngumu za mwisho. Lakini ili kumfurahisha Yehova, hatupaswi kuchochewa tu na tamaa ya kuendelea kuishi. Sababu yetu kuu ya kuendelea kuwa washikamanifu kwa Yehova na Yesu ni kwamba tunawapenda sana. (2 Kor. 5:14, 15) Upendo huo unatuchochea kuwaiga na kuwatangazia wengine tumaini tulilo nalo. (Rom. 10:13-15) Tunapojifunza kuepuka ubinafsi na kuwa wakarimu, tunakuwa aina ya watu ambao Yehova anataka wawe rafiki zake milele.​—Ebr. 13:16.

17. Tuna jukumu gani la kibinafsi? (Mathayo 7:13, 14)

17 Je, tutakuwa miongoni mwa wale ambao watapata uzima wa milele? Yehova ametufungulia njia hiyo. Sasa ni juu yetu kuendelea kutembea kwenye njia inayoongoza kwenye uzima. (Soma Mathayo 7:13, 14.) Maisha yatakuwaje tutakapoishi milele? Tutazungumzia jibu la swali hilo katika makala inayofuata.

UNGEJIBUJE?

  • Ni nini kinachothibitisha kwamba wanadamu walikusudiwa kuishi milele?

  • Tunajuaje kwamba Yehova hajabadilisha kusudi lake kwamba wanadamu waishi milele?

  • Ni sababu gani kuu inayopaswa kutuchochea tutamani kuishi milele?

WIMBO 141 Muujiza wa Uhai

a Je, unatazamia kwa hamu kuishi milele? Yehova ametuahidi kwamba siku moja tutaishi bila kuwa na hofu ya kufa. Makala hii inazungumzia baadhi ya sababu zinazofanya tuwe na uhakika kabisa kwamba Yehova atatimiza ahadi yake.

b Tazama sanduku “Neno ‘Milele’ Katika Biblia.”

c MAELEZO YA PICHA: Ndugu aliyezeeka anawazia baadhi ya mambo ambayo atafurahia kufanya milele wakati ujao.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki