Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w23 Novemba kur. 14-19
  • Dumisha Uhakika Katika Yehova Unapokabili Changamoto Zisizotarajiwa

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Dumisha Uhakika Katika Yehova Unapokabili Changamoto Zisizotarajiwa
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2023
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • JINSI CHANGAMOTO ZISIZOTARAJIWA ZILIVYOWAATHIRI WAYAHUDI WALIORUDI
  • KAZIA FIKIRA KUFANYA MAPENZI YA MUNGU
  • JINSI YA KUIMARISHA UHAKIKA WETU KATIKA YEHOVA
  • DUMISHA UHAKIKA WAKO KATIKA YEHOVA HADI MWISHO
  • Mambo Makuu Katika Kitabu cha Ezra
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
  • Kitabu Cha Biblia Namba 15—Ezra
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Yehova Atimiza Ahadi Zake!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Ezra Akazia Haki ya Hukumu na Rehema
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Funzo)—2023
w23 Novemba kur. 14-19

MAKALA YA 48

Dumisha Uhakika Katika Yehova Unapokabili Changamoto Zisizotarajiwa

“‘Jipeni moyo, . . . kwa maana niko pamoja nanyi,’ asema Yehova wa majeshi.”—HAG. 2:4.

WIMBO 118 “Tusaidie Tuwe na Imani Zaidi”

MUHTASARIa

1-2. (a) Hali za Wayahudi waliorudi Yerusalemu zinafananaje na hali zetu? (b) Eleza kwa ufupi changamoto walizokabili Wayahudi. (Tazama sanduku “Siku za Hagai, Zekaria, na Ezra.”)

JE, WAKATI mwingine una hofu kuhusu wakati ujao? Huenda umepoteza kazi na una wasiwasi kwamba utashindwa kuitunza familia yako. Huenda una wasiwasi kuhusu usalama wa familia yako kwa sababu ya misukosuko ya kisiasa, mateso, au upinzani katika kazi yetu ya kuhubiri. Je, unakabili hali kama hizo? Ikiwa ndivyo, utanufaika kwa kuchunguza jinsi Yehova alivyowasaidia Waisraeli wa kale walipokabili hali kama hizo.

2 Wayahudi walioishi Babiloni walihitaji imani ili kuacha maisha ya starehe na kwenda kwenye nchi ambayo wengi wao hawakuijua. Muda mfupi baada ya kufika huko, walianza kuathiriwa na hali mbaya ya kiuchumi, kisiasa, pamoja na upinzani. Kwa hiyo, baadhi yao walishindwa kukazia fikira kazi ya kujenga upya hekalu la Yehova. Hivyo, karibu mwaka wa 520 K.W.K., Yehova aliwatuma manabii wawili, Hagai na Zekaria, ili kuchochea upya bidii ya watu wake. (Hag. 1:1; Zek. 1:1) Kama tutakavyoona, kazi ya kutia moyo ya manabii hao ilikuwa na matokeo mazuri sana. Hata hivyo, karibu miaka 50 baadaye, Wayahudi waliotoka utekwani walipunguza bidii yao tena. Ezra, mwandishi wa Sheria mwenye ustadi, alitoka Babiloni kwenda Yerusalemu ili kuwatia moyo watu wa Mungu watangulize ibada ya kweli.—Ezra 7:​1, 6.

Siku za Hagai, Zekaria, na Ezra

Mfuatano wa matukio muhimu katika siku za Hagai, Zekaria, na Ezra (tarehe zote ni za K.W.K.). 537: Wayahudi waliohamishwa waondoka Babiloni. 520: Nabii Hagai na Zekaria wakizungumza na Waisraeli jijini Yerusalemu. 515: Hekalu jijini Yerusalemu. 484: Malkia Esta aenda mbele ya kiti cha ufalme cha Mfalme Ahasuero. 468: Ezra asafiri pamoja na msafara wa Wayahudi. 455: Kuta za Yerusalemu.

TAREHE ZOTE NI ZA K.W.K.

