Sura Ya 48
Unaweza kuishi katika ulimwengu mpya wa Mungu Wenye Amani
MUNGU aliwaweka Adamu na Hawa katika bustani ya Edeni. Ijapokuwa walifanya dhambi na kufa, Mungu amefanya mpango ili watoto wao, kutia ndani sisi tunaoishi leo, tuishi milele katika Paradiso. Biblia inatuahidi hivi: “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.”—Zaburi 37:29.
Biblia inazungumzia “mbingu mpya” na “dunia mpya.” (Isaya 65:17; 2 Petro 3:13) “Mbingu” za sasa ni serikali za wanadamu, lakini “mbingu mpya” ni serikali ya Yesu Kristo na wale wanaotawala pamoja naye mbinguni. Itafurahisha sana wakati mbingu mpya, ambazo ni serikali ya Mungu ya uadilifu na amani itakapotawala dunia yote.
Basi “dunia mpya” ni nini?— Dunia mpya itakuwa wanadamu wazuri wanaompenda Yehova. Wakati mwingine Biblia inaposema “dunia,” inamaanisha watu wanaoishi ndani yake wala si ardhi yenyewe. (Mwanzo 11:1; Zaburi 66:4; 96:1) Hivyo wale ambao ni dunia mpya watakaa papa hapa duniani.
Ulimwengu wa sasa wa watu waovu utakuwa umeondolewa. Kumbuka kwamba Gharika ya siku za Noa iliharibu ulimwengu wa watu waovu. Na kama tulivyojifunza, ulimwengu huu mwovu uliopo utaharibiwa kwenye Har-Magedoni. Hebu tuone jinsi hali itakavyokuwa katika ulimwengu mpya wa Mungu baada ya Har-Magedoni.
Je, ungependa kuishi milele katika Paradiso katika ulimwengu mpya wa Mungu wenye amani?— Hakuna daktari anayeweza kutupa uzima wa milele. Hakuna dawa inayoweza kutuzuia tusife. Ili tuishi milele, tunahitaji tu kumkaribia Mungu. Na Mwalimu Mkuu anatuambia jinsi ya kufanya hivyo.
Tusome pamoja katika Biblia zetu Yohana sura ya 17, mstari wa 3. Katika mstari huo Mwalimu Mkuu anasema: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.”
Hivyo, Yesu alisema tunahitaji kufanya nini ili tuishi milele?— Kwanza ni lazima tujifunze juu ya Baba yetu wa mbinguni, Yehova, na pia juu ya Mwana wake aliyetoa uhai wake kwa ajili yetu. Hii inamaanisha kwamba tunapaswa kujifunza Biblia. Kitabu hiki, Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu, kinatusaidia kufanya hivyo.
Lakini kujifunza kuhusu Yehova kutatusaidiaje tuishi milele?— Kama tu tunavyohitaji kula kila siku, ndivyo tunavyohitaji kujifunza kila siku kumhusu Yehova. Biblia inasema: ‘Binadamu hataishi kwa mkate tu, bali kwa kila neno linalotoka katika kinywa cha Yehova.’—Mathayo 4:4.
Tunahitaji pia kujifunza juu ya Yesu Kristo kwa sababu Mungu alimtuma ili atuondolee dhambi. Biblia inasema: “Hakuna wokovu katika mwingine yeyote.” Na inasema pia: “Yule anayemwamini Mwana ana uzima wa milele.” (Matendo 4:12; Yohana 3:36) Inamaanisha nini ‘kumwamini’ Yesu?— Inamaanisha kwamba tunamwamini Yesu kabisa na tunajua kwamba hatuwezi kuishi milele bila yeye. Je, tunaamini hivyo?— Iwapo tunaamini, tutaendelea kila siku kujifunza kutoka kwa Mwalimu Mkuu na tutafanya anayosema.
Njia moja ya kujifunza kutoka kwa Mwalimu Mkuu ni kwa kusoma kitabu hiki tena na tena, na kuzitazama picha zote zilizopo na kuzifikiria. Jaribu kujibu maswali yanayohusu picha hizo. Pia usome kitabu hiki na mama au baba. Iwapo wazazi hawako, soma na watu wengine wazima au na watoto wengine pia. Je, halitakuwa jambo la kupendeza ukiweza kuwasaidia wengine wajifunze kutoka kwa Mwalimu Mkuu kuhusu yale wanayopaswa kufanya ili waishi milele katika ulimwengu mpya wa Mungu?—
Biblia inatuambia hivi: “Ulimwengu unapitilia mbali.” Lakini Biblia inatuambia jinsi tunavyoweza kuishi milele katika ulimwengu mpya wa Mungu. Inasema: “Yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.” (1 Yohana 2:17) Basi tutawezaje kuishi milele katika ulimwengu mpya wa Mungu?— Tutaweza kuishi tukijifunza juu ya Yehova na juu ya Mwana wake mpendwa, Yesu. Na tunahitaji pia kufuata yale tunayojifunza. Kitabu hiki na kikusaidie kufanya hivyo.
[Sanduku katika ukurasa wa 251]
Unaposoma Isaya 11:6-9 na Isaya 65:25, unaona wanyama wanaoishi pamoja kwa amani. Hebu tazama picha hizi. Ona kuna mwana-kondoo, mwana-mbuzi, chui, ndama, simba, na watoto wakiwa pamoja nao. Je, unawajua hawa wanyama wengine wanaotajwa katika Biblia?— Mwone mvulana huyu anayecheza na nyoka! Wote wanaoishi katika ulimwengu mpya hawatakuwa na sababu ya kuogopa. (Hosea 2:18) Unaonaje hilo?—
[Sanduku katika ukurasa wa 252]
Hebu ona amani iliyoko miongoni mwa watu wa jamii zote. Wote wanapendana kama Yesu alivyosema wanafunzi wake wangependana. (Yohana 13:34, 35) Silaha za vita zinageuzwa kuwa vifaa vya kulimia. Biblia inatuambia amani na usalama ambao watu watafurahia katika ulimwengu mpya wa Mungu. Tunaweza kusoma mambo hayo kwenye Zaburi 72:7; Isaya 2:4; 32:16-18; na Ezekieli 34:25.
[Sanduku katika ukurasa wa 253]
Waone watu kwenye ukurasa huu. Wanaitunza dunia na kuifanya maridadi. Wanajenga nyumba nzuri na wana matunda na mboga kama inavyoonyeshwa hapa. Watu wanaishi kwa utulivu, na dunia imekuwa paradiso kama bustani ya Edeni ilivyokuwa. Tunaweza kusoma habari hizo zenye kupendeza kwenye Zaburi 67:6; 72:16; Isaya 25:6; 65:21-24; na Ezekieli 36:35.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 254]
Kama unavyoona hapa, watu wote wanafurahi na wana afya nzuri. Wanaweza kuruka juu kama kulungu. Hakuna aliyelemaa, aliye na upofu au mgonjwa. Kawatazame hawa waliofufuliwa! Biblia inataja mambo hayo kwenye Isaya 25:8; 33:24; 35:5, 6; Matendo 24:15; na Ufunuo 21:3, 4.