Sura ya 46
Njia ya Kuishi Milele
YEHOVA ametupa sisi zawadi nyingi za ajabu. Mojawapo ya zawadi zake nzuri sana ni uhai. Bila huo tusingeweza kufanya lo lote, sivyo?— Lakini ikiwa tunataka tuendelee kuwa na zawadi hiyo, kuna mambo fulani ambayo inatupasa tufanye.
Sasa hivi unafanya mojawapo ya mambo hayo. Ndivyo na mimi. Tunafanya mchana wote na usiku wote, hata wakati tumelala. Ikiwa tungeacha, tungekufa mara hiyo. Unajua ni nini?
Ndiyo, tunapumua. Kuna mambo mengine ambayo tunafanya kila siku ili tuendelee kuishi. Unaweza kutaja mengine kati ya hayo?— Tunakula chakula. Tunakunywa maji. Na tunalala usingizi. Mungu alitufanya hivyo ili tusiweze kuishi bila mambo haya.
Hakuna moja kati ya haya ambayo ni gumu kufanya. Kwa kweli, mimi napenda kula. Wewe hupendi? Lakini chakula kinatufanya sisi tuishi namna gani? Unajua? Kunatukia nini wakati tumekwisha kukimeza?
Mwili wetu unavunja chakula katika vipande vidogo sana sana. Halafu damu inavichukua hivi kupeleka kwenye kila sehemu ya mwili wetu. Chakula hiki kinatumiwa katika njia ya ajabu kujenga mfupa mpya, nyama mpya, nywele mpya, kucha, macho na sehemu nyingine za mwili. Ulijua hilo?—
Labda unataka kujua kunatukia nini kwa sehemu za zamani za mwili. Hizi zinakufa pole pole na kuondolewa kama takataka. Sehemu mpya zinakaa pahali pake.
Mageuzi haya yanatukia kila mahali katika mwili wetu. Haichukui muda mrefu mpaka mwili wetu wote unageuzwa upya. Yehova aliufanya mwili wetu ili ufanye hivi. Aliufanya uendelee kufanya hivi milele. Ndiyo, alimfanya mtu aishi milele.
Lakini watu wanakufa. Kwa sababu gani?— Kwa sababu Adamu alimkosea Mungu. Na sisi tukapata dhambi kutoka kwa Adamu. Yeye aliharibu hali njema ya mwanadamu na Mungu. Na uhai wetu unategemea juu ya Mungu.
lli kuishi milele, tunataka zaidi ya hewa na maji na chakula na usingizi. Lazima tuwe na hali nzuri pamoja na Mungu.
Hakuna daktari ambaye anaweza kutufanya tuishi milele. Hakuna dawa ya ajabu ambayo inaweza kutuzuia tusife. Njia peke yake ambayo tunaweza kuishi milele ni kwa kukaribia karibu kwa Mungu. Mwalimu Mkuu anatuambia namna ya kufanya hivyo.
Na tuchukue Biblia zetu na kuzifungua katika Yohana 17, mstari wa 3. Hapa tunapata maneno ya Yesu: “Na uzima wa milele ndio huu, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma.”
Mwalimu Mkuu alisema yatupasa tufanye nini ili tuishi milele?— Ni lazima tupate ujuzi. Hiyo maana yake inatupasa tujifunze. Ndiyo sababu tunajifunza Biblia.
Lakini kujifunza juu ya Yehova kutatusaidia namna gani tuishi milele?— Kumbuka, uzima wote unatoka kwake. Ili tupate upendeleo wake, inatupasa tumwabudu yeye kama Mungu wa pekee wa kweli. Lakini hatuwezi kumwabudu katika njia nzuri isipokuwa tunasikiliza maneno yake. Kama vile tunavyotaka chakula kila siku, vivyo ni lazima tujifunze juu ya Yehova kila siku. Hii inatuleta karibu na yeye. Biblia inasema: ‘Mtu hataishi kwa mkate tu, bali kwa maneno yote yanayotoka katika kinywa cha Yehova.’—Mathayo 4:4.
Tena inatupasa tupate ujuzi juu ya mwingine zaidi ya Mungu. Ni nani huyo?— Yesu Kristo. Hii ni kwa sababu Mungu alimtuma Yesu kuondoa dhambi. Yeye anaweza kuondoa dhara ambalo Adamu alifanya wakati Adamu alipomkosea Mungu. Yesu anaweza kutusaidia sisi turudie hali njema pamoja na Mungu. Na hilo haliwezekani katika njia nyingine yo yote.
Ndiyo sababu Biblia inasema: “Hakuna wokovu katika mwingine awaye yote.” Inatupasa tujifunze juu ya Yesu ikiwa tunataka kuishi milele. Na ikiwa kweli tuna imani katika yeye. tutaweza kuishi milele. Wakati atakapoleta hali nzuri kwenye dunia yote, atatusaidia tuishi milele na kufurahi. Ni jambo la hakika. Ndiyo sababu Biblia inasema hivi: “Yeye anayejizoeza imani katika Mwana anao uzima wa milele.”—Matendo 4:12; Yohana 3:36, NW.
Sasa, ina maana gani ‘kujizoeza imani’ katika Yesu?— Maana yake kwamba tunasadiki kweli kwamba hatuwezi kuendelea kuishi bila yeye. Tunaamini kwamba Mungu anatupa uzima wa milele kupitia kwa Yesu. Unasadiki hilo?—
‘Kujizoeza imani’ katika Yesu kunamaanisha jambo jingine tena. Ina maana kwamba tunamsadiki sana hata tunafanya ayasemayo. Hatufanyi mambo mengine tu na tusifanye mengine. Tunafanya mambo yote ambayo anasema. Na tunayafanya kwa sababu kweli tunataka. Je! hivyo ndivyo unataka kufanya?
Mojawapo ya mambo ambayo Mwalimu Mkuu anatuambia kufanya ni kusema kwa watu wengine juu ya Mungu na ufalme wake. Yeye mwenyewe alifanya hivyo ili kutuonyesha namna ya kufanya. Basi, ikiwa kweli tumejifunza kwa Yesu, hilo ndilo jambo ambalo tutafanya. Je! wewe unafanya hivyo?—
Lakini si hilo tu. Kila siku imetupasa tufanye mambo ambayo Biblia inasema ni mazuri. Inatupasa tuwe waangalifu tusifanye mambo mabaya. Imetupasa tuonyeshe kwamba kweli tunapendana.
Ikiwa tunafanya mambo haya, inaonyesha kwamba kweli tumekuwa tukimsikiliza Mwalimu Mkuu.
(Wanafunzi wa kweli wa Yesu Kristo wataweza kweli kuishi milele katika furaha duniani. Soma Biblia inayosema juu ya hili katika Zaburi 37:29, 34, Mathayo 19:16-21 na Warumi 6:23.)