  1. 537: Kikundi cha kwanza cha Wayahudi waliohamishwa charudi Yerusalemu

  2. 520: Hagai na Zekaria watoa unabii wakiwa Yerusalemu

  3. 515: Hekalu lakamilika

  4. 484: Esta achukua hatua baada ya Shasta wa Kwanza (Ahasuero) kutoa agizo la kuwaangamiza Wayahudi

  5. 468: Ezra asafiri kwenda Yerusalemu pamoja na kikundi cha pili cha Wayahudi waliohamishwa

  6. 455: Kuta za Yerusalemu zakamilika

3. Tutachunguza maswali gani? (Methali 22:19)

3 Kama unabii wa Hagai na Zekaria ulivyowasaidia watu wa Mungu kuendelea kumtumaini Yehova wakati wa upinzani, ndivyo unavyoweza kutusaidia kuendelea kuwa na uhakika katika msaada wa Yehova licha ya changamoto zisizotarajiwa. (Soma Methali 22:19.) Tunapochunguza ujumbe wa Mungu uliotolewa na Hagai na Zekaria na mfano wa Ezra, tutajibu maswali yafuatayo: Wayahudi waliorudi waliathiriwaje na changamoto zisizotarajiwa? Kwa nini tunapaswa kukazia fikira kufanya mapenzi ya Mungu tunapokabili changamoto zisizotarajiwa? Na tunawezaje kuimarisha uhakika wetu katika Yehova tunapokabili hali ngumu?

JINSI CHANGAMOTO ZISIZOTARAJIWA ZILIVYOWAATHIRI WAYAHUDI WALIORUDI

4-5. Huenda ni hali gani zilizofanya Wayahudi wapunguze bidii yao ya kujenga upya hekalu?

4 Wayahudi hao walipofika Yerusalemu, walikuwa na kazi nyingi za kufanya. Mara moja walianza kujenga upya madhabahu ya Yehova na kuweka msingi wa hekalu. (Ezra 3:​1-3, 10) Lakini bidii yao ilififia baada ya muda mfupi. Kwa nini? Zaidi ya kazi ya ujenzi wa hekalu, walihitaji kujenga nyumba zao, kupanda mazao, na kulisha familia zao. (Ezra 2:​68, 70) Isitoshe, walikabili upinzani kutoka kwa maadui waliopanga kuzuia kazi ya kujenga upya hekalu.—Ezra 4:​1-5.

5 Pia, Wayahudi hao waliorudi waliathiriwa na hali mbaya ya kiuchumi na kisiasa. Nchi yao ilikuwa chini Milki ya Uajemi. Mfalme Koreshi wa Uajemi alipokufa mwaka wa 530 K.W.K., mfalme aliyemfuata, Cambyses, alianzisha kampeni ya kijeshi ili kuishinda Misri. Inawezekana wanajeshi wake walipokuwa wakienda Misri, waliagiza wapewe chakula, maji, na makao kutoka kwa Waisraeli, jambo lililofanya hali iwe ngumu zaidi. Mfalme aliyefuata, Dario wa Kwanza, alipoanza kutawala, bado kulikuwa na matatizo mengi, kama vile uasi na misukosuko ya kisiasa katika Milki ya Uajemi. Bila shaka, hali hizo zilisababisha Wayahudi wengi waliotoka uhamishoni wawe na wasiwasi kuhusu jinsi ambavyo wangetunza familia zao. Kwa sababu ya changamoto hizo zisizotarajiwa, baadhi ya Wayahudi walihisi kwamba huo haukuwa wakati unaofaa wa kujenga upya hekalu la Yehova.—Hag. 1:2. 

6. Kulingana na Zekaria 4:​6, 7, Wayahudi walikabili changamoto gani nyingine, na Zekaria aliwahakikishia nini? 

6 Soma Zekaria 4:​6, 7. Mbali na changamoto za kiuchumi na za kisiasa, Wayahudi walikabili pia mateso. Mwaka wa 522 K.W.K., maadui wao walifanikiwa kusababisha kazi ya kujenga upya hekalu la Yehova ipigwe marufuku. Hata hivyo, Zekaria aliwahakikishia Wayahudi kwamba Yehova angetumia roho yake yenye nguvu kuondoa vipingamizi vyovyote. Mwaka wa 520 K.W.K., Mfalme Dario aliondoa marufuku na kuwaruhusu Wayahudi waendelee na ujenzi wa hekalu na hata aliwapa pesa za kufanya hivyo. Pia, aliwaagiza magavana wa eneo hilo wawasaidie.—Ezra 6:​1, 6-10.

7. Wayahudi waliorudi walipata baraka gani walipotanguliza kufanya mapenzi ya Mungu?

7 Kupitia Hagai na Zekaria, Yehova aliwaahidi watu wake kwamba angewasaidia ikiwa wangetanguliza kazi ya kujenga upya hekalu. (Hag. 1:​8, 13, 14; Zek. 1:​3, 16) Baada ya kutiwa moyo na manabii hao, Wayahudi waliorudi walianza tena kazi ya kujenga hekalu mwaka wa 520 K.W.K. na walikamilisha kazi hiyo kabla ya miaka mitano. Kwa kuwa Wayahudi walitanguliza kufanya mapenzi ya Mungu licha ya changamoto zisizotarajiwa, Yehova aliwasaidia kimwili na kiroho pia. Matokeo ni kwamba walimwabudu Yehova kwa shangwe.—Ezra 6:​14-16, 22.

KAZIA FIKIRA KUFANYA MAPENZI YA MUNGU

8. Maneno ya Hagai 2:4 yanawezaje kutusaidia kuendelea kukazia fikira kufanya mapenzi ya Mungu? (Tazama pia maelezo ya chini.)

8 Kwa kuwa dhiki kuu inakaribia, tunatambua jinsi ilivyo muhimu sana kutii amri ya kushiriki katika kazi ya kuhubiri. (Marko 13:10) Hata hivyo, huenda ikawa vigumu kukazia fikira huduma yetu ikiwa tunakabili hali ngumu ya kiuchumi au upinzani katika kazi yetu ya kuhubiri. Ni nini kitakachotusaidia kutanguliza masilahi ya Ufalme? Kuendelea kuwa na uhakika kwamba “Yehova wa majeshi”b yuko upande wetu. Atatutegemeza ikiwa tutaendelea kutanguliza masilahi ya Ufalme badala ya masilahi yetu. Hivyo, hatuhitaji kuogopa chochote.—Soma Hagai 2:4.

9-10. Wenzi wa ndoa fulani walijionea jinsi gani ukweli wa maneno ya Yesu kwenye Mathayo 6:33?

9 Fikiria mfano wa Oleg na Irina,c wenzi wa ndoa wanaotumikia wakiwa mapainia. Walipohamia eneo lingine ili kusaidia kutaniko lenye uhitaji, walipoteza kazi yao kwa sababu ya matatizo ya kiuchumi kwenye nchi yao. Ingawa kwa mwaka mmoja hivi hawakupata kazi ya kudumu, sikuzote walihisi utegemezo wenye upendo wa Yehova na pindi fulani walipata msaada kutoka kwa ndugu na dada. Walikabilianaje na changamoto hizo zisizotarajiwa? Oleg, ambaye mwanzoni alishuka moyo, anasema hivi: “Kuwa na mambo mengi ya kufanya katika huduma, kulitusaidia kukazia fikira mambo muhimu zaidi maishani.” Yeye na mke wake walipokuwa wakitafuta kazi, waliendelea kufanya utumishi kwa bidii.

10 Siku moja waliporudi kutoka katika huduma, waligundua kwamba rafiki yao wa karibu alikuwa amesafiri kilomita 160 hivi ili kuwaletea mifuko miwili ya bidhaa. Oleg anasema hivi: “Siku hiyo, kwa mara nyingine tena tulijionea jinsi Yehova na kutaniko linavyotujali sana. Tuna uhakika kwamba Yehova hawezi kamwe kuwasahau watumishi wake, hata wanapohisi kwamba hali haziwezi kubadilika.”—Mt. 6:33.

11. Tunaweza kutarajia nini tukiendelea kukazia fikira kufanya mapenzi ya Mungu?

11 Yehova anataka tukazie fikira kazi ya kufanya wanafunzi inayookoa uhai. Kama ilivyotajwa kwenye fungu la 7, Hagai aliwasihi watu wa Yehova waanze upya utumishi wao mtakatifu. Ikiwa wangefanya hivyo, Yehova aliahidi ‘kuwaletea baraka.’ (Hag. 2:​18, 19) Sisi pia tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atabariki jitihada zetu ikiwa tutanguliza kazi aliyotuagiza kufanya.

JINSI YA KUIMARISHA UHAKIKA WETU KATIKA YEHOVA

12. Kwa nini Ezra na Wayahudi wenzake walihitaji imani yenye nguvu?

12 Mwaka wa 468 K.W.K., Ezra alisafiri kutoka Babiloni kwenda Yerusalemu pamoja na kikundi cha pili cha Wayahudi. Ezra na Wayahudi wenzake walihitaji imani yenye nguvu ili kusafiri kwenda Yerusalemu. Walisafiri kwenye barabara zenye hatari, wakiwa wamebeba kiasi kikubwa cha dhahabu na fedha zilizotolewa kama mchango kwa ajili ya hekalu. Jambo hilo lingefanya iwe rahisi kushambuliwa na wanyang’anyi. (Ezra 7:​12-16; 8:31) Isitoshe, baada ya muda mfupi waligundua kwamba hata Yerusalemu hapakuwa na usalama. Kulikuwa na watu wachache walioishi katika jiji hilo, na kuta na malango yake yalihitaji marekebisho. Tunaweza kujifunza nini kutoka kwa Ezra kuhusu kuimarisha uhakika wetu katika Yehova?

13. Ezra aliimarishaje uhakika wake katika Yehova? (Tazama pia maelezo ya chini.)

13 Ezra alikuwa ameona jinsi Yehova alivyowategemeza watu Wake wakati wa majaribu. Miaka mingi mapema, mwaka wa 484 K.W.K., huenda Ezra alikuwa akiishi Babiloni wakati Mfalme Ahasuero alipotoa agizo la kuwaangamiza Wayahudi wote katika Milki ya Uajemi. (Esta 3:​7, 13-15) Uhai wa Ezra ulikuwa hatarini! Ili kukabiliana na tishio hilo, Wayahudi “katika kila mkoa” walifunga na kuomboleza, na bila shaka walisali kwa Yehova ili awapatie mwongozo. (Esta 4:3) Wazia jinsi Ezra na Wayahudi wenzake walivyohisi mambo yalipowageukia wale waliopanga njama ya kuwaangamiza Wayahudi! (Esta 9:​1, 2) Huenda mambo ambayo Ezra alijionea wakati huo mgumu yalimtayarisha kwa ajili ya majaribu ya wakati ujao na bila shaka yaliimarisha uhakika wake katika uwezo wa Yehova wa kuwalinda watu Wake.d

14. Dada mmoja alijifunza somo gani alipojionea utunzaji wa Yehova alipokabili changamoto zisizotarajiwa?

14 Tunapojionea jinsi Yehova anavyotujali tunapokabili changamoto zisizotarajiwa, ndivyo tunavyoimarisha uhakika wetu kwake. Fikiria mfano wa Anastasia, anayeishi Ulaya Mashariki. Aliacha kazi yake ili kutounga mkono upande wowote katika masuala ya kisiasa. Anasema hivi: “Hiyo ilikuwa mara ya kwanza maishani mwangu kutokuwa na pesa kabisa.” Kisha akaongezea kusema: “Niliacha mambo yote mikononi mwa Yehova, na nilijionea jinsi alivyonitunza kwa wororo. Nikipoteza tena kazi, sitaogopa. Ikiwa Baba yangu wa mbinguni ananitunza leo, atanitunza hata kesho.”

15. Ni nini kilichomsaidia Ezra kudumisha uhakika wake katika Yehova? (Ezra 7:​27, 28)

15 Ezra alijionea mkono wa Yehova katika maisha yake. Bila shaka, Ezra aliimarisha uhakika wake katika Yehova alipotafakari wakati ambapo alimsaidia. Fikiria maneno kama vile “mkono wa Yehova Mungu ulikuwa juu yangu.” (Soma Ezra 7:​27, 28.) Ezra alitumia msemo kama huo mara sita katika kitabu cha Biblia kinachoitwa kwa jina lake.—Ezra 7:​6, 9; 8:​18, 22, 31.

Ni katika hali gani tunaweza kuona waziwazi mkono wa Mungu katika maisha yetu? (Tazama fungu la 16)e

16. Ni katika hali gani tunaweza kujionea waziwazi mkono wa Yehova maishani mwetu? (Tazama pia picha.)

16 Yehova anaweza kutusaidia tunapokabili hali ngumu. Kwa mfano, tunapomwomba mwajiri wetu ruhusa ya kuhudhuria kusanyiko au tunapomwomba arekebishe ratiba ya kazi ili tuweze kuhudhuria mikutano yote, tunatengeneza fursa ya kujionea mkono wa Yehova katika maisha yetu. Huenda tukashangazwa sana na matokeo mazuri tutakayopata. Jambo hilo, litaimarisha uhakika wetu katika Yehova.

Ezra na Waisraeli wengine wakiomboleza hekaluni. Shekania akimsaidia Ezra kusimama.

Ezra akilia na kusali hekaluni kwa sababu ya kuhuzunishwa na dhambi za watu. Umati wa watu pia unalia. Shekania anamfariji Ezra kwa kumhakikishia hivi: “Bado kuna tumaini kwa Israeli. . . . Nasi tuko pamoja nawe.”​​—⁠Ezra 10:​2, 4 (Tazama fungu la 17)

17. Ezra alionyeshaje unyenyekevu alipokabili hali ngumu? (Tazama picha kwenye jalada.)

17 Kwa unyenyekevu, Ezra aliomba msaada wa Yehova. Ezra alisali kwa unyenyekevu kwa Yehova kila mara alipohisi amelemewa na majukumu yake. (Ezra 8:​21-23; 9:​3-5) Kwa kuwa Ezra alimtegemea Yehova, wengine walikuwa tayari kumtegemeza na kuiga imani yake. (Ezra 10:​1-4) Tunapolemewa na mahangaiko kuhusu mahitaji yetu ya kimwili au usalama wa familia yetu, tunapaswa kusali kwa Yehova tukiwa na uhakika.

18. Ni nini kinachoweza kutusaidia kuimarisha uhakika wetu katika Yehova?

18 Ikiwa kwa unyenyekevu tutatafuta msaada wa Yehova na kukubali utegemezo wa waabudu wenzetu, uhakika wetu kwa Mungu utaimarika. Erika, mama mwenye watoto watatu, alidumisha uhakika wake katika Yehova alipofiwa. Katika kipindi kifupi cha wakati, mtoto wake alifia tumboni na pia alifiwa na mume wake mpendwa. Anapokumbuka kipindi hicho, anasema hivi: “Huwezi kujua mapema jinsi Yehova atakavyokusaidia. Msaada unaweza kuja kwa njia usizotarajia. Nimejionea kwamba sala zangu nyingi zimejibiwa kupitia maneno na matendo ya rafiki zangu. Ninapowaambia rafiki zangu mambo ninayokabili, wanaweza kunisaidia vizuri zaidi.”

DUMISHA UHAKIKA WAKO KATIKA YEHOVA HADI MWISHO

19-20. Tunajifunza nini kutokana na Wayahudi ambao hawakurudi Yerusalemu?

19 Tunaweza kujifunza pia somo muhimu kutokana na Wayahudi ambao hawakurudi Yerusalemu. Huenda baadhi yao walishindwa kurudi kwa sababu ya umri, matatizo makubwa ya afya, au majukumu katika familia. Hata hivyo, kwa hiari walitoa michango ili kuwategemeza waliorudi. (Ezra 1:​5, 6) Inaonekana kwamba miaka 19 hivi baada ya kikundi cha kwanza kuwasili Yerusalemu, wale waliobaki Babiloni walikuwa wakiendelea kutuma michango ya hiari kwenda Yerusalemu.—Zek. 6:10.

20 Hata ikiwa tunahisi hatuwezi kufanya yote tunayotamani katika utumishi wa Mungu, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova anathamini yote tunayofanya kutoka moyoni ili kumfurahisha. Tunajuaje hilo? Katika siku za Zekaria, Yehova alimwomba nabii huyo atengeneze taji kutokana na dhahabu na fedha iliyotolewa na Wayahudi waliokuwa uhamishoni Babiloni. (Zek. 6:11) “Taji lenye utukufu” lilikuwa “ukumbusho” wa michango yao ya ukarimu. (Zek. 6:​14, maelezo ya chini) Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova hatasahau jitihada zetu za kumtumikia kutoka moyoni, tunapokabili changamoto zisizotarajiwa.—Ebr. 6:10.

21. Ni nini kitakachotusaidia kukabili wakati ujao tukiwa na uhakika?

21 Bila shaka, tutaendelea kukabili changamoto zisizotarajiwa katika siku hizi za mwisho, na huenda hali zikawa mbaya zaidi wakati ujao. (2 Tim. 3:​1, 13) Hata hivyo, hatuhitaji kulemewa na mahangaiko. Kumbuka maneno ambayo Yehova aliwaambia watu wake katika siku za Hagai: “Niko pamoja nanyi . . . Msiogope.” (Hag. 2:​4, 5) Sisi pia tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atakuwa pamoja nasi tukijitahidi kadiri tuwezavyo kufanya mapenzi yake. Tukitumia mambo tuliyojifunza kutoka katika unabii wa Hagai na Zekaria na mfano wa Ezra, tutadumisha uhakika wetu katika Yehova hata tukikabili changamoto zisizotarajiwa wakati ujao.

UNGEJIBUJE?

  • Changamoto zisizotarajiwa zinaweza kuathirije utumishi wetu kwa Yehova?

  • Kwa nini tunapaswa kukazia fikira kufanya mapenzi ya Mungu licha ya changamoto zisizotarajiwa?

  • Tunawezaje kuimarisha uhakika wetu katika Yehova tunapokabili hali ngumu?

WIMBO 122 Iweni Imara, Thabiti!

a Makala hii imetayarishwa ili kutusaidia kuimarisha uhakika wetu katika Yehova tunapokabili hali ngumu za kiuchumi, misukosuko ya kisiasa, au upinzani katika kazi yetu ya kuhubiri.

b Msemo “Yehova wa majeshi” hutokea mara 14 katika kitabu cha Hagai. Uliwakumbusha Wayahudi na unatukumbusha sisi pia kwamba Yehova ana nguvu zisizo na mipaka na ana mamlaka juu ya majeshi makubwa ya malaika.—Zab. 103:​20, 21.

c Baadhi ya majina yamebadilishwa.

d Ezra, alikuwa mwandishi stadi wa Sheria ya Mungu, pia alisitawisha uhakika wenye nguvu katika unabii wa Yehova hata kabla ya kusafiri kwenda Yerusalemu.—2 Nya. 36:​22, 23; Ezra 7:​6, 9, 10; Yer. 29:14.

e MAELEZO YA PICHA: Ndugu anamwomba mwajiri wake ruhusa ya kuhudhuria kusanyiko, lakini mwajiri anakataa. Anamwomba Yehova msaada na mwongozo anapojitayarisha kumwona tena mwajiri wake. Anamwonyesha mwajiri wake mwaliko wa kusanyiko, na kumweleza umuhimu wa elimu ya Biblia. Mwajiri wake anafurahishwa na jambo hilo na kumruhusu aende.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki